BIDHAA za tumbaku kwa vyovyote
itakavyotumika inaleta madhara makubwa kwa mtumiaji ikiwemo kumsababishia
maradhi mbalimbali na hata kifo.
itakavyotumika inaleta madhara makubwa kwa mtumiaji ikiwemo kumsababishia
maradhi mbalimbali na hata kifo.
Takwimu za shirika la afya
ulimwenguni(WHO) za mwaka 2003 zinaonesha kuwa kila baada ya sekunde kumi mtu
mmoja hufariki dunia kutokana na maradhi yanayotokana na matumizi ya bidhaa za
tumbaku.
Inakadiriwa kuwa ifikapo mwaka 2025
vifo vinavyotokana na matumizi ya
tumbaku vitaongezeka kwa kiwango cha asilimia 70 na kwamba mwaka 2030 watu
milioni 10 watakufa kila mwaka kutokana na uvutaji wa sigara ulimwenguni.
Kulingana na WHO,asilimia 70 ya wavutaji hao watatoka katika nchi
zinazoendelea ikiwemo Tanzania ambapo wanaume wanaovuta sigara barani Afrika ni
asilimia 36 na wanawake wanaovuta sigara katika Afrika ni asilimia tisa. Hata hivyo hapa nchini inakadiriwa
kuwa katika baadhi ya mikoa wanaume wanaovuta sigara ni asilimia 46 na wanawake
wanaovuta sigara ni asilimia nne tu.
Wataalamu wa afya wanasema matumizi ya
tumbaku yapo ya aina nyingi ikiwa ni pamoja na kubwia,kunusa,kuvuta na kutafuna ambapo
wananchi wengi katika maeneo ya mijini
na vijijini wamekuwa wakitumia tumbaku kwa wingi bila kujua madhara yanayoweza
kuwapata kiafya.
Kwa mujibu wa WHO matumizi makubwa ya
tumbaku yanaendelea zaidi katika nchi zinazoendelea kuliko zilizoendelea
kutokana na juhudi za makampuni makubwa yanayotengeneza bidhaa zinazotokana na
tumbaku kupanua wigo wao kibiashara kwa kuweka matangazo mbalimbali.
Kwa mujibu wa wataalam wa afya yapo
magonjwa mbalimbali ambayo yanaweza kusababishwa na matumizi ya tumbaku yakiwemo
Madhara mengine ya tumbaku na bidhaa zake ni pamoja na kuathirika kwa mimba,mtoto
anayezaliwa kuwa mlemavu wa akiri, kupungua kwa nguvu za kiume,vidonda vya
tumbo,mtoto wa jicho,kunyonyoka nywele na kuziba kwa mishipa ya damu.
Matumizi ya
bidhaa za Tumbaku iwe kwa kuvuta au kutafunwa husababisha shinikizo la
damu ambalo husababisha ugonjwa wa moyo, kiharusi, puma, matatizo ya kifua,kansa
ya mdomo,kansa ya mapafu,kansa ya figo,kansa ya matiti,kansa ya tumbo,kansa ya
koo,watoto kuzaliwa na uzito mdogo na kuwa na matatizo ya kiafya ambayo
humwezesha mtoto kufa haraka akiwa bado mchanga,matatizo ya meno,uvimbe katika
ubongo,ngozi kunyauka.

Kwa mujibu wa wataalamu, tiba ya magonjwa hayo inahitaji gharama kubwa hali inayosababisha wengi kushindwa kutibiwa kutokana na ukweli kuwa wananchi wengi ni masikini na hawana uwezo wa kumudu gharama za matibabu hivyo wanaugua na hatimaye kupoteza maisha.
Katika kukabiliana na madhara ya
matumizi ya tumbaku,dunia imetenga siku maalum ya kutotumia tumbaku duniani
ambayo huadhimisha kila mwaka Mei 31, hata hivyo utafiti umebaini kuwa bado
tatizo la matumizi ya tumbaku linaongezeka kwa kasi kubwa katika jamii mwaka
hadi mwaka.
Sababu kubwa ya kuendelea kwa matumizi
ya tumbaku na bidhaa zake ni wananchi kutokuwa na uelewa wa kutosha kuhusu madhara ya tumbaku hali inayochangia
kuongezeka kwa madhara yatokanayo na tumbaku.
