Wednesday, June 20, 2012

Askofu mkuu Mtega awafunda mapadri wapya

Na Albano Midelo
ASKOFU mkuu wa jimbo kuu katoliki la Songea mhashamu Norbert Mtega amewafunda mapadre nchini kutambua kuwa upadre sio kazi ya ajira bali ni kazi ya utume na majitoleo.
Mhashamu Mtega alitoa somo hilo wakati anahubiri kabla ya kuwapatia daraja takatifu la upadre mashemasi wawili  katika adhimisho la misa takatifu iliyofanyika katika kanisa la parokia ya Mjimwema jimbo kuu la Songea.
Mashemasi waliopatiwa daraja takatifu la upadre  na Askofu mkuu Mtega ni shemasi David Mhagama kutoka kigango cha Lizaboni parokia ya Songea na shemasi Markus Komba kutoka Kigango cha Mwengemshindo parokia ya Mjimwema.
“Upadre  sio kazi bali ni utume,leo mnapokea utume hapa siwapatii kazi,wala mimi sio mwajiri wenu,anayefikiri askofu ni mwajiri wake amekosa imani ,nenda kwa Rais Jakaya Kikwete utaajiri,nenda kwa waziri wa TAMISEMI utaajiriwa,unapojiweka hapa mbele ya Taifa la Mungu wewe ni sadaka ’’,alisisitiza.

 Askofu mkuu Mtega pia amewakumbusha waumini kuwa na moyo wa kujitolea katika shughuli mbalimbali za kanisa na kuacha kuona kichefuchefu  kutoa sadaka na huduma za kanisa la Mungu kwa kuwa kufanya hivyo  ni kumtumikia mwenyezi Mungu.
Alisisitiza kuwa bila kufikia kilele cha kutoa sadaka na kujitoa sadaka ni kazi bure na kwamba anayesali,anayepokea ekaristi takatifu na anayepata daraja takatifu kama upadre ajue siri yake yote ni majitoleo  kama Yesu Kristo alivyojitolea mwili wake kwa wanadamu.
Mhashamu Mtega amewatahadharisha mapadre kuwa upadre unaweza kuonekana mgumu iwapo tu watashindwa kuwa na moyo wa kujitolea sadaka katika  mwili,muda,roho na uzima  na kuacha kuona kichefuchefu kwenda kufanyakazi kwa waumini katika maeneo mbalimbali mijini na vijijini.
  “Ukifanyakazi ya Mungu utaheshimiwa na Mungu na ili uweze kupata heshima hiyo jitolee sadaka,poteza nafsi yako hapa ulimwenguni Mungu atakuheshimu katika maisha ya milele mbinguni ,wito wa upadre ni wa Mungu, uwe mnyenyekevu, usiogope upadre ukatoroka,jitoe sadaka,pokea utume bila kujitolea utume wako una kasoro’’,alisisitiza.
Amewaasa mapdre hao wapya kuwa wameitwa na Mungu hivyo wanatakiwa kuifanya ipasavyo kazi ya Mungu ambayo wametumwa kwenda kuifanya  kwa unyenyekevu mkubwa kwa kumtukuza Mungu kwa kuhubiri, kufungisha ndoa, kubatiza, kutoa kitubio na misa takatifu.
Kwa upande wake paroko wa parokia ya Mjimwema padre Nowe Duwe amemshukuru askofu mkuu Mtega kukubali kutoa daraja takatifu kwa mashemasi mawili katika kanisa la parokia hiyo licha ya kwamba  ujenzi wake bado haujakamilika hali ambayo inasababisha waumini kupigwa na jua,upepo na vumbi.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:

Post a Comment