Tuesday, September 25, 2012

Chuo Kikuu Huria cha Tanzania sasa ni cha kimataifa


Na Albano Midelo
CHUO kikuu Huria cha Tanzania (OUT) sasa ni cha kimataifa kwa kuwa kina wanafunzi wanaosoma kutoka nchi mbalimbali za Afrika.
Mmoja wa wahadhiri wa OUT kutoka makao makuu jijini Dar es salaam Joseph Mbese anazitaja nchi ambazo wanafunzi wanasoma masomo mbalimbali kutoka OUT kuwa ni pamoja na Uganda,Rwanda,Kenya na Burundi.
Anabainisha kuwa wanafunzi hao wanapata masomo yao kwa njia ya mtandao na kwamba wanasoma masomo yao kupitia mtandao,wanajibu maswali na wahadhili wanasahihisha maswali kwenye mtandao na kisha mwanafunzi hupata majibu ya maswali na mitihani kwa njia ya mtandao.
Hata hivyo anasisitiza kuwa kuanzia mwezi Juni mwaka 2012 masomo yote yamewekwa kwenye tovuti maalum ya chuo ambapo mwanafunzi anasoma masomo yote na kujibu maswali kwa njia ya mtandao na kwamba hakuna masomo ambayo yatatumwa kwa njia ya kutuma vitabu yaani hard copies badala yake masomo yote yatakuwa katika soft copies.

