Wednesday, September 7, 2011

VETA Songea kutumia milioni 100 kujenga mabweni


  



Na Albano Midelo
CHUO cha ufundi stadi VETA kilichopo katika Halmashauri ya manispaa ya Songea mkoani Ruvuma kinatarajia kujenga mabweni nane ya kulala wanachuo yatakayogharimu kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 100.
Kauli hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki na mkuu wa chuo hicho Gideon Ole Lairumbe wakati akizungumza na gazeti hili ofisini kwake mjini hapa
Alifafanua kuwa mabweni hayo yatatumika kwa ajili ya kulala wanachuo wanaotoka mbali na Songea kwa lengo la kuwapunguzia umbali mrefu na usalama kwa wanachuo wa kike.
Mbali na hilo aliyataja matarajio mengine ya chuo hicho kuwa ni ujenzi wa ukumbi wa mikutano ,nyumba za watumishi,vyumba vya madarasa na utengenezaji wa viwanja mbalimbali vya michezo.
Aliongeza kuwa chuo cha VETA kina mpango wa kuanzisha kozi mpya ya uzalishaji wa chakula yaani food production pamoja na  kutoa mafunzo kwa ajili  mafundi vinyozi na wasusi wa nywele kwa akinamama.
VETA Songea imekuwa mstari wa mbele katika kuwajengea uwezo vijana katika fani  mbalimbali ikiwemo umeme wa majumba, ushonaji, useremala, uungaji vyuma, uashi, ufundi magari, umeme wa magari, uhadhili na kompyuta kwa wanafunzi wa kozi ndefu jambo ambalo limepunguza udhururaji na kuepuka vitendo viovu.
Changamoto zinazokikabili chuo hicho kwa mujibu wa mkuu huyo wa chuo ni pamoja na ukosefu wa sehemu ya kufanyia mazoezi ya vitendo,
 na mtazamo hasi kwa jamii kwamba vijana wanaosoma VETA ni wale walioshindwa kuendelea na elimu ya juu.
Ametoa wito kwa wamiliki wa viwanda kuwapokea vijana hao pindi wanapotafuta ajira na kusisitiza kwa wazazi na walezi kuwapeleka vijana wao kwenye chuo hicho ili kuongeza ujuzi zaidi.
Kwa mawasiliano albano .midelo@gmail.com
 

No comments:

Post a Comment