Saturday, March 3, 2012

Marejea mbolea inajibu dhana ya kilimo kwanza


  


 Na Albano Midelo
 Hakuna ubishi kuwa Tanzania ni nchi  inayojihusisha zaidi katika kilimo kwa kuzingatia mchango mkubwa unaotolewa kupitia sekta hiyo katika uchumi wa taifa hali ambayo imefanya kilimo kuitwa uti wa  mgongo na hivi sasa kuna kauli ambayo inasema kilimo kwanza.

Takwimu za kitaifa zinaonesha kilimo kinachangia asilimia  26.7 ya pato la taifa ,asilimia 95 ya pato la chakula kinachotumika nchini ,asilimia 30 ya mauzo ya nje na kilimo kinachangia asilimia 65 ya malighafi zinazotumika katika viwanda vya ndani.


Kilimo ni mwajiri mkuu wa watanzania kutokana na takwimu kuonesha kuwa asilimia 80 ya watanzania wote wamejiajiri katika sekta ya kilimo.Kwa ujumla ili Tanzania uweze kufikia malengo yake ya maendeleo sekta ya kilimo inatakiwa ikue kutoka asilimia nne hivi sasa angalau ifikie asilimia 10 ndiyo maana serikali iliamua kuanzisha dhana ya kilimo kwanza.

Serikali ya awamu  ya nne ambayo inaongozwa na Rais Jakaya Kikwete kwa kushirikiana na waziri mkuu Mizengo Pinda mtoto wa mkulima inafanya juhudi za makusudi kuhakikisha kuwa yanafanyika mapinduzi ya kilimo kwa kutoa ruzuku katika pembejeo na kuhakikisha wakulima wanaondokana na jembe la mkono na sasa wanaingia katika kilimo cha wanyamakazi pamoja na matumizi ya trekta dogo yaani powertiller.

 Pamoja na juhudi hizo kuchukuliwa bado sekta ya kilimo inaonekana inakabiliwa na changamoto nyingi zikiwemo idadi kubwa ya wakulima kuendelea kutumia jembe la mkono,bei ya mbolea bado ipo juu licha ya serikali kutoa ruzuku ya pembejeo pamoja na ukosefu wa soko la uhakika kwa wakulima wanapovuna mazao yao.

 Serikali kila mwaka imekuwa ikijitahidi kutoa mbolea ya ruzuku kwa wakulima ili kupunguza makali ya bei ya mbolea ambapo utafiti unaonesha kuwa mbolea  ya ruzuku bado sio msaada kwa wakulima wadogo wadogo kwa kuwa bei ya ruzuku bado ipo juu ukilinganisha na uwezo wa wananchi walio wengi wenye kipato chini ,ni idadi ndogo sana ya wakulima ambao wanapata fursa ya kupata mbolea ya ruzuku hivyo wengi wanashindwa kumudu kununua.

Mbolea ya ruzuku pia inakabiliwa na tatizo sugu la mawakala  wasiokuwa waaminifu kwa kushirikiana na baadhi ya viongozi wa serikali katika ngazi mbalimbali wanasababisha idadi kubwa ya wakulima kushindwa kupata mbolea hiyo kutokana na kufanya ufisadi wa waziwazi hali ambayo inasababisha wakulima wengi vijijini kushindwa kupata mbolea ya ruzuku.

  Pamoja na kwamba wakulima kila mwaka wanajitahidi kulima mazao kwa gharama  kubwa ya pembejeo,bado hakuna soko la uhakika ya mazao yao kwa mfano mwaka huu mikoa inayozalisha mahindi kwa wingi kama Ruvuma  na Rukwa wakulima walipata hasara hali inayosababisha walanguzi wa mazao kununua kwa bei ndogo kwa wakulima kwa kutumia vipimo batili na hivyo kuwanyonya wakulima.

Mkoa wa Ruvuma ni miongoni mwa mikoa inayoongoza kwa uzalishaji wa mazao ya chakula mikoa mingine  ni   Rukwa,Mbeya,Iringa pia serikali imeingiza mikoa ya Morogoro na Kigoma hivyo kufanya ni mikoa sita  itakayopewa kipaumbele katika uzalishaji wa mazao ya chakula nchini .

