Wednesday, March 14, 2012

Hali ya amani yarejea Songea

 Pichani mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu.
 
Na Albano Midelo
HALI ya amani na usalama imerejea katika mji wa Songea baada ya serikali kwa kushirikiana na wananchi kudhibiti mauaji ya watu yaliokuwa yanafanyika kwa mfululizo na kuleta hofu .
Tangu mwanzoni mwa mwaka huu yamekuwa yakitokea mauaji mfululizo ya watu ambayo yalidaiwa yanatokana  na imani za kishirikina ambayo yamesababisha vifo vya watu 14 hali ambayo ilizua hofu na mashaka kwa wakazi wa mji wa Songea.


Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Thabit Mwambungu wiki hii amezungumza  na waandishi wa habari ofisini amesisitiza kuwa mji wa Songea  sasa umerejea katika hali amani na utulivu na  kwamba hakuna tena matukio ya mauaji tangu .
“Serikali imefanikiwa kuwakamata karibu watuhumiwa wote waliohusika na mauaji yaliyosababisha vifo vya watu 14 na hivi sasa watuhumiwa hao wakiwemo askari wanaotuhumiwa kuuwa watu wawili kwa risasi kwenye maandamano wapo mbele ya vyombo vya sheria na upelelezi zaidi unaendelea’’,alisisitiza.
 Amewatahadharisha wananchi kuacha kujichukulia sheria mkononi  pamoja na kuacha kufanya maandamano yasiokuwa ya vibali kwa kuwa yanachangia kuleta ghasia na uvunjifu wa amani ambao unaleta athari na kwamba wanapokuwa na malalamiko au kero wazifikisha kwa viongozi wao kwa njia halali.
Hata hivyo uchunguzi ambao umefanywa na gazeti hili katika viunga mbalimbali vya mji wa Songea umebaini kuwa licha ya mkuu wa mkoa kudai hali ya amani na utulivu imerejea,bado wananchi wengi wanaishi kwa hofu na mashaka kuhofia usalama wao.
Mohamed Kudeka ni mkazi wa Msamala mjini hapa anadai kuwa  wakazi wa eneo hilo bado wanaogopa kwenda kuweka mbolea na kufanya palizi kwenye mashamba yao kuhofia kuuwawa na kwamba mashamba mengi ya mahindi  yamedumaa  kwa kukosa matunzo.
Hamza Abdalah mkazi wa Matarawe anadai kuwa  nguvu ya wananchi kufanya maandamano ingawa hayakuwa halali  imesaidia kuiamsha serikali kufufua ulinzi shirikishi kwenye mitaa yote ya mji wa Songea na kwamba amani na utulivu iliyozoeleka katika mji wa Songea bado haujarudi katika hali yake ya kawaida.
“Baadhi ya maeneo klabu za  usiku zinafungwa kabla ya saa tatu usiku mfano maeneo ya Mkuzo,Matarawe,Ruhuwiko,maeneo ya katikati ya mji klabu za usiku kama Ikweta,   zinaendelea kutoa huduma zaidi ya saa tano usiku,hata hivyo wateja ni wachache ukilinganisha na hali kabla matukio ya mauaji’’,alisema Abdalah.
Madereva pikipiki waliohojiwa Rashid Juma,John Komba,Frank Haule,Hamis Rajabu na Musa Ngongi walidai kuwa hawakubali kuwabeba abiria wasiwafamu vizuri majira ya mchana na usiku kutoka katikati ya mji kuelekea pembezoni kwa sababu bado wana hofu kuporwa pikipiki na usalama wa maisha yao.
Mkuu wa wilaya ya Songea Thomas Sabaya alisema serikali imejipanga kila kata katika mji wa Songea kuwatafutia sare maalum madereva wote wa pikipiki ili kuwatambua maeneo wanayotoka  hali ambayo itasaidia kuzuia uharifu unaofanywa na baadhi ya madereva wa pikipiki au abiria wanaowabeba.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:

Post a Comment