Monday, September 10, 2012

Je mikaratusi inamaliza maji ardhini


 Na Albano Midelo
 SIKU za hivi karibuni  baadhi ya viongozi,vyombo vya habari na wadau wa mazingira wameilaumu mikaratusi(eucalyptus)  kutokana na kudaiwa miti hiyo inanyonya maji katika kiwango kikubwa.

Kutokana na hali hiyo yamefanyika maazimio ya kuing’oa miti hiyo  kama ambavyo inafanyika kwenye msitu wa serikali wa milima ya Matogoro iliyopo wilayani Songea mkoani Ruvuma.

Meneja wa hifadhi  ya msitu wa Matogoro Abedinego Sakafu anasema majaribio ya upandaji wa miti ya kigeni aina ya misindano na mikaratusi ulianza mwaka 1957 na upandaji kamili  ulianza mwaka 1961 na kukamilika mwaka 1978 ambapo jumla ya ekari 867.2 zilipandwa .

Hata hivyo Sakafu anabainisha kuwa licha ya miti hiyo kuwa na faida kibiashara  siku zilivyokwenda ilibainika miti hiyo ina madhara kwenye vyanzo vya maji vilivyopo kwenye milima ya Matogoro.


Kwa mujibu wa mhifadhi huyo miongoni mwa madhara ambayo yalianza kujitokeza kwenye msitu huo ni uwingi wa maji yaliokuwa yanatiririka kutoka katika mito iliyopo yalianza kupungua na ubora wa maji pia ulipungua kutokana na kuongezeka kwa  acidity kwenye maji kuliko viwango vinavyotakiwa kwa matumizi ya binadamu.

“Baada ya kuona madhara hayo wizara ya maji iliiomba wizara ya maliasili na utalii ibadili lengo la shamba la miti Matogoro kutoka kuwa la kibiashara hadi kuwa pori la hifadhi kwa kuondoa miti yote ya kigeni na kupanda miti ya asili ambayo ni rafiki wa maji’’,anasisitiza.

Sakafu anabainisha kuwa kazi ya kuondoa miti ya kigeni ilioanza mwaka 2003 ipo katika hatua za mwisho ambapo jumla ya ekari 827 zimekwishavunwa na eneo lililosalia ni ekari 40 tu na kwamba kazi ya kuvuna miti yote inatarajia kukamilika mwaka huu.

Hata hivyo anasema upandaji wa miti ya asili unaendelea kwa wastani wa ekari 40 kwa mwaka na ameitaja miti ya asili ambayo inapandwa kuwa ni minyenda,minyonyo na migwina ambapo jumla ya ekari 550 zimeoteshwa miti hiyo na upandaji unaendelea katika eneo ambalo uoto wa asili ni mdogo.

Hata hivyo Sakafu anasema miti ya kigeni aina ya mikaratusi ambayo imevunwa  hivi sasa inaota na kusambaa katika  maeneo yaliovunwa hali inayoathiri miti ya asili  na kwamba mikaratusi inadumaza ukuaji wa miti ya asili na wakati mwingine kuiua kabisa kutokana na ukuaji wake wa haraka.
 Enock Buja afisa maliasili wa mkoa wa Ruvuma  anaelezea mashaka yake kuhusu utafiti uliofanywa na shirika moja la nje ya nchi mwaka 2000 katika milima ya Matogoro kwamba miti aina ya mikaratusi iliyopandwa katika msitu huo yote ivunwe kwa madai kuwa  inanyonya maji mengi kwenye vyanzo vya maji na kwamba utafiti huo  kwa maoni yake una mashaka.

“Utafiti wa kisayansi unaonesha kuwa sio miti yote aina ya mikaratusi ikiwemo ya milima ya Matogoro ina tabia ya kunyonya maji kwenye vyanzo vya maji,miti ile ni rafiki wa vyanzo vya maji ndiyo maana katika misitu mingine nchini kama ile ya SARNIWAT Njombe na Sao Hill Mafinga imepandwa miti ya mikaratusi tena karibu na vyanzo vya maji ambavyo vimeendelea kutoa maji na hakuna dalili zozote za ukame au maji kupungua”,anasisitiza.

