Mji
wa
Peramiho uliopo wilayani Songea mkoani Ruvuma ni miongoni mwa miji ya zamani
yenye historia ya kipekee katika kanda ya kusini.Mji wa Peramiho unafahamika
zaidi nje ya nchi pengine kuliko miji mingine iliyopo kusini mwa Tanzania
kutokana na mji huo kuwa na historia ya namna yake kipekee.
Historia ya mji wa Peramiho uliopo
kilometa 24 tu kutoka makao makuu ya mkoa wa Ruvuma mjini Songea inaunganishwa na wabenediktini wa kanisa katoliki kutoka
St.Otilia nchini Ujerumani,ambao waliamua kuweka makao makuu yao katika Abasia
ya Peramiho.
Wabeneditine hao waliingia kwa mara ya
kwanza katika mji huo mkongwe mwaka 1898
wakiongozwa na Kasian Spiss.Tangu wakati huo wabenediktine hao wamekuwa na wakifanya mambo mazuri na ya kipekee katika
mji huo hali iliyosababisha kuutambua mji wa Peramiho kuwa ni mji unaokidhi
vigezo kuwa mji wenye utalii wa kihistoria.
Mhifadhi kiongozi wa makumbusho ya Taifa
ya Majimaji Philipo Maligisu anasema
wabenediktine wa Abasia ya Peramiho wametengeneza historia ya kipekee na
kuvutia katika nchi ya Tanzania ambapoWabenedikitine hao jambo kubwa la kwanza
ambalo limeacha historia katika mji wa Peramiho na taifa kwa ujumla ni pale
walipoamua kujikita katika suala zima la elimu na kuamua kuwekeza katika elimu
zaidi ya miaka 100 iliyopita hadi sasa.
Historia inaonesha kuwa walipoingia
kwa mara ya kwanza wabenediktine hao kwa kutambua umuhimu wa elimu waliamua kuanzisha madarasa kwa kufundisha
walimu na kufundisha wanafunzi hivyo kufundisha elimu zote mbili yaani elimu ya
kiroho na elimu dunia.
Kwa msingi huo eneo la Peramiho katika historia ya Tanzania lina historia ya
kipekee kwa zaidi ya miaka 100 sasa hivyo kuna ushahidi ambao unaonyesha
wabenediktine walidhamiria kufanya mambo ya msingi katika mji wa Peramiho na
taifa kwa ujumla.
Utafiti uliofanywa katika mji wa Peramiho
unaonesha kuwa wabenediktine hao walizindua rasmi mji huo Julai 31,1898 na
tangu hapo waliendelea na shughuli zao wakiwa na mahusiano mazuri wakati huo na
utawala wa machifu katika eneo hilo.
Hata hivyo mahusiano hayo mazuri baina
ya wabenedikitine hao wa kutoka nchini Ujerumani na machifu ulikuja kuharibika wakati wa vita vya
majimaji ambavyo vilianza mwaka 1905 na kumalizika mwaka 1907 na kusababisha padre
Fransis Scuss kuuwawa Septemba 9 1905.
Baada ya kumalizika vita hivyo vya
majimaji ilijitengeneza tena historia ya kanisa la Abasia ya Peramiho hivyo kulichukulia eneo hilo la mji wa
Peramiho kama eneo la kipekee kwa kuzingatia misingi ya sheria ya Tanzania
namba 10 ya mwaka 1964 na maboresho yake sheria 22 ya mwaka 1979 ambayo
inayatambua maeneo yote ya kihistoria kulingana na umuhimu wake katika jamii.
Hadi sasa watanzania wengi hapa nchini
bado hawajatambua kuwa mji wa Peramiho una historia ya kipekee inayowaunganisha
wananchi wa Ruvuma na sehemu nyingine duniani na hasa nchi ya Ujerumani ambao
wanaitambua sana Peramiho.
“Wananchi wa Ujerumani wanaijua sana Peramiho pengine kuliko hata
sisi watanzania,ndiyo maana kizazi na
kizazi wanasafiri kwa gharama kubwa hadi katika mji huo ili kufanya utalii wa
kihistoria kwa kutembelea katika maeneo mbalimbali ya kihistoria na kujifunza
mambo mbalimbali”,anasisitiza Maligisu.
Sera ya taifa ya utamaduni ya
mwaka 1997 ina tamka bayana kuwa eneo lolote la kihistoria linapokuwa
limetimiza miaka 100 tayari moja kwa moja linaingia katika urithi wa utamaduni
wa taifa.Kutokana na hali hiyo
ukiangalia mji huo wa Peramiho tayari umekidhi vigezo na maeneo yake yote ya
kihistoria kuingia katika urithi wa utamaduni wa taifa kwa ajili ya kujifunza
elimu na utalii .
