![]() |
Na Albano Midelo
KLABU ya waandishi wa habari mkoa wa Ruvuma imejipatia
viongozi wake wapya ambao wataiongoza klabu hiyo katika kipindi cha miaka mitatu
ijayo.
Viongozi hao wapya
wamechaguliwa kwenye mkutano mkuu wa uchaguzi uliofanyika kwenye ukumbi wa EMAU
Peramiho nje kidogo ya mji wa Songea na kusimamiwa na mwakilishi wa mkuu wa
wilaya ya Songea Richard Mbambe.
Waliochaguliwa kwenye
uchaguzi huo ni pamoja na mwenyekiti Andrew Kuchonjoma,makamu mwenyekiti
Leticia Nyoni,katibu mkuu Andrew Chatwanga na katibu mkuu msaidizi amechaguliwa
kuwa ni Julius Konala.
Akizungumza mara
baada ya kuchaguliwa mwenyekiti mteule Andrew Kuchonjoma ameahidi kuendelea
kuimarisha umoja na mshikamano wa wanachama na kuepusha migogoro ambayo
imechangia kurudisha nyuma maendeleo ya klabu hiyo.
“Ndugu wanachama
katika kipindi cha miaka mitatu ijayo kwa kushirikiana na viongozi wenzangu
naahidi kuleta mabadiliko makubwa ndani ya klabu yetu,ikiwemo kuanzisha mradi
wa redio yetu ya klabu’’,alisisitiza.
Kwa upande wake
makamu mwenyekiti Leticia Nyoni aliahidi kushirikiana na wanachama wote na hasa
kusukuma maendeleo kwa waandishi wa habari wanawake waweze kujiunga kwenye
klabu hiyo na kuleta maendeleo kwa kuwa mwanamke ni nguzo ya familia.
Katibu mkuu wa klabu
hiyo Andrew Chatwanga aliyataja
matarajio katika kipindi cha miaka mitatu ijayo kuwa licha ya kuanzisha redio
,pia wanatarajia kuanzisha kitega uchumi cha kudumu vikiwemo nyumba ya kulala
wageni na mashamba.
Matarajio mengine
aliyataja kuwa ni kutafuta wafadhili watakaosaidia wanachama wa klabu hiyo
kupata mafunzo ya muda mfupi na mrefu yatakayofanyika ndani na nje ya mkoa kwa
lengo la kuwajengea uwezo waandishi ili waweze kukabiliana na mabadiliko
yanayotokea katika nyanja mbalimbali.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:
Post a Comment