Sunday, February 17, 2013

Ruvuma:Nusu ya wanafunzi hawajaripoti sekondari


Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu

 Na Albano Midelo
KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida karibu nusu tu ya wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mkoani Ruvuma mwaka huu hawajaripoti katika shule za sekondari ambazo zimefikia 179.
Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Thabiti Mwambungu amesema jumla ya wanafunzi waliochaguliwa katika mkoa mzima kujiunga na kidato cha kwanza mwaka huu walikuwa ni zaidi ya 16,000 lakini hadi sasa walioripoti ni wanafunzi zaidi ya 9000 idadi ambayo ni karibu nusu tu ya wanafunzi.
Uchunguzi ambao umefanywa katika Halmashauri zote tano za mkoa wa Ruvuma  kwa wanafunzi walioripoti shuleni baada ya  kuchaguliwa kidato cha kwanza hadi kufikia Februari 13,2013 unaonyesha kuwa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga ilipangiwa wanafunzi 5988 walioripoti 3606,wasioripoti 2382 sawa na asilimia 60.2.

Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo waliopangwa ni wanafunzi 2410,walioripoti 1432,wasioripoti 978 sawa na asilimia 59.4,Songea manispaa waliopangwa 3274,walioripoti 1983 wasioripoti 1291 sawa na asilimia 61,Songea vijijini waliopangiwa 2118,waliripoti 1308,wasioripoti 810 sawa na asilimia 61.76 na Tunduru waliopangiwa ni 2788,walioripoti 1059,wasioripoti 1729 sawa na asilimia 38.
Uchunguzi huo umebaini katika shule nyingi wanafunzi walioripoti wameshindwa hata kufikia nusu ya wanafunzi waliopangiwa kwa mfano katika sekondari ya  Chandarua iliyopo manispaa ya Songea wanafunzi walioripoti ni 62 kati ya wanafunzi 132 waliopangiwa,shule ya sekondari ya Barabarani iliyopo katika Halmashauri ya wilaya ya Songea wanafunzi wawili tu ndiyo wameripoti kati ya wanafunzi 23 waliopangiwa.
Kulingana na uchunguzi huo katika shule ya sekondari Gumbiro iliyopo Halmashauri ya wilaya ya Songea wanafunzi walioripoti ni 31 kati ya wanafunzi 101 waliopangiwa katika shule hiyo na sekondari ya Nguluma wanafunzi walioripoti ni 54 kati ya wanafunzi 144 waliopangiwa.
Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo  katika sekondari ya Magazini wanafunzi walioripoti ni 62 kati ya wanafunzi 145 waliopangiwa,sekondari ya Sasawala wanafunzi walioripoti ni 62 kati ya wanafunzi 145 waliopangiwa,sekondari ya Mpunga wanafunzi waliopangiwa ni 148 lakini walioripoti ni 48 na sendari ya Nasuli wanafunzi walioripoti ni 131 kati ya wanafunzi 204 waliopangiwa.
Uchunguzi uliofanywa katika Halmashauri ya wilaya ya Tunduru umebaini kuwa katika sekondari ya Marumba wanafunzi walioripoti ni 10 tu kati ya wanafunzi 148 waliopangiwa,sekondari ya Mtutura walioripoti ni 22 kati ya wanafunzi 159 waliopangiwa,sekondari ya Namwinyu walioripoti ni 14 kati ya wanafunzi 109 waliopangiwa na sekondari ya Semeni walioripoti ni 20 kati ya 135 waliopangiwa.
“Idadi hii wanafunzi walioripoti ndogo sana na imenishitua mimi na wenzangu  hivyo inatakiwa kuchukuliwa hatua za haraka  kwa nafasi hii naagiza wazazi na walezi ambao bado watoto wao hawajaripoti hadi kufikia Machi mosi mwaka huu  wahakikishe kuwa wanawapeleka watoto wao shuleni hawana sababu za msingi za kutowapeleka shuleni’’,alisema mkuu wa mkoa wa Ruvuma.
Mwambungu amewaagiza wakuu wa wilaya zote mkoani Ruvuma,wakurugenzi,watendaji wa vijiji,vitongoji,kata,mitaa na watendaji wengine kuanza kuwachukulia hatua wazazi na walezi wote ambao watashindwa kuwapeleka watoto wao waliochaguliwa katika sekondari walizopangiwa.
Baadhi ya wazazi na walezi wakiwemo Adamu Nindi, AshuraRajabu, Stella Komba na John Hyera wamedai kuwa moja ya sababu kubwa ambayo inachangia wazazi kushindwa kuwapeleka wanafunzi shuleni ni michango iliyokidhiri katika shule za sekondari za kata ambayo baadhi ya shule inafikia zaidi ya 300,000 .
“Wazazi na walezi walio wengi ni masikini wanashindwa kumudu michango hiyo,ni kweli ada kwa mwaka katika sekondari za kata ni shilingi 20,000 lakini michango ndiyo kikwazo kwa wazazi wengi ambao baadhi yao wanasomesha watoto hadi watatu hivyo wanashindwa kumudu kulipa hivyo wanafunzi wanashindwa kupelekwa shuleni’’,alisema Adamu Nindi mzazi anayesomesha watoto wawili.

No comments:

Post a Comment