Tuesday, June 5, 2012

Wanafunzi 2000 hatarini kupata magonjwa


Na Albano Midelo
WANAFUNZI zaidi ya  2000 wa shule nne za msingi mjini Namtumbo mkoani Ruvuma  wapo katika hatari ya kupata magonjwa ya milipuko kutokana na shule hizo kukatiwa maji ya bomba.
Shule hizo ni Namtumbo yenye wanafunzi 669,Rwinga yenye wanafunzi  592,Selous yenye wanafunzi 477 na shule ya msingi Kidugalo yenye wanafunzi 453.
Mamlaka ya maji katika Halmashauri ya Namtumbo imeamua kuzikatia shule hizo maji kutokana na kile ambacho kinaelezwa kuwa shule hizo ni wadai sugu wa bili za maji hali ambayo inasababisha wanafunzi kutumia maji ya mto na visima ambayo sio salama na yanapatikana mbali .
Akizungumza kwa niaba ya mwalimu mkuu,mwalimu wa taaluma katika shule ya msingi Namtumbo Habibu Omary alisema tangu wamekatiwa huduma ya maji imekuwa ni kero kubwa kwa walimu na wanafunzi ambao walikuwa wanagemea maji hayo kwa matumizi mbalimbali yakiwemo kunywa,kufanyia usafi ,chooni pamoja na matumizi mengine.

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Kidugalo Owini Mpangala anasema shule hiyo haina maji ya bomba ,hivi sasa wanatumia wanatumia maji ya mto na visima vya jadi ambavyo vipo mbali na maji yake sio salama hivyo ametoa wito kwa mamlaka ya maji kupeleka huduma ya maji kwenye shule hiyo .
Naye mwalimu anayeshughulikia kitengo maalumu cha wanafunzi wenye ulemavu wa akiri katika shule ya msingi Namtumbo Lanziry Kampango anasema hali ni mbaya zaidi kwa wanafunzi wake wenye ulemavu wapatao 26 kwa kuwa mahitaji ya maji kulingana na mahitaji yao ni muhimu.
“Wanafunzi wenye ulemavu ni lazima wapate chai,sasa chai inatengenezwa vipi kama hakuna maji,wanafunzi hawa  wana masomo mengi  yanayotakiwa kufundishwa kwa vitendo mfano usafi chooni ,wakitoka kujisaidia maji hakuna tunaomba serikali ilipe bili na kurejesha maji shuleni’’,alisisitiza.
Mwalimu Onesmo Mbawala wa shule ya msingi Rwinga anasema tangu wamekatiwa huduma ya maji hali ni mbaya na kwamba huduma hiyo isiporejeshwa haraka kuna hatari wanafunzi na walimu wakapata magonjwa ya milipuko  kama vile kuhara kwa kuwa wanafunzi wanakwenda kujisaidia chooni bila kunawa jambo ambalo ni hatari kiafya.
“Hatua ambazo tunazichukua ili kukabiliana na hali hiyo ni kuwaagiza wanafunzi wanapofika asubuhi waje na maji,wengine wanasaidiwa na walimu kuwapatia maji ya kunywa pale wanapohitaji lakini maji katika shule yetu ni tatizo kubwa’’,alisisitiza mwalimu Mbawala wa shule ya Rwinga.
Makamu mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo Kassimu Ntara amesema hakuwa na taarifa kuwa baadhi ya shule katika zimekatiwa huduma ya maji hivyo ameahidi kufuatilia na kuhakikisha kuwa maji yanarudi katika hali ya kawaida.
“Tatizo la wanafunzi kukatiwa maji ndiyo kwanza nakusikia wewe nitafuatilia na kukaa na wataalamu wangu wa maji kwenye Halmashauri kuhakikisha kuwa maji yanarejeshwa haraka ingawa mamlaka ya maji ni mamlaka inayojitegemea nitafuatilia ili taasisi hizo ziweze kupata huduma ya maji’’,alisisitiza.
  
albano.midelo@gmail.com

No comments:

Post a Comment