Elimu ya chuo kikuu Tanzania inaelezeka vizuri zaidi kama historia hiyo itajumuisha sehemu ya Afrika mashariki ikijumuisha nchi za Tanzania ,Kenya na Uganda.
Baada ya vita kuu ya kwanza,Afrika mashariki ilikuwa chini ya utawala wa Uingereza na mkoloni huyo alikuwa  na lengo la kupata  asilimia  kubwa ya watu wenye ujuzi na nidhamu ya kazi ndipo alimua kuimarishe utoaji wa elimu ambapo mwaka 1921  kilianzishwa chuo cha Makerere nchini Uganda kikiwa kinatoa elimu ya kidato cha nne na kazi ya diploma kwa watu wote wa Afrika mashariki.
Historia ya vyuo vikuu Afrika mashariki inaonesha kuwa hadi kufikia mwaka 1949 hakukuwa na chuo kikuu hadi chuo kikuu cha London nchini Uingereza kilipoamua kukipandisha hadhi  chuo kikuu  cha Makerere kuwa chuo kikuu kishiriki cha chuo kikuu cha London.
Chuo cha Makerere kiliitwa chuo kikuu cha Afrika mashariki baada ya kupandishwa hadhi ambapo ilimlazimu mtu yeyote wa Afrika mashariki wakati huo ili aweze kupata elimu ya chuo kikuu ni lazima kwenda Makerere nchini Uganda ambapo kati ya mwaka 1956 na 1961 kampasi ya Nairobi nchini Kenya na Dar es salaam Nchini Tanzania zilianzishwa.
Kampasi hizi tatu za Makerere ziliunda shirikisho la chuo kikuu cha Afrika mashariki mwaka 1963 ambapo kutokana na kushindwa kukidhi mahitaji kampasi hizo zilianzisha vyuo vikuu ambavyo ni chuo kikuu cha Makerere,chuo kikuu cha Nairobi na chuo kikuu cha Dar es salaam
Chuo kikuu cha Dar es salaam kilizunduliwa rasmi na Rais wa awamu ya kwanza hayati Julius Nyerere Agosti 29,1970 ambapo miaka ya themanini chuo kikuu cha Dares salaam kiliweza kudahili wanafunzi 900 kwa mwaka wa masomo na baadaye kuanzisha kampasi ya Morogoro ilianzisha kitivo cha kilimo.
Historia ya vyuo vikuu nchini inaonesha kuwa kampasi ya Morogoro ilipandishwa hadhi kuwa chuo kikuu kamili mwaka 1984 na kwamba pamoja na juhudi zote hizo za kupanua elimu ya chuo kikuu  bado mahitaji ya watanzania kujiunga na vyuo vikuu yalikuwa ni makubwa kuliko uwezo wa vyuo vikuu.
Hali hiyo ndiyo iliisukuma serikali kuona uwezekano wa kuanzisha chuo kikuu ambacho kinaweza kutoa elimu kwa njia ya masafa ndipo Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kilianzishwa chini ya sheria ya Bunge namba 17 ya mwaka 1992.
Kati ya mwaka 1993 hadi 1994 chuo kikuu Huria cha Tanzania yaani OUT kilipata mkuu wake wa chuo  waziri mkuu mstaafu Dk.John Malecela na makamu mkuu wa chuo hivi sasa ni professa Tolly Mbwete,udahili ulianza mwaka 1994 wanachuo wa kwanza walikuwa 766.
Akizungmzia mafanikio ya OUT tangu mwaka 1992 hadi 2012 mkurugenzi wa OUT kituo cha Ruvuma Andrew Komba anasema chuo kinakuwa kwa kasi ambapo hadi kufikia mwaka 2011 OUT ilikuwa imefungua matawi karibu mikoa yote nchini na kwamba Chuo Kikuu Huria kinatambuliwa kimataifa.
Anabainisha kuwa OUT ina program 50 za masomo  mbalimbali ambazo zinatolewa Katika ngazi ya cheti,shahada,shahada ya uzamili na shahada ya uzamivu na kwamba  katika kipindi cha miaka ya 1992 hadi 2012 taasisi za kidini ,mashirika na watu binafsi kuthubutu kuingia kwenye mchakato wa kutoa elimu ya chuo kikuu bado kuna kazi kubwa .
“Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kimekuwa msaada mkubwa kwa wanyonge,wasiokuwa na nguvu za kiuchumi,waliokuwa pembezoni na kutengwa na mifumo mbalimbali,leo hii sio ajabu hata mfungwa anaweza kusoma ‘’,alisisitiza.
Utafiti ambao ulifanywa na Benki ya Dunia  yaani WB mwaka 2000 katika  baadhi ya nchi za Afrika, unaonesha kuwa  kati ya watu 100,000 wenye sifa na nia ya kupata elimu ya chuo kikuu ni watu 43 tu ndiyo wanapata fursa hiyo ambapo nchini Afrika ya kusini  kati ya watu 100,000 watu1524 wanapata fursa.
Kwa mujibu  wa utafiti huo nchini Nambia kila watu 100,000 wenye sifa za kupata elimu ya juu ni watu 738 wanapata elimu ya chuo kikuu na kwamba utafiti mwingine ambao ambao unafanana na huo uliofanywa hapa nchini mwaka 2006  unaonesha kuwa kati ya watu 100,000 watu 129 wanapata fursa ya chuo kikuu.
Takwimu za Tume ya Vyuo vikuu Tanzania TCU kuhusu udahili wa mwaka 2011/2012 zinaonesha kuwa  jumla ya wanachuo 37,924 na kwamba  vyuo vikuu,vyuo vikuu vishiriki na taasisi za elimu ya juu zilizoko nchini hivi sasa zina uwezo wa kudahili wanafunzi 40,000 kwa mwaka.
Kutokana na mchango mkubwa ambao OUT inatoa kwa elimu ya chuo kikuu Komba anatoa wito kwa watanzania kutumia fursa ya OUT ambayo inatoa elimu ndani ya mazingira ambayo mtu anaishi  badala ya kusafiri kwenda mbali kwa lengo la kuitafuta elimu hiyo.

Kwa upande wao wanachuo wanasoma chuo kikuu Huria cha Tanzania  wameishukuru serikali kwa kuanzisha Chuo kikuu Huria ambapo wamesema hadi sasa idadi kubwa ya watanzania wamefanikiwa  kuhitimu shahada mbalimbali na kuongeza ufanisi katika kazi zao, hivyo kupanda vyeo katika fani na nyadhifa zao.




No comments:

Post a Comment