ASKOFU mkuu mstaafu
wa jimbo kuu la Songea Norbert Mtega amewaaga rasmi waumini wake katika kanisa
kuu la kiaskofu la jimbo kuu la Songea
baada ya kustaafu majukumu ya uaskofu tangu Mei 15 mwaka huu.
Askofu mkuu mstaafu
Mtega alitumia misa zote tatu Jumapili hii katika kanisa hilo kuwaaga rasmi
maelfu ya waumini ambao walikusanyika kwa wingi ndani na nje ya kanisa hilo huku baadhi yao wakiwa na majonzi
hali iliyosababisha baadhi ya akinamama kutokwa na machozi kutokana na kile
walichodai kuwa alikuwa ni msaada mkubwa kimwili na kiroho.
Akihubiri katika kila
adhimisho la misa takatifu Askofu mkuu mstaafu Mtega ambaye amekuwa askofu mkuu
jimbo kuu la Songea kwa miaka 22 alisema aliamua kuandika barua ya kuomba
kustaafu kwa Baba mtakatifu kutokana na kukabiliwa na matatizo ya kiafya .
“Ndugu zangu waumini
nipo hapa leo katika adhimisho la misa hii kwa namna ya pekee nitoe ushuhuda
kwenu,nimemaliza kazi yangu hapa Jumatano Mei 15 kama kiongozi lakini kama
Askofu ningali bado kazini,bado nipo kati yenu kama mwanasongea, mtu wa imani
ya kanisa katoliki na mimi ni muumini mwenzenu’’,alisisitiza.
Hata hivyo alisema
katika uongozi wake wa miaka 22 akiwa Askofu mkuu wa jimbo kuu la Songea
ameshuhudia utendaji wa ajabu wa roho mtakatifu ndani ya wahudumu na waumini
wote wa kanisa hilo na kusisitiza kuwa chochote ambacho kimetendeka katika
jimbo hilo kwa miaka 22 ambayo yeye alikalia kiti hicho mtendaji mkuu amekuwa
mtu asiyeonekana ambaye ni Mungu roho mtakatifu.
“Kanisa ni la Mungu
roho mtakatifu,kila kauli na mkakati ni wa roho mtakatifu,mimi nikiwa katika kiti hicho kwa miaka 22 imeshuhudia
mapadre,watawa na waumini wanavyotenda kazi ,nasema hayo yote ni matendo makuu
ya Mungu,kwa hiyo leo ninapowaaga wajibu wangu ni kusema asifiwe na kutukuzwa
Mungu,nawaomba tuungane katika neno la imani la kumshukuru na kumtukuza Mungu
kwa matendo yake makuu’’,alisema.
Katika nafasi hiyo
Askofu mkuu mstaafu Mtega amekiri kuwa watendaji wakuu katika kipindi chote
walikuwa ni waumini ambao wamewezesha jimbo kuu la Songea kusimama kiimani kwa
kutoa mchango wa hali na mali.
Hata hivyo alisema
baada ya yeye kustaafu jimbo linaingia katika kipindi cha mpito hadi hapo
atakapopatikana Askofu mkuu mteule wa jimbo kuu la Songea na kwamba katika
kipindi hiki cha mpito Baba mtakatifu amemweka askofu wa jimbo la Iringa
mhashamu Tarcius Ngalalekumtwa awe msimamizi wa kitume.
Alisema katika
kipindi hiki cha mpito Baba mtakatifu anaendelea na mchakato wake wa kuandaa,
kumteua na kumchagua atakayekuwa askofu mkuu wa jimbo kuu la Songea na kwamba
waumini waendelee kusali kwa kuwa askofu mteule atapatikana.
“Nawaomba waumini
wote tuingie katika kipindi muhimu cha sala
maombi,matumaini na imani kubwa ili afike roho mtakatifu na kujaa kwa
Baba mtakatifu na waumini wote ili tupate askofu mkuu haraka iwezekanavyo, pia
nachukua nafasi hii kuwaombeni radhi niliowakosea na mimi nawasamehe wote walionikosea’’,alisema.
Akizungumza kwa niaba
ya waumini wa jimbo kuu la Songea Naibu Askofu jimbo kuu la Songea padre
Camilius Haule ametoa shukurani za dhati kwa askofu mkuu mstaafu Norbert Mtega
kwa kujitoa kwa dhati kulihudumia jimbo kuu la Songea kwa miaka 22 kwa kutoa
karama zake zote kwa ustawi wa jimbo hilo.
“Baba askofu mkuu
tunakushuru kwa kukubali kwako kujitoa kafara kwa ajili ya kutimiza kazi za
Yesu kristo katika ekaristi takatifu,neno la Mungu na sakramenti ya
kitubio,umedhihirisha kuwa ni
nabii,kiongozi, mchungaji na kuhani unayejitoa sadaka kwa mfano wa Yesu Kristo’’,alisema.