Kutokana na madhara hayo makubwa ya
zao la tumbaku na matumizi yake katika jamii,serikali ,wadau na jamii kwa
ujumla inatakiwa ishirikiane kwa pamoja kuhamasisha na kuelimisha watumiaji wa
tumbaku ili waepuke tabia hiyo na hatimaye kulinda afya yao.
Uvutaji wa sigara ni njia moja kuu ya
utumiaji wa tumbaku.Moshi utokanao na jani la tumbaku una sumu kali
iitwayo'nikotini' na mvutaji sigara huivuta sumu hii ambayo huchanganyika na hewa ya sumu
ya 'kaboni monoksaidi' na lami ya moshi wa tumbaku
Wataalamu wanabainisha kuwa katika
sigara kuna kemikali zipatazo 4000. Kemikali zote hizi kwa pamoja ndizo
zinazoleta madhara ya moja kwa moja kwa mtumiaji na kwa watu wengine walio
karibu na mvutaji sigara.Nikotini pamoja na kemikali hizo za moshi wa tumbaku uliokwama
kwenye njia ya hewa humsababishia mvutaji magonjwa,ikiwa ni pamoja na saratani ya
koo,mapafu,kizazi na kipofu cha mkojo.Husababisha pia shinikizo kubwa la damu,vidonda
vya tumbo,kikohozi sugu na kubanwa kifua.
Kemikali za sumu zipatazo 4000
zimethibitishwa kuwepo katika jani la tumbaku,na ambazo zikiingia mwilini hata kwa kiasi kidogo tu humsababishia mvutaji na
walio karibu naye kuathirika.
Kulingana na wataalamu wa afya, moshi
wa sigara humfikia mtu asiyevuta toka kwa mvutaji aliye karibu naye na
kumsababishia madhara mbalimbali ikiwa ni pamoja na kukohoa,kupiga chafya ovyo,kuumwa
kichwa au kichefuchefu,kubanwa pumzi.
Utafiti umebaini kuwa tabia ya wazazi
kuvuta sigara mbele ya watoto wao ni chanzo cha watoto kuwaigiza na kuanza
uvutaji wa sigara mapema ambapo inakuwa vigumu kwa mvutaji kukemea uvutaji,ndiyo
maana mara nyingi watoto wa wanaovuta sigara huishia kuwa wavutaji.
Makampuni yanayotengeneza mazao ya
tumbaku yakiwemo ya sigara yanatakiwa
yaelimishe wazi wazi bila kificho kuhusu madhara ya sigara kwa watumiaji badala
ya kuweka matangazo ya kusifia sigara huku madhara yakiwa hayajaoneshwa wazi wazi.
Matangazo ya kuandika neno 'ONYO'kwa
maandishi yasiyoonekana kwa urahisi juu ya paketi za sigara hayawezi kusaidia
jamii kutambua kwa urahisi madhara ya bidhaa za tumbaku.
Matangazo hayo yanachochea matumizi ya
tumbaku,licha ya wananchi wengi kutokuwa na uelewa wa kutosha kuhusu madhara
yatokanayo na matumizi ya bidhaa za tumbaku
Baadhi ya nchi ulimwenguni
zimeshatunga sheria kali zinazomlinda yeyote atakayeathirika kutokana na
matangazo yanayoshawishi jamii kutumia au kuzalisha tumbaku ambapo Kupitia
vyombo vya sheria,waathirika hudai fidia ya mamilioni ya fedha ambayo makampuni
ya tumbaku hulazimika kulipa fidia hizo.
Hata hivyo serikali imeanzisha sheria ya
udhibiti wa bidhaa za tumbaku kwa ushirikiano na chama cha afya ya jamii
Tanzania(TPHA) hali ambayo inaonesha matumizi ya tumbaku yanaweza kupungua
hivyo jamii kuwa yenye afya bora.
Wakulima katika maeneo ambayo wanategemea kilimo cha tumbaku kama zao la biashara ni vema sasa wakazalisha zao mbadala la tumbaku kama vile ufuta,paprika alizeti na mazao mengine kulingana na hali ya hewa ya eneo husika ambayo hayana madhara katika afya na hata soko lake ni kubwa.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:
Post a Comment