Na Albano Midelo
WAANDISHI wa habari kanda ya kusini wamemchangia mwandishi
mwenye ulemavu wa macho Musa Chilungo zaidi ya shilingi 340,000.
Kiasi hicho cha fedha kilipatikana katika harambee iliyoongozwa na mwenyekiti wa chama cha waandishi wa habari mkoa wa Mbeya Christopher Nyenyembe kwenye ukumbi wa chuo kikuu cha Ruaha mjini Iringa.
Waandishi wa habari zaidi ya 150 kutoka mikoa ya Mbeya,Iringa,Ruvuma,Lindi,Mtwara,Katavi,Rukwa na Njombe walikuwa wanapata mafunzo ya siku mbili ya sensa ya watu na makazi itakayofanyika usiku wa kuamkia Agosti 26,2012 nchini kote.
Katika mafunzo hayo yalioendeshwa na ofisi ya Taifa ya takwimu wanahabari walijifunza umuhimu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012,maeneo ya kuhesabia watu,maswali ya sense,sheria ya takwimu na wajibu na majukumu ya vyombo vya habari katika kufanikisha sensa ya watu na makazi.
Nyenyembe ambaye alikuwa mwenyekiti wa mafunzo hayo
aliwafahamisha wanahabari kuhusu ulemavu wa macho aliopata mwandishi Chilungo
ambaye hivi sasa ni mtangazaji wa kituo cha redio cha Ruangwa FM kilichopo
wilayani Ruangwa mkoani Lindi.
“Ndugu zangu wanahabari Musa Chilungo nimefanya naye kazi kwa
miaka mingi akiwa hana ulemavu,sisi wote ni walemavu watarajiwa naomba
tumchangie mwenzetu kwa kuanza mimi namchangia shilingi 20,000’’,alisisitiza
Nyenyembe.
Chilungo alipata ugonjwa wa macho na hatimaye kupata ulemavu
wa macho na kushindwa kuona tena tangu mwaka 2007 na kwamba kabla ya mwaka 2006
wakati akiwa anaona alikuwa mwandishi wa magazeti ya serikali za mitaa( ALAT).
Mwandishi huyo mkongwe ambaye pia kitaaluma ni mwalimu
anasema kutokana na kupata ulemavu wa macho mwaka 2010 alistaafishwa
kufanyakazi serikalini ambapo hivi sasa
anaishi maisha ya kubangaiza kwa kuwa ana familia ambayo inamtegemea kwa kila
kitu.
“ licha ya kwamba naendelea kufanyakazi ya utangazaji katika
kituo cha redio ya Halmashauri ya Ruangwa napata posho tu,hali ni ngumu tangu
nilipoachishwa kazi ya ualimu mwaka 2010
kutokana na ulemavu wa macho,watoto wangu wanasoma fedha zinahitajika kwa
ujumla maisha yangu hivi sasa ni magumu’’,alisisitiza.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:
Post a Comment