Na Albano Midelo
KANISA katoliki jimbo
kuu la Songea limepata pigo kubwa baada ya kufariki mfululizo mapadre watatu na
mabruda wawili katika kipindi
kisichozidi siku 10 .
Vifo hivyo ambavyo vimezua maswali kwa waumini vimewakuta
mapadri watatu kutoka parokia za
Matogoro,Njombe na Mbinga na
mabruda wawili wote kutoka Abasia ya Hanga.
Mwezi Juni mwaka 2012 hautasahaulika na waumini wa jimbo kuu
la Songea kutokana na matukio hayo ya vifo ambavyo vilianza Juni 16 ambapo
Abasia ya Hanga ilimpoteza bruda Markusi Nchimbi OSB ambaye alifia Kurasini jijini Dar es salaam
kutokana na maradhi na kuzikwa Juni 20 katika Abasia ya Hanga.
Siku moja baada ya kifo cha Bruda huyo yaani Juni 17 jimbo
kuu la Songea lilipata pigo jingine baada ya kifo cha padre Alfonsi Mapunda
ambaye alikuwa paroko msaidizi wa parokia ya Matogoro ambacho kilitokea katika hospitali ya KCMC
mjini Moshi na kufuatiwa na misa
takatifu ya mazishi iliyofanyika Juni 21
kwenye makaburi ya mapadre parokia ya Matogoro mjini hapa.
Vifo vya watawa viliendelea na kuwaweka waumini katika wakati mgumu ambapo
Juni 20 padre Gabriel Mwilongo aliyekuwa
mkurugenzi katika ofisi ya Caritas jimbo la Njombe alifariki baada ya
kusumbuliwa na shida kubwa ya shinikizo la damu ya kushuka na kuzikwa Juni 22 mwaka
huu jimboni humo.
Juni 20 ilikuwa ni siku mbaya katika jimbo kuu la Songea kwa
kuwa baada ya kifo cha padre Mwilongo,siku hiyo Bruda Paschal Mkalawa OSB
alifariki dunia katika hospitali ya misheni Peramiho kutokana na maradhi na
kuzikwa katika makaburi ya Abasia ya Hanga Juni 22 mwaka huu.
Katika hali ya kukatisha tamaa waumini wa jimbo kuu la Songea
walipata msiba mwingine wa padre John Nchimbi ambaye alikuwa ni mkuu wa chuo
cha ufundi Mbinga ambaye alipoteza
maisha Juni 22 katika ajali ya gari iliyotokea katika kijiji cha Likalangilo
wilayani Songea.
Marehemu padre Nchimbi alikuwa na watawa wenzake katika gari
dogo wakitokea Njombe kwenye mazishi ya padre Gabriel Mwilongo hivyo majira ya
saa mbili usiku walipata ajali ya gari lao kugongana na gari kubwa la mizigo na
kusababisha kifo cha padre huyo ambaye amezikwa parokia ya Kigonsera.
Historia ya maisha ya marehemu padre Alfonsi Mapunda
iliyotolewa na Askofu mkuu Norbert Mtega siku ya mazishi yake katika parokia ya
Matogoro inaonesha kuwa alizaliwa katika kijiji cha Ndumbi wilayani Nyasa
mkoani Ruvuma mwaka 1944,alipokea sacramenti ya ubatizo mwaka 1945,komunyo ya
kwanza 1952 na kipaimara mwaka 1954 katika kanisa la Lituhi.
Padre Mapunda alimaliza elimu ya msingi mwaka 1956 ,alijiunga
na seminari ndogo ya Kigonsera mwaka 1957 kisha kumaliza kidato cha nne katika
seminari ndogo ya Likonde na mwaka 1966 alijiunga na seminari kuu Peramiho kwa
masomo ya falsafa na teolojia.
Historia hiyo inaonesha kuwa marehemu padre Mapunda alipata
ushemasi mdogo mwaka 1971 ,alipokea daraja takatifu la upadre mwaka 1972 ambapo
tangu wakati huo ametumwa sehemu mbalimbali kuwa paroko msaidizi na
paroko,mlezi wa sekondari ya Kigonsera na mwaka 1979 alitumwa nchini Ujerumani
kujifunza malezi ya vijana .
Tangu Novemba mwaka 1993 hadi kifo chake marehemu padre
Alfonsi Mapunda alikuwa paroko msaidizi
wa parokia ya Matogoro ambapo
alijishughulisha kikamilifu kuwasaidia waumini
wa dini zote kimwili na kiroho hali iliyosababisha waumini wa dini zote
kumtumia kikamilifu.
Padre Mapunda kwa takriban miaka zaidi ya 20 alikuwa na tatizo la ugonjwa wa mifupa ya uti wa mgongo
na mishipa ya fahamu ambayo ametiwa hospitali ya Muhimbili,Ulaya na hatimaye
KCMC .
Kwa upande wake Askofu Alfred Maluma wa jimbo katoliki la
Njombe akitoa historia ya marehemu padre Gabriel Mwilongo alieleza kuwa Padre Gabriel
Mwilongo alizaliwa Igwachanya, Oktoba 19, 1962, Alipata Sakramenti ya
Ubatizo Oktoba 28, 1962, alipewa Sakramenti za Komunyo ya Kwanza mwaka 1972 na
Kipaimara 1972.
Alipata elimu ya Msingi ya kuhitimu darasa la saba mwaka 1980 katika
shule ya msingi Igwachanya, Kuanzia 1981 hadi 1987 alipata elimu ya Sekondari
Kidato cha kwanza hadi cha sita katika Seminari ya Mt. Kizito, Mafinga.
Baadaye alijiunga na Seminari Kuu ya Mt.
Augustino, Peramiho kwa masomo ya Falsafa (1987 - 1989) na Teolojia
(1989-1993). Siku ya Juni 14, 1992, Padre Gabriel alipewa Daraja Takatifu ya
Ushemasi na Mhashamu Baba Askofu Mkuu Norbert Mtega katika Kanisa Kuu la
Kiaskofu Njombe.
Julai 4, 1993
alipewa Daraja Takatifu ya Upadre na Mhashamu Baba Askofu Raymond
Mwanyika katika Kanisa la Watakatifu Malaika Wakuu.
Marehemu padre Mwilongo katika uhai
wake alitumwa kuwa paroko msaidizi katika parokia za Luilo, Mundindi na kwamba 1999 hadi mwaka huu 2012 alikuwa Mkurugenzi katika
Ofisi ya Caritas Jimbo la Njombe na
Mwenyekiti wa Caritas Kanda ya Kusini
(SHICANET – Southern Highlands Caritas
Network).
Tangu mwaka 2003 Padre Gabriel
aliwahi kupata shida ya shinikizo la damu ambapo Jimbo lilimsaidia kupata
matibabu katika hospitali za hapa nchini na baadaye alipelekwa nchini Italia
kwa uchunguzi zaidi. Baadaye alipata nafuu
na kuendelea na kazi kama kawaida.
Hata hivyo Juni 19 mwaka huu
aligundulika kuwa na shida
kubwa ya shinikizo la damu la kushuka na kumsababishia mauti yake Juni 20.
albano.midelo@gmail.com

No comments:
Post a Comment