Sunday, September 16, 2012

Wauguzi watahadharishwa kuhusu rushwa


Na Albano Midelo
MKURUGENZI wa Kanisa la Upendo wa Kristo Masihi(KIUMA) wilayani Tunduru Mkoani Ruvuma Dk.Matomora Matomora amewatahadharisha wauguzi na madaktari nchini kujiepusha na vitendo vya rushwa wanapowahudumia wagonjwa.
Dk.Matomora alitoa tahadhari hiyo wakati anazungumza kwenye mahafali ya chuo cha uuguzi cha KIUMA  ambapo jumla ya wahitimu 79 walitunukiwa vyeti baada ya kuhitimu mafunzo ya uuguzi ya miaka miwili.
Alisisitiza kuwa uhai wa mgonjwa unamtegemea muuguzi na daktari hivyo ni dhambi kubwa na kitu kibaya kwa muuguzi kuanza kuchangisha fedha kutoka kwa mgonjwa na jamaa zake ambapo amewashauri iwapo mshahara hautoshi ni vema kumdai mwajiri  husika badala ya kuomba rushwa kwa wagonjwa ambao hawana hatia bali wanahitaji huduma za afya.
Awali akitoa taarifa ya chuo hicho Bi. Elvira Makota ambaye ni mkuu wa chuo cha uuguzi KIUMA alibainisha kuwa katika chuo hicho wanachuo walianza mwezi Agosti 2010 wakiwa wanachuo 84 ambapo waliomudu kuhitimu ni wanachuo 79.

Makota alibainisha kuwa katika kipindi cha miaka mitatu chuo cha uuguzi KIUMA kimeweza kuzalisha wauguzi 191 ambao hivi sasa wanafanyakazi ya uuguzi karibu mikoa yote Tanzania.
Akisoma risala ya wahitimu wa chuo hicho kwa niaba ya wenzake mwanachuo Luciana Haule amepongeza mfadhili wa Taasisi ya KIUMA Profesa Dr.Deichmann ambaye ni Rais wa misioni ya Neno na Tendo kutoka nchini Ujerumani ambaye amewezesha vijana kutoka mikoa ya kusini kupata elimu kwa gharama nafuu.
Hata hivyo risala hiyo imezitaja changamoto mbalimbali zinazokikabili chuo hicho kuwa ni pamoja na ukosefu wa umeme wa uhakika unaosababisha mazingira ya wanachuo kujisomea kuwa magumu,pia chuo kimekosa mawasiliano ya mtandao wa intaneti hali inayosababisha wanachuo kukosa taarifa mbalimbali na upungufu wa wauguzi katika hospitali ya KIUMA unaathiri wanachuo katika mazoezi ya vitendo.
Kwa upande wake mgeni rasmi katika mahafali hayo Profesa Dk.Deichmann Rais wa misioni ya Neno na Tendo kutoka nchini Ujerumani ameahidi kuendelea kuisaidia Taasisi ya KIUMA kutokana na maendeleo makubwa ya kiroho na kimwili yaliopatikana.
Taasisi ya KIUMA inaendesha Taasisi mbalimbali ambazo ni chuo cha uuguzi,hospitali,chuo cha ufundi,chuo cha Biblia,sekondari na chuo cha ualimu ambacho kinatarajia kuanza mwaka huu kozi ya stashahada.

 albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:

Post a Comment