Friday, March 2, 2012

Songea na shetani wa mauaji


  
Na Albano Midelo
TAKRIBAN watu 14 hadi sasa wamekufa na 48 kujeruhiwa kutokana na  maandamano na vitendo vya mauaji vinavyoendelea kwenye viunga vya mji wa Songea ambao ndiyo makao makuu ya mkoa wa Ruvuma.
Mauaji hayo yakinyama yalianza tangu mwezi Novemba mwaka jana ambapo awali mauaji yalikwenda sanjari na vitendo vya unyang’anyi wa pikipiki kisha madereva wa pikipiki hizo kuuwawa kikatili na miili yao kutupwa katika misitu iliyopo nje kidogo ya mji wa Songea.
Mwanzoni mwa mwaka huu vitendo vya mauaji viliendelea na kusababisha hofu kubwa kwa wakazi wa mji wa Songea ambao walitarajia mauaji hayo yangekomeshwa na jeshi la polisi lenye dhamana ya kulinda uhai wa raia pamoja na mali zake.

Katika hali isiyotarajiwa kasi ya mauaji iliendelea ambapo sasa ilidaiwa wauaji walianza kuuwa wasichana na wanawake kisha kuondoa baadhi ya viungo vya mwili zikiwemo sehemu za siri  kwa madai viungo hivyo vilitumika kwa ajili ya vitendo vya kishirikina.
Mwezi Februari mwaka huu hali ya mauaji iliendelea kwa kasi ambapo matukio ya mauaji yaliendelea kuripotiwa mara kwa mara.Hali hiyo iliwafanya wakazi wa mji wa Songea kuamua kuingia vitani ili kupambana na janga hilo ambalo linatishia usalama na amani ya wakazi wa mkoa wa Ruvuma ambayo walikuwa wameizoea kuiona tangu kuzaliwa kwa mkoa wa Ruvuma.
Wananchi baada ya kuona ndugu zao wanaendelea kuteketea waliamua sasa kujilinda wao wenyewe ikiwemo kuchukua sheria mkononi bila kutambua kufanya hivyo ni kinyume cha sheria.
Kwa mfano wakazi wa eneo la Ruhuwiko ambao ndugu zao kadhaa wameteketea kwa kuuwawa na watu wasiojulikana,mwezi Februari mwaka huu waliamua kuwachoma kwa moto watu wawili ambao walidaiwa kuwa ni majambazi.

