Na Albano Midelo
TANZANIA
ni nchi pekee katika Afrika mashariki ambayo imebahatika kuwa na vivutio vya
kipekee vya utalii ambavyo huwezi kuviona katika sehemu nyingine yeyote
duniani.
Nchi yetu
imebahatika kuwa na maziwa mengi kuliko nchi yeyote katika bara la
Afrika.Maziwa hayo ni pamoja na ziwa Viktoria,Tanganyika,Nyasa,Rukwa na maziwa
mengine madogo.
Ziwa Tanganyika lililopo magharibi mwa nchi ni
miongoni mwa kivutio cha utalii.Ziwa
hilo lipo katika mikoa ya Kigoma na Rukwa na kuelekea hadi katika nchi jirani
za Kongo DRC na Burundi.
Ziwa
Tanganyika lina sifa kuu nne ambazo pamoja na kuwa ziwa refu kuliko maziwa yote
ulimwenguni likiwa na urefu wa kilometa 673 kutoka kaskazini hadi kusini mwa
ziwa hilo.
Sifa
nyingine ya ziwa Tanganyika ni kuwa na kina kirefu kwenda chini.Ziwa hilo
linashika nafasi ya pili kwa kina kirefu ulimwenguni baada ya nafasi ya kwanza
kuchukuliwa na ziwa Baikar ambalo lipo
katika nchi ya Rusia.
Kina cha
ziwa Tanganyika ni kilometa 1.47 au meta 1470
hivyo ziwa hilo kuwa na kina cha kipekee ambacho ni kivutio cha utalii
kianchoweza kuwasukuma watalii kufika
katika ziwa hilo kuona maajabu hayo.
Ziwa hilo
linawashangaza wengi kwa ukubwa na ujazo wake ambao ni kilometa za ukubwa 18,900
na kwamba ziwa hilo linachukua asilimia 17 ya maji yote baridi ulimwenguni.
Kana
kwamba haitoshi ziwa Tanganyika lina utajiri mkubwa wa viumbe hai wa aina mbalimbali wakiwemo
samaki,mamba,viboko pamoja na viumbe wengine wa majini.
Watu
wanaotaka kujifunza kupitia ziwa hilo wanapata fursa ya mambo mbalimbali ya kibaiolojia na kiuchumi
hasa kutokana na samaki wa aina
mbalimbali waliomo katika ziwa hilo.
Ziwa
Tanganyika lina aina za samaki zaidi ya 400
na kati ya aina hizo za samaki
kuna aina ya samaki ambao wana uwezo wa kutoa umeme wanaofahamika kwa jina la
electric fish haya ni maajabu mengine ya
dunia ambayo yanawashangaza wengi.
Kutokana
na sensa ya samaki ya mwaka 1999 ziwa Tanganyika linakadiriwa kuzalisha samaki
kati ya tani 165,000 hadi 200,000 zenye thamani ya dola za kimarekani milioni
80 hadi milioni 100.Miongoni mwa samaki maarufu katika ziwa hilo ni dagaa, migebuka,
kambale, sangara, magege,samaki wa mapambo, singidae na kuhe.
Mhifadhi
kutoka hifadhi ya Gombe Noelia Mnyonga ambaye analifahamu vyema ziwa Tanganyika,
akizungumzia samaki ambao wanatoa
umeme,anabainisha kuwa aina hiyo ya samaki wanatoa umeme pale wanaposogelewa na
adui hivyo kuwa kivutio adimu na cha kipekee ulimwenguni.
“Samaki
huyu kwa kuwa anatoa umeme iwapo angetangazwa ndani na nje ya nchi watalii
wengi wangemiminika kwenda katika ziwa Tanganyika ili kwenda kuwaona na hivyo
serikali kupata kipato kikubwa”,anasisitiza Mnyonga.
Anaongeza
kuwa watalii hao baada ya kusikia habari za samaki anayetoa umeme hakuna ubishi
wangependa kufika ziwa Tanganyika na kuona samaki hao wanatoaje umeme na kwamba
aina hiyo ya samaki haipatikani katika maziwa mengine duniani zaidi ya ziwa
Tanganyika.
Baadhi ya
watalii wanapenda kujifunza maisha ya viumbe wa majini akiwemo samaki huyo
anayetoa umeme hivyo wanapopata fursa ya kufika katika maziwa kama ziwa Tanganyika wangependa kufanya
utafiti wa aina mbalimbali za samaki na kufahamu aina na tabia za samaki.
H
ata hivyo
utafiti wa kimataifa ambao umefanyika mwezi Aprili mwaka huu na nerouetholojist
Erick Fortune kutoka chuo kikuu cha Johns Hopkins cha nchini Marekani unaonesha kuwa samaki hao
wana uwezo wa kutoa umeme kwa kutumia
ogani umeme iliyopo kwenye mikia ya samaki hao.
Utafiti huo unaonesha kuwa samaki huyo anaweza
kutumia umeme unaozalishwa mwilini mwake kwenye mawindo yake na kwamba umeme
unaozalishwa na samaki huo ni kidogo na hauwezi kuleta madhara yeyote na kwamba
samaki umeme ni wa kipekee na wanavutia watu wengi ambao wanapenda kwenda
kufanya uchunguzi zaidi.
Mtafiti huyo anasema katika utafiti kuhusiana na samaki wanaotoa umeme aliweza kujifunza tabia za samaki hao baada ya kufanya majaribio na kuweka vifaa katika makazi yao ya asili majini ambapo aliweza kusikiliza na kurekodi maisha yao,wanavyoweza kuwasiliana na viumbe wengine kwa kutumia ogani ya umeme,kupata hisia na namna wanavyoweza kujipatia chakula chao kwenye mazingira wanayoishi majini.
