WANAFUNZI wengi
wanaosoma katika shule za sekondari wilayani Tunduru mkoani Ruvuma wanakatishwa
masomo yao wanapofikia kidato cha pili na cha tatu baada ya kupata mimba na kuolewa wakiwa
shuleni.
Hali hiyo inatokana
na historia ya wakazi wa wilaya hiyo ambao ni kabila la wayao kutokuwa na
mwamko katika elimu hasa kutokana na kutoa kipaumbele kwa desturi na mila za
kabila hilo ambazo zinatoa fursa zaidi katika mila potofu za unyago,msondo na
jando kwa wanafunzi wa shule za msingi
na sekondari hali ambayo inaathiri suala zima la elimu.
Takwimu ambazo
zimetolewa na mkuu wa wilaya ya Tunduru Chande Nalicho zinaonyesha kuwa mwaka
2012 wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na sekondari mwaka huu walikuwa ni 2788
hata hivyo hadi kufikia mwezi Aprili mwaka huu ni wanafunzi 1710 tu ndiyo
walioripoti hali ambayo inakwamisha maendeleo ya elimu.
Flavian Nchimbi kaimu afisa
elimu msingi wilaya ya Tunduru anasema tatizo la mimba katika shule za
msingi zimepungua ukilinganisha na miaka mitatu nyuma kulikuwa na mimba karibu
250 ambapo takwimu za mwaka jana zinaonyesha kuwa katika shule za msingi
zililipotiwa mimba 16 na kwamba kuanzia mwezi Januari hadi Aprili mwaka huu
imeripotiwa mimba moja tu.
Hata hivyo afisa
elimu sekondari wilaya ya Tunduru Ally Mtamila amekiri tatizo la mimba na ndoa
za utotoni kwa wanafunzi wa shule za sekondari kuwa ni kubwa ambapo wanafunzi
wa kike wanakatishwa masomo kwa mimba au kuolewa.
Sarah Michael(15)
mkazi wa Tunduru alikuwa anasoma katika shule ya sekondari Makita ambapo alipewa
ujauzito akiwa kidato cha tatu na mwanaume ambaye alitoroka mara baada ya tukio
hilo hali ambayo ilimfanya aishi kwa shida hadi alipojifungua salama mtoto wake
wa kiume.
“Baada ya kupata
ujauzito niliacha masomo wazazi walinipokea licha ya kupata misukosuko mingi
hasa kutoka kwa baba yangu mzazi,nimejifungua naendelea kumlea mwanangu katika
mazingira magumu sana kwa kweli nakumbuka shule mwaka huu ningekuwa namaliza
kidato cha nne’’,alisema.
Sarah alisema
anapenda sana kusoma lakini wazazi wake hawana uwezo wa kumsomesha hivi sasa hivyo endapo atampata
mtu wa kumsomesha anaweza kuendelea na masomo ya sekondari na kwamba kitendo
cha kupata mimba na kukatisha masomo yake kimetoa fundisho kubwa kwake hivyo
hawezi kurudia makosa ambayo yameharibu ndoto za maisha yake.
Hata hivyo anasema
baba yake ni mwajiriwa wa serikali anafanya kazi ya uaskari magereza wilayani
Mbinga ambaye kitendo cha yeye kukatishwa masomo kilimchukiza na alitaka
mtuhumiwa kukamatwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria,hata hivyo wazazi wa pande zote mbili waliyamaliza na
kufuta kesi.
“Hivi sasa baada ya
mwanangu kukua nimemwomba baba anisomesha ili niweze kuendelea na masomo,lakini
baba bado ana hasira amekataa na kusema ningoje kwanza nijifunze maisha kwa
kuwa mimi niliacha shule na kukimbilia mambo yaliosababisha kupata mimba
naendelea kumuomba radhi baba kwamba sitarudia tena nikipata nafasi ya
kusoma’’,alisema kwa huruma.
Salima Hamad(15)
mkazi wa Tunduru anasema alikatishwa masomo yake baada ya kupata mimba akiwa kidato cha tatu mwaka 2012 na kwamba wazazi wake walichukizwa
na kitendo hicho ,walifungua kesi ya mwanaume aliyempa mimba,alikamatwa na
kutiwa ndani hata hivyo mwanaume huyo ametorokea nchini Msumbuji hadi leo.
“Wazazi walinisakama
pamoja na viongozi wa serikali ya kijiji,nilitamani kutoa mimba lakini nilipiga
moyo konde,nilivumilia kulea mimba katika mazingira magumu kwa kuwa wazazi
wangu ni masikini hadi nikajifungua salama kwa kufanyiwa upasuaji mtoto wa
kike,natamani kusoma lakini sina uwezo’’,alisisitiza.