“Tuliwakamata watu hawa wawili wakijaribu kufanya mauaji katika eneo letu ambapo walidai walitumwa kumuua mama mmoja,baada ya kuwakamata tuliwahoji na kuanza kuwapa kipigo ili watueleze ukweli ndipo walidai kuwa wao ni wauaji  tayari wameua watu 10 hadi wanakamatwa’’,alidai mwananchi mmoja ambaye hakutaka jina lake liandikwe.
Mwananchi huyo alidai kuwa watu hao baada ya kukiri wao wenyewe kuwa ni wauaji ndipo wananchi  wanawake kwa wanaume walichachamaa na kuanzia kuwapiga ,kuwafunga kamba miguu na mikono kisha kuanza kuwachoma moto wakiwa hao.Tukio la wananchi kuchukulia sheria mkononi pia limefanywa na wakazi wa Mkuzo ambao waliwauwa watu wawili wakidai kuwa ni wauaji.
Baada ya matukio hayo jeshi la polisi liliamua kufanya mkutano wa pamoja na wakazi wa maeneo hayo na kuwataka wanapowakamata watuhumiwa wasichukue sheria mkononi badala yake wawafikishe kwenye vyombo vya dola ili haki itendeke.
Hata hivyo kasi ya mauaji ya wananchi iliendelea katika viungo mbalimbali vya mji wa Songea hali ambayo  iliongeza hasira kwa wananchi ambao walidai kuwa jeshi la polisi limeshindwa kukomesha mauaji.
 Kamanda wa polisi wa mkoa wa Ruvuma Michael Kamuhada mara kadhaa alikaririwa katika vyombo vya habari akitoa rai kwa wakazi wa mji wa Songea kutulia kwa kuwa jeshi hilo linajipanga ili kuhakikisha kuwa mauaji hayo yanakwisha na hali ya usalama na utulivu inarudi kama kawaida.
Kitendo cha kuchelewa kuchukua hatua za kumaliza tatizo la mauaji ndicho ambacho kilisababisha wananchi kuamua kufanya maandamano bila kibali kwa kuwa mauaji yaliendelea kutokea mfululizo na jeshi la polisi pamoja na serikali ya wilaya na mkoa ilidai kuwa inajipanga kukabiliana na wauaji bila mafanikio.
Hatimaye wananchi waliandamana bila kibali na kuleta athari zaidi katika mji wa Songea ikiwemo kusababisha vifo vya watu wanne ambao waliuwawa na polisi katika harakati za kutuliza maandamano hayo kwa kutumia mabomu na risasi za moto.
Wanaharakati wamelaani jeshi la polisi mjini Songea kutumia risasi za moto kwa lengo la kusambaratisha maandamano hayo  na kusisitiza kitendo cha kuuwa raia ni cha kinyume na haki za binadamu .
“Tatizo la polisi ni kutumia nguvu ya ziada hata katika mambo yatayotakiwa kucheza na saikolojia ya watu,mbinu ambayo naamini makamanda wa polisi  wanapaswa kuitumia ili kutuliza hasira za wananchi wanaolalamika kutotendewa haki’’, anasema Daniel Mwaijega.
Anabainisha kuwa wananchi wa Songea waliandamana kwenda kwa mkuu wa mkoa wa Ruvuma kutoa kilio chao kutokana na hofu na uchungu wa kutosikilizwa ,nguvu kubwa ya polisi iliyotumika kuwapiga mabomu,risasi pamoja na vitisho vingine.
Nguvu gani hiyo ya kuamua kutumia risasi za moto ghafla,mbona kule Mbeya ambako hali ilikuwa mbaya polisi waliishia kutumia mabomu ya machozi na maji ya kuwasha kwa siku tatu mfululizo?anahoji Mwaijage na kutokubaliana na maelezo ya kamanda wa polisi wa mkoa wa Ruvuma Michael Kamunda kwamba walilazimika kutumia risasi za moto ili kujihami na umati wa watu uliokuwa unawazidi nguvu.
Naye Neville Meena mhariri wa Mwananchi Jumapili  anadai polisi wanachotakiwa ni kueleza ukweli wa wao kuuwa raia wasikuwa na hatia  na kwamba wananchi hao walichokuwa wanahitaji ni neno la faraja kutoka kwa polisi ambao ni walinzi wa amani ili wajue  usalama wao dhidi ya mauaji.
“Jambo hili tuwe wakweli kama wananchi waliwazidi nguvu polisi,je polisi wangapi waliojeruhiwa,haiingii akilini katika ukubwa wa vurugu kama zilivyoelezwa na jinsi waandamanaji wanavyotajwa kwamba walikuwa wanapambana na polisi halafu asiwepo hata askari mmoja aliyejeruhiwa’’,anahoji Meena.
Meena anasisitiza kuwa nguvu iliyotumika kuwadhibiti waandamanaji zikiwemo risasi za moto,mabomu,fedha na gharama nyingine zingetumika kuwadhibiti wauaji wa raia kitu ambacho ndiyo kiini cha wakazi wa Songea kuandamana.
