Thursday, April 5, 2012

Ukombozi Saccos yatoa mamilioni kwa wanachama


  
Na Albano Midelo
CHAMA cha ushirika wa akiba na mikopo cha Ukombozi saccos kilichopo jimbo kuu katoliki la Songea kimewakopesha wanachama wake 977 mkopo wenye thamani ya shilingi milioni 552.5 mwaka 2011.
Hayo  yalisemwa na meneja wa saccos hiyo Rainery Ngatunga wakati anasoma taarifa ya  chama chake kwenye mkutano mkuu wa nane uliofanyika kwenye ukumbi wa Centenary mjini hapa.
Alibainisha kuwa mkopo huo ulitolewa kwa wanachama kwa ajili ya kilimo,mifugo,elimu,afya,ujenzi wa nyumba na biashara na kwamba lengo lilikuwa kutoa mkopo wa
shilingi milioni 470 katika kipindi cha kuanzia mwezi Januari hadi Desemba mwaka jana.
Kulingana na meneja huyo hadi  Desemba 31 mwaka jana chama hicho  kilikuwa na Hisa zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 26,amana milioni 43.3 na akiba  zaidi ya shilingi milioni 400.
Naye mwenyekiti wa Ukombozi saccos Gerald Chabruma alisema saccos hiyo tangu kuanzishwa kwake imepata mafanikio makubwa  yakiwemo kutoa mkopo wa zaidi ya shilingi bilioni moja  na kununua gari  lenye thamani ya shilingi milioni 15.
Hata hivyo Chabruma ameyataja matarajio ya saccos hiyo mwaka huu kuwa ni pamoja na kuongeza Hisa kutoka  milioni 26 hadi milioni 32,akiba kutoka milioni 400 hadi milioni 500 na amana kutoka milioni  43 hadi 50 na mikopo kutoka milioni  552 hadi 600.
Mgeni rasmi katika mkutano mkuu huo, mama mkubwa wa jamii ya masista wa mtakatifu Agnes Chipole Sr.Subira Mhowela OSB amewahimiza wanachama hao kukopa kwa malengo  badala ya kuitumia mikopo hiyo kwa kufanya starehe na anasa.
Ukombozi saccos ambayo ilianzishwa mwaka 2004 ikiwa na wanachama 49, hivi sasa saccos hiyo idadi ya wanachama imeongezeka hadi kufikia 977.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:

Post a Comment