Wednesday, June 13, 2012

Watu 13,000 hawajui kusoma Songea


Na Albano Midelo
WATU 13,706 katika Halmashauri ya wilaya ya Songea mkoani Ruvuma hawajui kusoma,kuandika na kuhesabu.
Afisa elimu  watu wazima katika Halmashauri hiyo Christopher Mwamalili alibainisha kuwa idadi hiyo imetokana na sense iliyofanyika  mwezi Februari mwaka huu idadi ambayo ni sawa na asilimia 14 ya watu wote wazima.
 Kulingana na sensa hiyo kati ya watu hao wanaume ni 6069 na wanawake ni 7637 ambapo takwimu za mwezi Februari mwaka huu zinaonesha kuwa Halmashauri ya wilaya ya Songea ina watu wazima  wanaojua kusoma,kuandika na kuhesabu 94,800 kati yao wanaume ni 45,900 na wanawake 48,981.
Kata ambazo zinaongoza kwa idadi kubwa ya watu wasiojua kusoma,kuandika na kuhesabu katika Halmashauri hiyo ni Ndongosi watu 585,Muhukuru watu 882,Matimira watu 664 na Mpitimbi watu 832.
Afisa elimu watu wazima huyo alikitaja chanzo cha Halmashauri hiyo kuwa na idadi kubwa ya watu wasiojua kusoma,kuandika na kuhesabu kuwa ni  kuwepo kwa idadi kubwa ya watoto ambao hawakuandikishwa darasa la kwanza kabla ya kuanza kwa Mpango  wa uboreshaji wa Elimu ya Msingi (MMEM).

Kwa mujibu wa Mwamalili sababu nyingine zilizochangia kuongezeka kwa idadi kubwa ya wajinga katika Halmashauri hiyo ni michango mingi waliokuwa wanatozwa wazazi na walezi,upungufu wa vyumba vya madarasa,utoro na mimba.
Hata hivyo amezitaja hatua ambazo idara yake imeanza kuzichukua ili kukabiliana na tatizo hilo ikiwemo ya  kuanzisha madarasa 92 ya Mpango wa uwiano kati ya  elimu ya watu wazima na jamii yaani MKEJA na kwamba walimu wa kujitolea waliohitimu kidato cha nne watatumika kufundisha madarasa hayo.
“Lengo ni kuhakikisha kuwa hadi kufikia mwaka 2013 idadi ya watu wazima wasiojua kusoma,kuandika na kuhesabu inapungua kutoka asilimia 14 hivi sasa hadi asilimia kati ya sita na saba na kufuta madarasa ya Mpango wa Elimu ya Msingi Kwa Walioikosa yaani MEMKWA kwa kuwa sio mpango endelevu kama ilivyo kwa mfumo rasmi wa utoaji elimu’’,alisisitiza Mwamalili.

  
albano.midelo@gmail.com


No comments:

Post a Comment