Padre Haule ameahidi
kwa niaba ya waumini kumsindikiza kwa sala askofu mkuu mstaafu Mtega
anapokwenda nje ya nchi kwa ajili ya kupata matatibu ili Mungu roho mtakatifu
aweze kumponyesha katika maradhi yanayomsumbua hatimaye aweze kurudi jimboni
Songea akiwa mzima wa afya.
John Komba mkazi wa
Songea amesikitishwa na hatua ya askofu mkuu Mtega kustaafu na kudai kuwa bado
kanisa lilikuwa linamtegemea katika majukumu mbalimbali kutokana na kazi kubwa
ambayo ameifanya katika kipindi chote cha miaka 22 akiwa askofu mkuu wa jimbo
kuu la Songea.
“Askofu mkuu mstaafu
Mtega ndiye aliyetufundisha kujitegemea,kabla yake waumini tulikuwa tegemezi
tunangojea misaada kutoka kwa wamisionari,hivi sasa tunaweza kujitegemea,
waumini wanajenga makanisa wao wenyewe katika hili tutamkumbuka sana’’,alisema
Komba.
Njafura Njafura
ambaye ameishi mjini Songea tangu miaka 1960,alisema askofu mkuu mstaafu Mtega
ameleta mabadiliko makubwa katika jimbo hasa kusimamia elimu kikamilifu ambapo
hivi sasa kuna vyuo vikuu vya kanisa ambavyo alivitaja kuwa ni chuo kikuu cha
SAUT tawi la Songea na chuo kikuu cha mtakatifu Joseph.
“Mimi binafsi
sijisikii vizuri kustaafu kwa askofu mkuu Mtega,nimekosa amani kabisa
moyoni,hata hivyo waumini wenzangu nawaasa kumuenzi katika mambo yake mema
kwa kuyaendeleza ikiwemo sera yake ya kulitegemeza kanisa ambayo
amefanikiwa kuieneza katika jimbo kuu la Songea, kuna mifano kadhaa ya parokia
mpya ambazo zimeanzishwa na waumini wenyewe ikiwemo parokia ya
Mjimwema,Bombambili na Subira na nyinginezo’’,alisema.
Catherine Nchimbi(70)
ambaye alitokwa na machozi wakati askofu anawaaga waumini kwa kuwapungia
mikono,alisema anasikitika sana kwa kitendo cha baba askofu kustaafu kwa kuwa
walikuwa wanamtegemea sana kimwili na kiroho na kwamba kitendo cha kustaafu
kwake amekipokea kwa shingo upande.
“Sina namna yeyote
kwa kuwa amestaafu na leo anatuaga rasmi,baba huyo alinisaidia sana katika
maisha yangu ya kiroho na kimwili,sifahamu kwanini amestaafu ghafla,mbona bado
ana nguvu za kuendelea kuwahudumia waumini wa Songea,tunamlilia sana
’’,alisisitiza.
Ally Rashid fundi
cherehani mjini Songea anasema askofu mstaafu Mtega alikuwa kiungo muhimu kwa
dini zote na kwamba licha ya kuwa yeye ni mwislamu,aanakiri kuwa askofu mkuu
mstaafu Mtega ameibadilisha Songea hasa katika sekta ya elimu na afya vitu
ambavyo ni muhimu bila kujali wewe ni dini gani.
“Taarifa za kustaafu
kwake sio tu zimewashitua wakristo pekee bali hata sisi waislamu tunatambua
mchango wake,si unaona hapa leo Jumapili baadhi yao waliposikia kwenye vyombo
vya habari hawakuamini hadi leo wamefika kushuhudia anapowaaga waumini rasmi,askofu
Mtega alijenga mahusiano mazuri na dini zote’’,alisisitiza.
Julius Konala
mwandishi wa habari wa gazeti la Tanzania Daima Songea amewatahadharisha
wanahabari kuacha kuandika habari za uzushi kuhusiana na kustaafu kwa Askofu
mkuu Mtega badala yake kuandika habari za ukweli kutoka vyanzo vya kuaminika na zilizofanyiwa utafiti wa
kina ili kujiepusha na kashfa.
“Baadhi ya wanahabari
wameandika askofu mkuu Mtega amejiuzuru jambo ambalo sio kweli,ukweli ni kwamba
askofu mkuu Mtega amestaafu majukumu ya uaskofu lakini uaskofu wake umebakia
palepale ndiyo maana hata leo ameongoza na kuhubiri katika kanisa kuu la
kiaskofu’’,alisema.
albano.midelo@gmail.com,simu
0766463129

No comments:
Post a Comment