Monday, May 13, 2013

Mvua yaizamisha Mbambabay,mmoja afariki



Meli ya  Mv.Songea imetia nanga bandari ya Mbambabay Nyasa

Na Albano Midelo

MVUA kubwa ambayo imenyesha kwa  saa nne mfululizo kata ya Mbambabay wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma imesababisha kifo cha mtu mmoja na kuleta uharibifu mkubwa wa mali.

Mtu aliyefariki dunia baada ya kusombwa na maji  ametambulika kwa jina la Albat Likeli(70) aliyekuwa mkazi wa kijiji cha Ndengele kata ya Mbambabay wilayani Nyasa mkoani Ruvuma.

Mkuu wa wilaya ya Nyasa Erenest Kahindi ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama amethibitisha mvua iliyonyesha hivi karibuni imeleta madhara makubwa yakiwemo kifo na uharibifu mkubwa wa mali za watu.

Kulingana na mkuu huyo wa wilaya mvua hiyo imeleta madhara makubwa ya uharibifu wa mali katika vijiji vya Ndengele,Kilosa,Lundo na Mbambabay ambayo ni makao makuu ya wilaya ya Nyasa.


“Mvua hii ilisababisha  kujaa maji katika ujazo wa mita moja na nusu kutoka usawa wa ardhi katika mji wa Mbambabay hali iliyosababisha nyumba katika vijiji vilivyoathirika kujaa maji, imeharibu ekari zaidi ya 45 za zao la muhogo katika kijiji cha Kilosa pamoja na zao la mpunga’’,alisisitiza.

Athari nyingine ambazo zimeletwa na mvua hizo ni ng’ombe saba wamekufa maji,madarasa mawili ya shule za msingi yamesombwa na maji na kwamba hivi sasa hakuna mawasiliano ya barabara kati ya makao makuu ya wilaya Mbambabay na kata za Liuli hadi Lituhi baada ya daraja la mto Mbawa kusombwa na maji.

Mkuu wa wilaya ya Nyasa amelipongeza jeshi la polisi katika mji wa Mbambabay kufanikiwa kuwaokoa watoto watatu wasiojiweza waliokolewa wakiwa wanaelea juu ya maji ya mafuriko ya mvua,hata hivyo majina ya watoto hao hayakuweza kufahamika mara moja.

Wakati huo huo mafuriko hayo katika mji wa Mbambabay yamesababisha mamba mmoja kutoka ziwa Nyasa kusafiri hadi katikati ya mji wa Mbambabay akifuata maji ya mafuriko ambapo baada ya maji kukauka amebakia katikati ya dimbwi la maji lililopo katikati ya mji huo na kuzua wasiwasi mkubwa kwa wakazi wa mji huo.

Hata hivyo mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ambaye pia ni mkuu wa wilaya ya Nyasa Erenest Kahindi  amesema taratibu za kumuua mamba huyo zinafanyika hivyo amewaomba wananchi kuwa watulivu.

Victor Komba mkazi wa kijiji cha Liuli ametoa lawama kwa wakala wa barabara mkoa wa Ruvuma kuwa wanachangia kila mwaka kuleta usumbufu kwa wakazi wa mwambao mwa ziwa Nyasa kwa kuwa msimu wa mvua barabara zinapomoka na madaraja yamekuwa yanasombwa na maji ya mvua.

“Madaraja yanajengwa chini ya viwango ndiyo maana yanasombwa na maji,hata barabara zinajengwa chini ya viwango,nani anawasimamia makandarasi wanaojenga miundombinu hii kama ina ubora unaotakiwa,  je makandarasi wanaopewa tenda wana sifa? lawama zote tunazipeleka kwa TANROADS sasa hatuna mawasiliano na makao makuu ya wilaya’’,alisisitiza.

Hata hivyo meneja wa wakala wa barabara mkoa wa Ruvuma TANROADS injinia Abrahamu Kisimbo hakuweza kupatikana mara moja kuzungumzia tuhuma dhidi ya TANROADS na  lini ujenzi wa daraja la Mbawa linalounganisha Mbambabay na miji midogo ya Liuli na Lituhi utaanza ili kumaliza kero ambayo wakazi wa maeneo hayo wanaipata hivi sasa.

Miongoni mwa kero ambazo wanazipata wakazi wa maeneo hayo ni gharama za usafirishaji kuongezeka kwa kuwa mabasi na magari yanaishia katika daraja la mto Mbawa lililobomoka hivyo inawalazimu kulipa gharama nyingine ili waweze kuendelea na safari hadi kufika kwenye makazi yao.

Mabasi ya abiria na magari mengine yanaishia katika eneo la daraja la Mbawa na kuanzia hapa ili kumaliza safari hadi Liuli inakulazimu kuingia gharama nyingine zikiwemo kukodi pikipiki na magari  hali ambayo inaleta usumbufu mkubwa kwa wananchi wasiokuwa na uwezo kutembea kwa mguu karibu kilometa 25 hadi Liuli.

Mary Challe mkazi wa Liuli anasema kutoka Songea hadi Liuli kabla ya kusombwa kwa daraja hilo nauli ya mabasi ilikuwa ni sh.12,000 ambapo hivi sasa inawalazimu kutumia hadi sh.20,000 na kwamba endapo unakuwa na mizigo mingi inakulazimu kutumia gharama kubwa zaidi kukodi vyombo vya usafiri.



1 comment:

  1. Asante kwa taarifa hii ya kina na natoa pole kwa waathirika. Endapo utafanyika utaratibu wa kuwapelekea michango, itakuwa vema ukituwekea hizo taarifa.

    ReplyDelete