Saturday, December 29, 2012

Bomoa bomoa Nyasa iendane na ulipaji wa fidia



Na Albano Midelo

WAKARA wa  barabara mkoa wa Ruvuma TANROAD wametoa mwezi mmoja kwa wakazi wa mwambao mwa ziwa Nyasa kuanzia Mbambabay hadi Lituhi kubomoa nyumba zao ambazo zinadaiwa zimejengwa katika hifadhi ya barabara.

Meneja wa TANROAD mkoa wa Ruvuma injinia Abrahamu Kisimbo anadai nyumba hizo zinabomolewa kutokana na sheria ya barabara  yaani Road Act namba 13 ya mwaka 2007 kifungu namba 29  ambacho kinasema eneo la hifadhi ya barabara ni mita 30 kutoka katikati ya barabara kwa kila upande.

Anabainisha kuwa kwa sheria hiyo hairuhusiwi kwa mtu au taasisi yoyote binafsi kujenga ndani ya eneo la hifadhi ya barabara na kwamba kutokana na hilo ametoa notisi ya mwezi mmoja kila mwenye nyumba au jengo kuvunja vinginevyo  ofisi yake itavunja jengo na muhusika atatakiwa kurejesha gharama zitakazotumika katika utekelezaji wa zoezi hilo.

Katika mji mdogo wa Liuli pekee nyumba 74  zinatarajiwa kubomolewa  hali ambayo imeleta malalamiko kwa wakazi hao ambao wanaamini serikali haijawatendea haki kwa madai kuwa nyumba zao zimejengwa  kwa mujibu wa sheria za halmashauri ya wilaya.


Wakizungumza na mwandishi wa makala haya wananchi wapatao 74 ambao ni wahanga wa barabara katika eneo la Liuli  wanasema wamesitushwa  na kushangazwa na kitendo cha TANROAD kuweka alama nyekundu ya x na kumkabidhi kila aliyewekewa alama hiyo barua ya amri ya kubomoa kwa hiari nyumba yake ndani ya kipindi cha mwezi mmoja.

Mwenyekiti wa wahanga hao John Komba  anasema kutambuliwa kwa Liuli kuwa mji mdogo kumetokana na uthibitisho uliofanywa kwa vipimo ambao ulifanywa na idara ya ardhi ambapo ramani ya mji huo sasa ipo makao makuu jijini Dar es salaam ili kusajiriwa rasmi.

“Watu wengi wa Liuli tunaishi ndani ya maeneo yenye alama za mji zinazotambuliwa(beacon) ramani hiyo inaonyesha mitaa na barabara kuu tunaomba TANROAD waitambue ramani hiyo ya mji wa Liuli uliopimwa mwaka 2004,kwanini ramani hiyo isifuatwe na TANROAD, barabara inapitishwaje sehemu nyingine,upimaji wa idara ya ardhi hautambuliki?,alihoji Komba kwa niaba ya wenzake.

Wamedai kuwa kutokana na barua ya TANROAD  ya Septemba 22,2012 inayowapa mwezi mmoja kubomoa nyumba zao kwa madai kuwa wamevamia hifadhi ya barabara,wao wanapinga na kudai kuwa TANROAD ndiyo imevamia makazi ya watu kwa kuacha barabara yao ya asili  na kuvamia barabara ambayo wananchi wenyewe walijiundia kwa shughuli zao mbalimbali.

“Waziri Magufuli tutendee haki kwa sababu Katika barabara hii TANROAD haikuweka tangazo lolote wala alama ya beacon kama zilivyowekwa katika maeneo mengine,wala kutolea taarifa yoyote kwa jamii ili isivuke alama zao hivyo kuthibitisha kuwa barabara haikuwa na mipaka wala kizuizi chochote,TANROAD wameivamia jamii’’,alisisitiza mwenyekiti huyo.

Historia inaonesha kuwa barabara ya Mbambabay-Liuli hadi Lituhi imejengwa tangu mwaka 1968 ikiwa chini ya Halmashauri ya wilaya na ilikabidhiwa TANROAD mwaka 2007,hali hiyo ndiyo inawafanya wakazi hao wa Liuli kuhoji nini kiliwafanya TANROAD wasiwape taarifa za sheria yao mapema iwapo barabara hiyo ilikuwa chini yao.