“Hivi sasa mimi kama mhifadhi kutoka
makumbusho ya taifa tupo katika mchakato wa kuliingiza eneo la Peramiho katika
urithi wa utamaduni wa taifa na watu wengi watatembelea kwa lengo la kuhitaji
kufanya utafiti, kujifunza na kujua nini kilichopo ndani”,anasema mhifadhi
kiongozi wa makumbusho ya Taifa.
Akizungumzia nini kilisababisha
wamisionari wabenedikitine kuchagua eneo la Peramiho na sio mahali
pengine,mhifadhi huyo anasema padre
Maurus ambaye wakati huo alikuwa ndiyo mkuu wa jimbo lililoitwa kusini ya
Zanzibar mwaka 1888 alipita wakati huo akiangalia namna wabenedikitine kutoka
St. Otilia Ujerumani wanavyoweza kufika nchini kueneza injili kusini magharibi
mwa Tanzania.
Wabenediktine hao walifika hapa nchini
kwa lengo la kufanya uinjilishaji na sio katika mambo ya kisiasa ndiyo maana
waliamua kujenga misheni nje ya makao makuu ya serikali.Hata hivyo mwanzilishi wa uinjilishaji aliwaonya wabenedikitine kujihadhari
kujiingiza katika mambo ya siasa badala yake wajikite katika lengo lililowaleta
hivyo walianzisha misheni katika maeneo ya mbali zaidi ya serikali kama
Peramiho badala ya Songea mjini.
Hata hivyo historia inaonesha wabenediktine
walifikia katika mlima wa Peramiho ambapo
waliamua kujenga kanisa la mwanzo na nyuma ya hospitali ya misheni ya Peramiho
ambako kuna chuo cha uuguzi.
Kabla ya kujengwa kanisa katika eneo
hilo, wabenediktini hao walisimika msalaba kwa mara ya kwanza Julai 31,1898 na
kuongoza misa na hatimaye kujenga monasteri ya masista na kuanza kujenga msingi
wa kanisa dogo lenye urefu wa mita 13 na upana mita saba. Kadri miaka
ilivyozidi idadi ya wakristo iliendelea kuongezeka na kufanya kanisa hilo la
mwanzo kuwa ndogo ndipo wabenedikitine hao waliamua kujenga kanisa kubwa jipya
la sasa .
Kwa mujibu wa machapisho ya ujio wa wabenedikitine katika Abasia ya Peramiho,padre Kassian Spiss
alifanya kazi Kurasini Dar es salaam mwaka 1893 na baadaye akahamishiwa
Tosamaganga Iringa mwaka 1897.Hata hivyo padre huyo alitumwa kuanzisha misioni
katika nchi ya wangoni yaani mkoa wa Ruvuma hususan Songea Peramiho Julai
31,1898.
Padre Spiss na wenzake mnamo walifanikiwa
kufika ungoni na siku iliyofuata walifika katika boma la Songea na kupokelewa
na wakuu wa boma wakati huo waliishi kwa siku tatu.Baada ya siku tatu
waliendelea na safari kuelekea magharibi,kisha walifuata barabara na kuchepuka
kushoto na kusimika hema lao katika kijiji cha Maposeni wakati huo kikiitwa
Mbinga mhalule.
Kwa mujibu wa historia hiyo siku
iliyofuata padre Kasian alisoma misa kwenye kaburi la sultani Mhalule ambaye alikuwa anaheshimiwa na wangoni wa
eneo hilo wakati huo,Chief wa wangoni aliposikia kwamba padre Kasian na ujio wa
wamisionari wamefika katika eneo hilo la wangoni alikwenda kusalimiana nao na kutoa
zawadi ya mbuzi dume yaani beberu aliyenona akionesha kuwaunga mkono
wamisionari hao.
Baada ya kuhafamiana padre Kasian
alimpa chifu Mputa zawadi ya nguo ambayo watoto wawili wa Sultani Mhalule na
chifu Mputa akiwa na mdogo wake Chemchaya
waliamua kuhama eneo hilo hivyo walijenga
eneo la umbali upande wa
kaskazini ambapo chifu Mputa aliwaalika wamisionari kumtembelea siku iliofuata
katika mji wake mpya wa Maposeni na walikaa kwake kwa siku mbili.