Hata hivyo uchunguzi umebaini kuwa tatizo la kutegemea mbolea za chumvi chumvi ambazo licha ya kuuzwa kwa bei ya juu pia zinaleta madhara makubwa katika udongo linaweza kumalizika kabisa kwa kufufua mradi wa mbolea wa kilimo mseto Peramiho wilayani Songea mkoani Ruvuma.

Historia inaonesha kuwa kilimo mseto kwa kutumia mradi wa kurutubisha ardhi kwa kutumia mbolea ya marejea  yaliyoletwa kutoka porini mwaka 1942 na kutambuliwa Peramiho na padre Otmar na Bruda Krisp OSB ambapo mwaka 1963 bruda Herman  alianza kutumia mbolea ya marejea kuzuia magugu na kulishia mifugo ambapo mwaka 1983 ilianzishwa benki ya mbegu za marejea Peramiho (sunnhemp seed bank).

Mwaka 1987 baada  ya kuona umuhimu wa marejea katika kurutubisha ardhi kilianzishwa kituo cha mradi wa kurutubisha  udongo kwa kutumia marejea  Peramiho(MRUMA) kituo ambacho hadi sasa kipo kinaendelea kutoa elimu ya kutumia mbolea ya marejea kwa wakulima katika nchi nzima.
   
Gabriel Mhagama ni mkuu wa kituo cha MRUMA anasema kuna mimea mingi ambayo ina uwezo wa kuongeza rutuba katika udongo  ikiwemo   mimea jamii ya kunde ambayo imegawanyika katika makundi matatu mimea ya porini,mimea ya mazao na mimea ya miti.

Mhagama anasema alikabidhiwa kuwa mkuu wa kituo hicho tangu mwaka 1991 kutoka kwa muasisi wa kituo hicho hayati padre Gerald ambaye alifariki dunia mwaka 2000 ambapo hivi sasa wataalamu wengi wa masomo ya kilimo kutoka ndani na nje ya nchi wamekuwa wakifika katika kituo hicho kufanya utafiti na kutunukiwa shahada za kwanza,shahada ya pili na wengine wametunukiwa PHD.

Hata Mhagama anasema utafiti uliofanywa katika kituo cha MRUMA tangu mwaka 1942 umebaini kuwa mimea ya porini aina marejea inachukua nafasi ya kwanza kwa kurutubisha ardhi na mkulima akitumia mbolea hiyo ana uwezo wa kuzalisha mazao mara dufu zaidi ya kutumia mbolea za viwandani.

Utafiti uliofanywa na kituo cha kilimo Uyole kuhusu mbolea ya marejea umebaini kuwa shamba la hekta moja  lililolimwa marejea mwaka uliotangulia linaweza kutoa magunia 68 ya mahindi yenye uzito wa kilo 100 badala ya magunia 14 tu iwapo haujatumia marejea.

  Mhagama anabainisha kuwa marejea  ni mbegu zinazofanana na  mbegu za ufuta ,baada ya kupandwa   na kuota ni lazima kufyeka marejea yenyewe baada ya wiki mbili hadi  mwezi mmoja na kuyageuza kwa kuchanganywa na udongo ili yaoze iwapo unataka kulima mazao katika shamba hilo ndani ya mwaka huo.

“Iwapo unataka shamba lililopandwa marejea kulima mwaka unaofuata unayaacha marejea yakue hadi yatoe mbegu ambapo utavuna mbegu  na yale majani ya marejea  unayachanganya na udongo ili kurutubisha ardhi tayari  kupanda mazao  marejea ni bora kwa kutoa mboleavunde,rahisi kufyeka na uoza haraka’’,anasisitiza.

Utafiti umebaini kuwa mbolea ya marejea ndiyo majibu ya mkulima ambaye hawezi kumudu kununua mbolea ya viwandani kwa kuwa mbolea hiyo  hurutubisha na kudumisha rutuba ardhini,vijidudu viitavyo bacteria hutoboa mzizi wa marejea na kusababisha vijinundu ambavyo ni nyumba yao na bacteria hao hutangua hewa aina ya naitrojen kama mbolea kwa kulishia mimea.

“Siku zote tunawambia watu kwanini wanang’ang’ania kulima mazao ya haraka haraka kwa kutumia mbolea za chumvi chumvi wakati zinawaumiza,badala ya kuchukua mbolea ya marejea ambayo hayana gharama yametolewa porini,watu wamekusanya na kuyaleta katika kituo chetu padre Gerod aliyapanda na kuyazalisha kwa wingi ambapo mwaka 1960 alipata kilo sita na kuanza kueneza mbegu za marejea nchini kote”,anasema Mhagama.