Katibu wa wahanga hao Lukas Kaunda amesisitiza kuwa wanatambua vya kutosha kuwa ardhi ni mali ya serikali na inapotaka ardhi kutoka kwa raia wake hupewa na kuichukua kwa utaratibu na sio kwa kushitukiza kama walivyofanya TANROAD.

Kutokana na hali hiyo wakazi hao 74 ambao nyumba zao zinatarajiwa kubomolewa ,wameiomba TANROAD na serikali iwaandalie maeneo mbadala ya kuishi mara watakapoondoka katika maeneo yao ya sasa.

Kwa kuwa nyumba zao zitabomolewa bila sababu mahususi,wananchi wameiomba  TANROAD na serikali kuandaa malipo kulingana na gharama za kujenga nyumba mbadala.

Hata hivyo wakazi hao wameomba kuwa kwa kuwa nyumba zao zitabomolewa katika majira haya ya mvua,wameiomba serikali  iwaandalie mahema kwa kujikinga na mvua za masika na kwamba wanalaani kitendo cha serikali kuikubalia TANROAD  kubomoa nyumba zao kipindi cha masika.

Mwenyekiti wa kijiji cha Liuli Roja Lihonga anahoji,inakuwaje mahali penye ramani halafu mwingine anatengua?,hivyo ndivyo halali ya maisha ya mtanzania?,barabara ni moja ya maendeleo sasa inakuwaje mtu avunje nyumba ndani ya mwezi tena kipindi cha mvua familia yake itaishi wapi’’,alihoji Lihonga.

Mwenyekiti huyo alidai kuwa wananchi wa Liuli wamesimamisha shughuli zote za ujenzi kutokana na kutolewa ramani  na kwamba hadi sasa ramani hiyo haijarudi toka makao makuu licha ya kuandika barua kwa mkurugenzi mtendaji kuomba ramani hiyo.

Diwani wa kata ya Liuli Charles Chawila anasema ramani ya mji wa Liuli inaonesha barabara kuu imepita nje ya mji huo ambapo TANROAD  wanadai kukataa kwa madai kuwa ramani hiyo bado haijarudi toka makao makuu hivyo hawawezi kufanyia kazi wazo tu la Halmashauri.

Diwani huyo ametoa wito kwa mkurugenzi wa Halmashauri kufuatilia ramani hiyo haraka kabla ya ujenzi wa barabara ya Mbambabay-Liuli kuanza ili kuepusha hasara ya wananchi wa Liuli kubomolewa nyumba 74  ambazo zipo tayari ndani ya ramani ya mji wa Liuli.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga Shaibu Nnunduma amesema ramani ya mji wa Liuli inafuatiliwa,hata hivyo amedai kuwa wananchi wamefuata barabara hiyo ambayo ilikuwepo tangu zamani.

Wananchi hao wanahoji kuwa wameshirikishwaje katika mabadiliko ya sheria ya TANROAD  ya mwaka 2007 ya kupanua barabara meta 30 kila upande kwenye serikali za vijiji na kata kwa madai kuwa sheria hizo zimeanzia mwaka 1967 na kurekebishwa mwaka 1979 na kubadilishwa tena mwaka 2007.

Shirika linalotetea haki za binadamu kwa kutoa msaada wa kisheria kwa watu wasiokuwa na uwezo(NOLA) limetoa pingamizi ya notisi ya siku 28 ya kubomoa nyumba kwa wananchi wa kijiji cha Nkali kata ya Liuli.

Mwanasheria wa NOLA James Maroda katika pingamizi ambalo amemwandikia meneja wa TANROAD mkoa wa Ruvuma pamoja na mambo mengine ametoa pingamizi hilo kufuatia ofisi ya TANROAD kutumia sheria ya mwaka 2007 ya barabara yaani Road Act namba 13 kifungu cha 29.

Mwanasheria huyo amedai kuwa sheria hiyo ni mpya na kwamba wakazi wa Liuli hawawezi kuwa wahanga wa sheria hiyo ambayo imetungwa wananchi wakiwa tayari wamejenga nyumba zao ambapo anasema wanastahili kulipwa fidia ya TANROAD endapo nyumba zao zitabomolewa.





No comments:

Post a Comment