Utafiti wa
Chuo Kikuu cha Johns Hopkins uliofanyika kwa msaada wa mfuko wa Taifa wa
Sayansi (NSF) ulioongozwa na injinia Nuhu Cowan umewezesha kujifunza zaidi kuhusu jinsi samaki umeme
wanavyoweza kufanyakazi ya kudhibiti tabia zao na mazingira yao majini.
"Katika
utafiti wetu tumefanya majaribio katika maabara kuhusu samaki wanaotoa
umeme hata hivyo uchunguzi unatakiwa
kufanyika zaidi ili kutuwezesha kujibu maswali maalum ya kisanyasi kwa kuwa
Watafiti tunataka kuelewa vizuri jinsi samaki hawa wanavyoweza kutoa umeme kwa
kutumia sense organs za umeme zilizopo mkiani ambazo zinawawezesha
kuwasiliana na wenzao,kutawala mazingira
yao na kupata chakula chao majini, "anaelezea Cowan wa NSF.
Utafiti
unaonesha kuwa kwenye mkia wa samaki huyo kuna kiungo kidogo ambacho kinahusika
na kuzalisha umeme na kwamba kiungo hicho kinapita hadi juu ya magamba au ngozi
ya samaki huyo na kutoa umeme kila anapohisi kuna hatari,au anapotaka
kuwasiliana na wengine na anapokuwa kwenye mawindo kwa ajili ya chakula.
“Samaki umeme anaweza kutoa umeme katika baadhi ya matukio, mabadiliko, ishara na mawasiliano, samaki umeme wawili wa kike na wa kiume wanatoa umeme wanapoanza kujamiiana anasisitiza mwanasayansi Cowan katika utafiti wake.
watafiti pia wanataka kujifunza kile kinachotokea wakati samaki umeme zaidi ya wawili wanapokutana pamoja na kujifunza kutokana na samaki umeme kutegemea organ ya umeme zaidi ukilinganisha na sense ogani nyingine tano za mwili zikiwemo macho,mapezi,masikio,magamba na pua anasema Elizabeth Cropper, mkurugenzi wa programu ya Biolojia ya NSF ilifadhili utafiti huo.
Anabainisha
zaidi kuwa samaki umeme kwa kutumia ogani ya umeme kwenye mkia wake inamwezesha
kufanya mambo mengi zaidi kama vile kuogelea mbele,nyuma na kufanya mzunguko wa
haraka majini,kuwasiliana,kuhisi na kula kuliko kutegemea maono katika sense
organ nyingine tano.
Ukiachia samaki huyo anayetoa umeme,ziwa Tanganyika pia lina aina nyingine za samaki wakiwemo dagaa maarufu wa kigoma.Katika miji ya Kigoma na Sumbawanga wakazi katika miji hiyo wanafanya biashara ya dagaa hao wanaovuliwa katika ziwa Tanganyika.
Biashara
ya dagaa kutoka ziwa hilo endapo itaboreshwa
na wadau wake kujipanga vizuri dagaa hao wanaweza kuleta maendeleo
makubwa kwa wananchi na kuinua maendeleo yao kiuchumi.
Hata
hivyo baadhi ya wakazi katika miji hiyo wanapeleka dagaa hao katika nchi za
jirani ikwemo Kongo DRC,Burundi na Zambia katika kiwango ambacho hakitoi mapato
makubwa.
Mhifadhi
wa ziwa Tanganyika anatoa wito kwa serikali kutoa fursa kwa wawekezaji kuwekeza
katika ziwa hilo kwa kujenga viwanda vya kusindika dagaa ili hatimaye dagaa hao
waweze kupelekwa kuuzwa nje ya nchi katika viwango vya kimataifa ili kutoa
faida kubwa zaidi .
Hata
hivyo mkuu wa mkoa wa Rukwa Injinia Stella Manyanya ameshauri kuimarisha ushirikiano baina ya nchi jirani za
Kongo DRC , Burundi na Tanzania ili kulifanya ziwa Tanganyika kuwa na matumizi
endelevu kwa kuwa ziwa hilo limezungukwa na nchi hizo na lina utajiri wa
maliasili ambazo ni urithi wa Taifa.
Ameshauri
mabalozi katika nchi hizo wasaidia kuunganisha utalii kutoka katika nchi zote
sanjari na kuboresha mazingira ya ziwa Tanganyika ili kuwalinda viumbehai
waliomo ndani ya ziwa ziwa hilo wakiwemo samaki.
Hata
hivyo uchunguzi umebaini kuwa kina cha ziwa Tanganyika kinapungua mwaka hadi
mwaka kutokana na uharibifu mkubwa wa mazingira
ambao unaendelea kufanywa kutokana na shughuli mbalimbali za kibinadamu.
“ Watu
wanakata miti ovyo kwenye hifadhi ya ziwa Tanganyika,vyanzo vya maji
vinavyotiririka kuelekea kwenye ziwa hilo vimeharibiwa katika kiwango
kinachotisha hivyo kuathiri ziwa hilo ambalo ni muhimu kwa uchumi wa Taifa’’anasisitiza
mhifadhi wa ziwa hilo Leonia Mnyonga.
Anashauri
wadau wote wa mazingira katika nchi zinazozunguka ziwa Tanganyika kuungana kwa
pamoja katika kulinda mazingira ya ziwa Tanganyika hasa kuhamasisha kupanda
miti katika maeneo mbalimbali hivyo kufanya ziwa Tanganyika kuwa endelevu.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129.


No comments:
Post a Comment