Friday, September 7, 2012

Abate mwafrika wa kwanza aadhimisha jubilei


Na Albano Midelo
ABATE wa kwanza mwafrika  katika shirika la wabenediktini la mtakatifu Otilia padre Alcuin Nyirenda  ameadhimisha Jubilei ya miaka 25 ya upadre katika kigango cha Lizaboni parokia ya Songea.
Abate mstaafu Nyirenda alizaliwa parokia ya Mgazini na kukulia katika kigango cha Lizaboni ambapo alipata elimu ya msingi katika shule za msingi Ruhuwiko,Mfaranyaki na Hanga utawani na kupata elimu ya sekondari katika seminari ya Likonde jimbo la Mbinga.
Abate mstaafu Nyirenda alipata masomo ya upadre katika seminari kuu za Kibosho na Peramiho na kupewa daraja takatifu la updare na Askofu mstaafu wa jimbo la Mbinga Emanuel Mapunda  mwaka 1978.
Abate mstaafu Nyirenda baada ya kupewa daraja la upadre alipewa majukumu mbalimbali yakiwemo katibu wa utawa wa Abasia ya Hanga,mlezi mkuu wa wanovisi wa Hanga kabla ya kwenda  masomoni Roma nchini Italia kuanzia mwaka 1991 hadi 1993 kwa ajili  ya masomo ya teolojia ya kitawa katika chuo kikuu cha wabenediktini wote.

Mara baada ya kuanzishwa kwa Abasia ya Hanga Desemba 13,1993 padre Alcuin Nyirenda  alichaguliwa kuwa Abate wa kwanza mnamo Januari 15,1994 hivyo kuwa Abate wa kwanza mwafrika katika shirika la wabenediktini wa mtakatifu Ottilia.
Historia ya Abate huyo inaonesha kuwa miaka 10 baadaye tangu awe Abate  yaani mwaka 2004 alistaafu na kwenda kufanyakazi makao makuu ya watawa wabenediktini wote ulimwenguni wa kike na wa kiume huko Roma nchini Italia katika chuo kikuu cha wabenediktini cha mtakatifu Anselimo ndiko anakoishi na kufanyakazi hadi  sasa.
Akihubiri katika jubilee hiyo Askofu mkuu wa jimbo kuu katoliki la Songea mhashamu Norbert Mtega amepongeza Abate mstaafu Nyirenda kwa kufanikisha kazi ya kichungaji ikiwemo ya kuwahahasisha waumini wa kigango hicho kujenga kanisa lao la kigango ambalo hadi sasa limegharimu zaidi ya shilingi milioni 89.
Katika nafasi hiyo mhashamu Mtega aliwaasa viongozi wa kanisa na serikali kuchukua maamuzi magumu ambayo ni kusimamia ukweli na kuchukua maamuzi yanayopingana na desturi zilizozoeleka na watu na inakuwa vigumu kubadilika.
“Maamuzi magumu kwetu sisi padre ni pale tunapotoa kauli na maamuzi kuhusu maagizo ya mwenyezi Mungu,kuelezea mambo ya Mungu yanayopingana na desturi zetu  kwa mfano kuachana na ushirikina, uchawi,rushwa,ufisadi na kufuata maagizo ya Mungu inakuwa ni vigumu kwa waumini kubadilika lakini ni lazima tuchukue maamuzi magumu kutetea ukweli’’,alisisitiza mhashamu Mtega.
Mhashamu Mtega ametoa rai kwa waumini na viongozi katika ngazi zote kuchukua maamuzi magumu ili kuiokoa dunia na Taifa la Mungu na amewaasa mapadre wasifanye kazi kisiasa badala yake wachukue maamuzi magumu kwa kutetea ukweli pale wanapoona waumini wao wanaonewa .
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:

Post a Comment