Mbinu aliyoitumia padre Gerod kupata marejea kutoka kwa wakulima ni kuwahamasisha wakulima kulima marejea na kumletea ambapo yeye aliwapatia mbolea ya chumvi chumvi na baada ya miaka mitatu padre huyo alipata maelfu ya tani za mbolea ya marejea ndipo aliwaambia sasa wananchi waache kutumia mbolea ya viwandani na kuanza kutumia marejea  lakini padre huyo aliendelea kununua marejea kutoka kwa wakulima.

Kulingana na mtaalamu huyo  mbolea ya marejea husaidia wiki mbili hadi mwezi mmoja baada ya kufyeka shamba  ambapo mkulima anatakiwa kupanda marejea kilo 20 kwa ekari na kutumia mfumo wa kubadilisha mazao yaani crop rotation ili kupata mafanikio wakati wa kutumia mbolea ya marejea.

“Wakulima ili wafanikiwe katika mbolea ya marejea wanatakiwa kubadili mazao kwa mfano mwaka wa kwanza katika ekari moja anapanda marejea,mwaka wa pili anapanda mahindi mwaka wa tatu anapanda mtama mwaka wa nne anapanda marejea pia anaweza kuchanganya mazao mwaka wa kwanza anapanda marejea na kahawa,mwaka wa pili marejea na jamii ya kunde,mwaka wa tatu marejea na mihogo na mwaka wa nne marejea ,migomba na  miti”,anasema.

Utafiti zaidi umebaini kuwa mbolea ya marejea  hupunguza na kuzuia magugu shambani,marejea ni malisho kwa wanyama pia majani yake ni mboga na mabua hutumika kwa ajili ya matandiko ya wanyama,marejea pia huzuia wadudu waharibifu.

 Mapato yatokanayo na matumizi ya mbolea ya marejea  ni ya kuridhisha na ya kudumu hata katika maisha ya vizazi vijavyo kwa kuwa udongo na mazingira vinabakia na asili ya kutotawanyika (soil structure stability).

Uchunguzi umebaini kuwa miaka ya 1983 mbolea ya marejea ilianza kutumiwa na wakulima wengi katika sehemu mbalimbali nchini ambapo wakulima na vikundi vya wakulima walifika katika kituo cha MRUMA Peramiho kujifunza kuhusu uzalishaji wa mbolea hiyo  hali ambayo ilisababisha maelfu ya tani za mbegu za marejea kununuliwa na kwenda kuzalishwa.

Mkuu wa kituo cha MRUMA Gabriel Mhagama anasema Baba wa Taifa mwalimu Julius Nyerere alitembelea kituo hicho na kufurahishwa na uzalishaji wa mbolea hiyo hali iliyosbabisha baba wa Taifa kununua tani za mbegu za marejea pamoja na kununua vitabu mbalimbali vinavyotoa elimu ya mbolea ya marejea.

Mhagama anasema padre Gerodi na hayati Baba wa Taifa walikuwa ni wafuasi wakubwa wa mbolea ya marejea ambapo mama Maria Nyerere bado anaendelea kutumia mbolea ya marejea na mara kwa mara anaagiza vitabu vingi  vinavyozungumzia mbolea ya marejea pamoja na kilimo mseto hivi karibuni amenunua tani mbili za marejea ambazo tumempelekea  nyumbani kwake Butihama”,anasisitiza Mhagama.

Mhagama anaongeza kuwa mbegu za marejea pamoja na  vitabu vinavyoelekeza matumizi ya mbolea hiyo na kilimo hai vinaagizwa na wakulima wengi toka nje ya nchi kila mwaka ingawa  idadi ya watanzania wanaotumia marejea ni wachache kutokana na serikali kutoa uhamasishaji zaidi katika matumizi ya mbolea za viwandani ambazo  zinauzwa kwa bei ya juu pia sio endelevu kwa kuwa zina madhara kwenye udongo.