Kwa upande wake Askofu mkuu wa jimbo kuu katoliki la Songea mhashamu Norbert Mtega akizungumzia maandamano na mauaji yanayofanywa na polisi  anasema yanatokana na serikali  kuchelewa kutoa ufumbuzi wa matatizo yanayowakabili wananchi pamoja na serikali kutoa majibu ya juu juu hivyo kuchochea chuki na kuleta vurugu.
Kamishina wa operesheni maalum Paul Chagonja akizungumzia maandamano yaliosababisha vifo vya raia alidai kuwa  askari watatu walijeruhiwa baada ya kushambuliwa na wananchi kwa mawe,fimbo,nondo,kuchoma matairi na zana nyingine za jadi huku wakipaza sauti kwamba askari polisi hao lazima wauawe.
Hata hivyo kamishina huyo wa operesheni maalum anatahadharisha kuwa polisi wanaruhusiwa kuuwa chini ya kifungu cha sheria namba 18(c)cha sheria za kanuni za adhabu .
“Iwapo polisi watashindwa kuzima vurugu kwa kutumia maneno,virungu,mabomu ya machozi na maji ya kuwasha,njia pekee inayobakia ni ya kutumia risasi za moto ili kuepusha maafa makubwa,ni vema hilo likaeleweka ili kuondoa dhana potofu kwamba polisi hawaruhusiwa kuuwa’’,anasisitiza.
 Chagonja ameitaja mikakati na jitihada ambazo zimechukuliwa na polisi kuwa ni kuundwa kwa kamati ya kuchunguza kiini  cha maandamano na fujo zilizojitokeza katika mji wa Songea.
Mikakati mingine ameitaja kuwa ni kukutana na madiwani,maafisa tarafa,watendaji kata,mitaa na wenyeviti wa mitaa ili kupata suluhisho la kuondoa uharifu,kuimarisha ulinzi na usalama kupitia polisi jamii na kuendelea kutoa mafunzo kwa askari juu ya matumizi sahihi ya silaha katika udhibiti wa vurugu,fujo na maandamano kwa kuzingatia sheria na kanuni.
Athari nyingi zimejitokeza hadi sasa kutokana na mauaji hayo zikiwemo vifo vya watu,majeruhi na vilema na kwamba mauaji hayo yanaleta hofu kubwa kwa wananchi wa rika zote wakulima,wafanyakazi ,wafanyabiashara na wanafunzi.
Uchunguzi umebaini kuwa wakulima wa mji wa Songea ambao wanalima pembeni mwa mji huo huenda mwaka huu wakapata njaa kwa kuwa wanashindwa kwenda shambani kutia mbolea na kupalilia mashamba yao kwa hofu ya kuuwawa na wauaji .
Baadhi ya wanafunzi wa shule za msingi katika manispaa ya Songea wanaogopa kwenda shuleni kuhofia kutekwa na wauaji ambao hivi sasa wanadaiwa kutumia magari yenye vioo vyeusi na pikipiki kuwateka wanafunzi na hata watu wazima.
Mji wa Songea ambao unakadiriwa kuwa na pikipiki zaidi ya 6000  hivi sasa biashara ya kubeba abiria kwa pikipiki imepata dosari kutokana na abiria wengi kuogopa kupanda pikipiki hizo kwa madai kuwa baadhi ya madereva wanatumiwa na wauaji kuwapeleka abiria baada ya kulipwa fedha nyingi na wauaji hao.
“Sisi madereva wa pikipiki tunauwawa ovyo siku hizi kisha kunyang’anywa pikipiki,biashara hii hivi sasa haifai kwa kuwa ni sawa na kujitafutia kifo wewe mwenyewe,madereva wengi wameacha biashara hii na kufanya kazi nyingine za kujipatia kipato wengine wamerudi kwenye uhalifu’’,alidai Abdalah Ally dereva wa pikipiki mjini Songea.
Ally alidai kuwa wanaoendelea kufanya biashara ya kuendesha pikipiki ni wale tu ambao wana roho ngumu na kwamba wanachukua tahadhari kubwa ikiwemo kuhakikisha kuwa abiria wanaembeba wanamfahamu.
Mauaji ya Songea sio tu yanaleta athari kwa madereva wa pikipiki,bali pia hata kwa wafanyabiashara kwa mfano wanaoendesha biashara ya vinywaji kama vile bia hivi sasa wanakwama kwenye mauzo kwa kuwa wananchi wengi jua linapozama wanarudi majumbani kwao kuhofia kuuwawa.
Kwa ujumla maendeleo ya mji wa Songea yanarudi nyuma  kutokana  na mauaji yaliyotokea na kwamba kazi hazifanyiki ipasavyo,wakazi wa mji wa Songea wana hofu kubwa ,licha ya mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu kutoa rai kwamba wananchi warudi kazini wasiwe na hofu.
Wakazi wa mji wa Songea bado wana hofu kubwa .Hofu ya wakazi wa Songea itamalizika pale ambapo jeshi la polisi litakomesha kabisa mauaji haya ambayo hadi sasa bado uchunguzi na utafiti unaendelea kufanyika ili kujua nini hasa sababu ya vifo hivyo vya kinyama.



No comments:

Post a Comment