Salima anasema wazazi
wake wamekataa kumsomesha na kudai kuwa hawana uwezo wa kumpeleka tena shule na
hivi sasa anaishi kwa kujitazamia na kuuguza kidonda ambacho kimetokana na
kujifungua kwa upasuaji.
Hemed Ally mwanafunzi
wa kidato cha nne shule ya msingi Frank Weston wilayani Tunduru anasema katika mafunzo ya msondo na unyago wanafunzi wa kike wanaelezwa faida za kuishi
na mume lakini hawafundishwi madhara ambayo wanaweza kupata kwa kushiriki
katika ndoa wakiwa wadogo hali hiyo ndiyo inawahamasisha wanafunzi kujiingiza
kwenye ngono na kushawishika kuolewa na kupata mimba wakiwa wanafunzi.
Rehema Sara
mwanafunzi wa kidato cha nne sekondari ya Mgomba anasema mila za unyago na msondo zimesababisha
wanafunzi wengi wa kike katika shule hiyo kuacha masomo kwa kupata mimba au
kuolewa ambapo hivi sasa katika darasa lao waliofanikiwa kufika kidato cha nne
ni wanafunzi 106 tu kati ya wanafunzi zaidi ya 230 walioanza nao kidato cha
kwanza mwaka 2010.
Sarah mkombozi wa
kidato cha nne sekondari ya Mgomba ambaye alifanyiwa ngoma ya unyago na msondo
akiwa darasa la tatu amekiri moja ya mambo ambayo wanafundishwa katika msondo
na unyago ni kufanya mapenzi na watu
wazima na kwamba kukataa kufanya hivyo
ni kuvunja mila na desturi za wayao’’,alidai mwanafunzi huyo.
“wenzangu wengi ambao
nilikuwa nao shule ya msingi na wengine ilitakiwa niwe nao sekondari wameacha
masomo kwa kuwa wana watoto baada ya kupata mimba na wengine wameolewa na
kuachika hivyo wanaangaika na maisha’’,alisisitiza.
Mkuu wa wilaya ya Tunduru Chande Nalicho amekiri
mila na desturi za kabila la wayao zinachangia wilaya hiyo kuwa duni kielimu
hata hivyo amesema tayari serikali imeunda kikosi kazi cha kuonana na viongozi
wa mila, makungwi na manyakanga kuwaelimisha juu ya utoaji wa elimu kwa watoto
wa kike kupenda masomo tofauti na sasa ambapo kundi hilo limekuwa likifundishwa
kukabiliana na maisha ya ndoa hali iliyosababisha kuwepo kwa matukio mengi ya
ndoa za utotoni wakiwa shuleni.
“Mila
na desturi za kabila la wayao kuwafanyia unyago wanafunzi ndiyo chanzo kikuu cha tatizo hili,sisi kama
serikali ili kukabiliana na tatizo hili tumefanya vikao na viongozi wasiokuwa
rasmi lakini wanakubalika katika jamii wakiwemo makungwi, mangariba, masultani,mamwenye,mashehe
na maimamu kwa kuzingatia tumejadili kwa pamoja tatizo hili”,anasisitiza.
Kwa
mujibu wa Takwimu za Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, wasichana 8000 kila
mwaka huacha shule kutokana na ujauzito. Kati yao 3,000 ni wanafunzi wa shule
za msingi.
Kila
siku, wanawake 24 hufariki dunia kutokana na mimba au wakati wa kujifungua.
Wanawake watano mpaka sita wanaofariki kati ya hao ni watoto wadogo, watoto hao
hufariki dunia kwa kuwa miili yao haijakomaa vya kutosha kwa ajili ya kujifungua.
Naibu
mwakilishi mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa Linaloshughulikia Watoto
(UNICEF), Mohamed Safieldin anasema mbali na athari hizo, pia virusi vya ukimwi
(VVU), vinavyosambaa kwa kasi kwa wasichana hao. Tanzania kuna watoto yatima
milioni 1.3 walioathirika kwa ukimwi.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

Habari hii imenigusa sana ..mara nyingi nimekuwa nikisikitika sana kuhusu jambo hili. Wasichana wengi sana wanakatishwa masomo, halafu wavulana hawachukuliwi hatua..ndiyo wasichana ni wadhaifu na tamaa nyingi..lakini pia hata wavulani nao wanatamaa..Sio haki kabisa kijana wa kiume aendelee na masomo na msichana afukuzwe shule....nitaiweka pale kwangu kasho ile tupata maoni ya wasomaji wengine maana wote tunapenda kitu kimoja...
ReplyDelete