“Katika kituo chetu tunatoa elimu kwa wakulima kuhusu mbolea ya marejea lakini jambo la kusikitisha ukiachia aliyekuwa mkuu wa mkoa mstaafu wa Ruvuma hayati Dk.Lawrence Gama, baba wa Taifa na mke wake mama Maria Nyerere ambao wametembelea kituo chetu na walihamasisha matumizi ya mbolea ya marejea,hadi sasa hakuna kiongozi mwingine yeyote ambaye amewahi kufika hapa hakuna watalaamu wa ugani wa serikali mbunge,mkuu wa mkoa,mkuu wa wilaya,waziri wala Rais “,anasema.

Mhagama anasema hayati Dk.Gama akiwa mbunge wa Songea mjini alipeleka teknolojia ya mbolea ya marejea bungeni ili waziri wa kilimo aweze kufuatilia zaidi kuhusu matumizi ya mbolea hiyo na kwamba jambo la kusikitisha tangu wakati huo hadi sasa hakuna ufuatiliaji wowote wala hatua za kuhakikisha wakulima nchini wanahamasishwa kutumia mbolea ya marejea.

“Vikundi mbalimbali vya wakulima ambavyo vimetambua siri ya mbolea ya marejea vimekuwa vinaniita kutoa elimu ya uzalishaji pamoja na kilimo hai kwa mfano juzi nilikuwa mkoani Morogoro kwa siku tisa,mwezi uliopita nilikuwa mkoani Mbeya wilayani Mbozi nikitoa elimu ya marejea kwa wakulima raia wa Uswis waliniita kwa gharama zao, kila mwaka nakwenda katika mikoa mbalimbali nchini kutoa elimu hii”,anasema Mhagama.

Mtaalamu huyo wa marejea anasema dhana ya kilimo kwanza ambayo inapigiwa chapuo kwa ushirikiano wa Rais Jakaya Kikwete pamoja na waziri mkuu Mizengo Pinda inaweza kuwa endelevu na kupata mafanikio makubwa endapo watanzania wote watatumia mbolea ya marejea ambayo inapatikana bure na ni endelevu kwa udongo kwa kizazi cha sasa na kijacho.

“Nakuomba waziri mkuu Pinda utembelee katika kituo chetu za kuzalishia mbolea ya marejea  Peramiho ikiwezekana nipeni nafasi hata ya saa moja katika Bunge la Muungano ili niweze kutoa elimu hii kwa wabunge wote naamini wabunge watahamasisha wapiga kura wao kuachana na mbolea za viwandani na kuanza kutumia mbolea ya marejea ambayo ndiyo mkombozi wa wakulima na dhana nzima ya kilimo kwanza”,anasisitiza.
   
Thomas Lipuka mdau wa kilimo anasema kuwa sekta ya kilimo nchini kwa miaka mingi haijawanufaisha wakulima wadogo na kwamba cha kusikitisha zaidi wakulima wengi wameonekana ni kama ngazi ya kupandia wafanyabiashara wa kati na wakubwa,  mashirika na makampuni makubwa kwa kujinufaisha kupitia wakulima pamoja na mbolea ya ruzuku ambayo wanajinufaisha mawakala na viongozi wa serikali wasiokuwa waaminifu.

Mshauri wa kilimo katika mkoa wa Ruvuma Sixtus Msanga anasema wakulima nchini wanajitahidi kulima lakini kilimo kinazidi kukatisha tamaa kutokana na changamoto mbalimbali hasa bei kubwa ya pembejeo na ukosefu  wa soko la uhakika kwa ajili ya mazao yao

.Naye mwakilishi kutoka shirika la Tanzania Organic Agriculture Movement(TOAM) Noel Kwai anasema  kilimo hai sio kitu kigumu bali mkulima wa kawaida anaweza kufanya kwa kutumia mbolea za asili ambazo ni endelevu na hazina madhara kwenye udongo.

“Sisi kilimo hai tunaangalia mbele zaidi kwanini utumie mbolea za viwandani zenye bei kubwa badala ya kutumia samadi na mbolea nyingine za organic ukichukulia kuwa mbolea ya viwandani ni bei juu na haitoshi, kilimo hai hapa  nchini  historia yake imetokea Peramiho  ni makosa makubwa kulima bila kutumia  mbolea kwa kuwa marejea yapo tuache uvivu”,anasema.

Baruapepe amidelo@yahoo.com,simu 0766463129

              
 



No comments:

Post a Comment