Ameishauri serikali kutafakari tena kuhusu agizo  la kuvuna miti yote ya kupandwa katika msitu huo kwa wakati mmoja na kupanda miti ya asili jambo ambalo ametahadharisha kuwa miti ya asili inachelewa kukua hivyo inaweza kuathiri mlima wa Matogoro na kusababisha vyanzo vya maji kukauka na wananchi wa mji wa Songea kukabiliwa na ukame.

Hata hivyo utafiti uliofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Misitu nchini (TAFORI), umebaini kuwepo kwa aina kadhaa ya miti ambayo kwa kiwango kikubwa inanyonya maji mengi.
 
Kulingana na utafiti wa TAFORI miti hiyo ni Mikaratusi jamii ya Camaldulensis ambayo hunyonya maji kiasi cha milimita 1,240 kwa mwaka na Mikaratusi aina ya Microrhea inayonyonya maji milimita 1,050 kwa mwaka, Mikaratusi ya aina ya Patula nayo hunyonya maji kiasi cha milimita 665 kwa mwaka.

Changamoto iliyopo hivi sasa ni kwamba miti mingi aina ya mikaratusi imekwishaondolewa  isipokuwa tatizo la kujiotea kila inapovunwa ndilo linalosumbua na kuathiri miti ya asili ambayo imepandwa.

 TAFORI kuhusu ukweli  wa miti ya kigeni na matumizi ya maji imebainisha kuwa  mwaka 2000 eneo la mashamba ya miti ya kigeni aina ya mikaratusi duniani kote lilikaribia hekta milioni 18 kati ya hizo asilimia 37 ya eneo hilo lilikuwa barani Afrika na asilimia 73 ya eneo hilo lipo Afrika ya kusini.

Taarifa ya TAFORI  inabainisha kuwa mashamba mengine  makubwa ya mikaratusi barani Afrika yapo katika nchi za Morocco,Angola,Ethiopia na Tunisia  na kwamba katika Afrika mashariki nchi ya Kenya inaongoza  kwa mikaratusi ikifuatiwa na Uganda na Tanzania na kwamba maeneo ya mikaratusi katika nchi za Burundi na Rwanda ni maradufu ya maeneo ya nchi ya Kenya.

Kutokana na utafiti huo TAFORI inabainisha kuwa Tanzania haijumuishi kwenye nchi maarufu kwa upandaji wa mikaratusi na kwamba haiwezi kuchukua nafasi ya kwanza kubaini madhara ya mikaratusi.

Hata hivyo utafiti ambao umetolewa  na TAFORI kuhusu   miti ya kigeni na matumizi ya maji unaonesha kuwa  mikaratusi  iliyopo katika nchi ya Sudan kwa mwaka matumizi yake ya maji ni milimita 1240 wakati mikaratusi katika nchi ya Pakstani matumizi ya maji kwa mwaka ni milimita 1500.

Utafiti huo unaonesha kuwa mikaratusi iliyopo nchini Kenya kwa mwaka matumizi ya maji ni milimita 830 na miti aina ya misindano Tanzania katika msitu wa Sao hill  kwa mwaka hutumia maji milimita 665.

Kulingana na utafiti huo matumizi ya maji kwa mwaka kwa miti mingine na mazao ukilinganisha na mikaratusi unaonesha kuwa miti aina ya mvinje iliyopandwa  Bura nchini Kenya  kwa mwaka inatumia maji  milimita 5437, jamii ya mpingo katika eneo la Bura Kenya kwa mwaka inatumia maji milimita 1143 na Mgunga nchini Paktan unatumia milimita 2100 za maji kwa mwaka.

Utafiti huo unaonesha kuwa mazao ya kilimo nchini Pakstani yakiwemo ngano kwa mwaka yanatumia milimita 330 za maji,pamba milimita 460,mahindi nchini Marekani kwa mwaka yanatumia maji milimita 630 na pamba ya Marekani inatumia maji milimita 630.

Zao la korosho hapa nchini katika wilaya ya Nachingwea kwa mwaka linatumia maji milimita kati ya 814 hadi 1409,mpunga nchini Pakstan kwa mwaka unatumia maji milimita  1620 na miwa katika nchi ya Pakstani inatumia maji milimita 1400 kwa mwaka.

Utafiti huo unaonesha kuna miti kama mvinje na mgunga inatumia maji mengi kuliko mkaratusi na kwamba yapo baadhi ya mazao kama mpunga na miwa ambayo yanatumia maji karibu sawa au zaidi ya mikaratusi.

albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129




No comments:

Post a Comment