Baada ya muda padre Kassian alikwenda
Songea bomani ambapo ndiyo siku hizi wanaita kwa mkuu wa wilaya ili kufuatilia
mashauri ambapo wakati anakwenda alipita njia ya mkato ili afike mlima
Mbewike.Wakati anapita katika mlima Mbewike ndipo aligundua kuwa mahali pengine pazuri juu ya mlima Peramiho
ndipo akaamua kuanzisha misioni mahali hapo ndiyo Peramiho ya leo.
Mnamo Julai 31,1898 misa ya kwanza
ilisomwa Peramiho ndipo ukawa mwanzo wa misioni ya kwanza ilioanzishwa ungonini
na kwamba Agosti 5,1898 wamisionari hao walipima kiwanja na kujenga msingi wa
kanisa, jengo la kwanza la kanisa lilijengwa kwa miti ,mianzi na kuezekwa kwa
nyasi.
Wenyeji wa Peramiho walifanya kazi ya
ujenzi kwa kushirikiana na wamisionari bila shida yeyote ambapo kila jumbe
alikuwa anakuja na watu wake na kusaidia kazi kila alipohitajika.Majengo ya
kwanza ya wamisionari katika mji wa Peramiho yalijengwa mwaka 1898 zikiwemo
nyumba za wamisonari na kanisa dogo.
Mwaka1902 hadi 1905 kanisa zuri lilijengwa katika mji wa Peramiho pamoja na
nyumba nyingi za wamisionari ambapo padre Kasian Spiss alikuwa ndiyo paroko wa
kwanza wa Peramiho,Padre ambaye aliwekwa wakfu Novemba 16,1902 kuwa askofu wa
kwanza wa jimbo la Zanzibar kusini,makao makuu yake yalikuwa ni Peramiho na
Kigonsera.
Katika tukio la kusikitisha Askofu
Kasian mnamo Agosti 14,1905 ikiwa takriban saa mbili asubuhi akiwa anarudi
Kilwa baada ya kusikia Liwale kuna vurugu,alikutana na wapiganaji wa vita vya
Majimaji ambao walimua yeye pamoja na wenzake katika eneo la Mikukuyumbu
Liwale.
Baada ya kuuwawa Askofu Kasian nafasi
yake ilichukuliwa na padre Franziskus aliyekuwa paroko wa Peramiho ambaye baada
ya vita kutokea alikataa kutorokea Kigonsera hivyo na yeye aliuwawa na wangoni
huko Maposeni .
Ujenzi wa kanisa kuu la Peramiho
ulianza wakati Askofu Gallus Steiger na
bruda Gisral Stumpf ambaye aliandaa mchoro wa kanisa hilo mwaka 1940 na mwaka 1941 msanii wa majengo Hans Burkard wa Uswis alisanifisha rasimu ya
michoro hiyo na kumrejeshea Askofu Gallus mwaka 1943 na michoro kukamilisha na
bruda Gislar.
Juni 29,1943 matofali 10,000 yaliofyatuliwa
katika eneo la mto Luwawasi chini ya usimamizi bruda Mansuet Mendlel
yalifikishwa katika eneo la ujenzi wa kanisa hilo ambapo jumla ya matofali
milioni tatu yalihitajika.
Udongo kwa ajili ya kutengenezea vigae
pia ulihitajika ambapo vigae vilitengenezwa
na kusafirishwa kutoka Matomondo wilayani Songea hadi mto Ruvuma chini
ya usimamizi wa bruda Luitfried Kramer na kazi ya ujenzi wa kanisa hilo ilianza
Julai 6,1943 na kumalizika Septemba 9,1943.
Kenchi za mihimili ya kanisa kuu hilo
zenye uzito wa tani tano chini ya usimamizi wa mabruda Nonosius Bleicher na
Menas Leicht ilifanyika na kupandishwa kwa mashine maalum iliyotengenezwa na bruda
Jucundus Weigele Agosti 1946.
Mnamo Novemba 24,1945 vigae vyote
120,000 vilikuwa tayari kwa ajili ya kuezekea kanisa hilo na mnamo mwaka 1948
kanisa kuu Peramiho lilibarikiwa na padre Heribert na padre Gerod Rupper akawa padre wa kwanza
kuhubiri katika kanisa hilo jipya.
Ukiachia mbali kanisa la
kihistoria,lakini pia Abasia ya Peramiho ina seminari kuu,hospitali ya misheni
ambayo serikali imeipandisha hadhi kuwa hospitali ya rufaa,chuo cha
uuguzi,kiwanda cha uchapaji yaani Peramiho printing press,chuo cha ufundi
seremala,magari na umeme na tawi la chuo kikuu cha madaktari Bugando.
albano.midelo@gmail.com,simu
0766463129

No comments:
Post a Comment