![]() |
| Kaburi ambalo watu wawili mmoja akiwa hai walizikwa Chunya |
Na Albano
Midelo
MIKOA ya
Mwanza,Shinyanga na Tabora kwa miaka mingi imekuwa ni vinara kwa mauaji ya wakongwe kutokana na imani za
kishirikina.
Takwimu za mkoa
wa Tabora pekee zinaonyesha kuwa mwaka 2010 kutokana na imani za kishirikna
jumla ya watu 392 waliuwawa ambapo takwimu za mwaka 2011 zinaonesha kuwa watu
zaidi ya 370 waliuwa kutokana na imani za kishirikina kwenye mkoa huo.
Moto wa imani za kishirikina sasa unasambaa
kwa kasi hadi katika mikoa ya nyanda za juu kusini hususani mkoani Mbeya ambapo
wakazi wake wanadumisha imani za kishirikina na kusababisha vifo vya wazee
wasiokuwa na hatia.Uchunguzi
uliofanywa katika tarafa za Songwe na Kwimba wilayani Chunya na Kamsamba wilaya ya Mbozi mkoani Mbeya unaonyesha kuwa
imani za kishirikina katika maeneo hayo unashamiri na kuleta maafa makubwa yakiwemo kusababisha
vifo,ulemavu na uharibifu wa mali za watu kwa kuwa watuhumiwa uchawi wamekuwa
wanachomewa moto nyumba zao na mali zao hivyo kuongeza umaskini katika familia.
![]() |
| Kuchoma moto nyumba athari za imani za kishirikina |
Imebainika
kuwa baadhi ya vijiji kwenye tarafa hizo wazazi na walezi wameshindwa
kuwapeleka watoto wao kupata elimu ya msingi na sekondari kutokana kuwa na mwamko duni wa elimu hali
ambayo imechangia kwa kiasi kikubwa jamii ya watu kujiingiza katika imani za kishirikina.
Takwimu
za mwaka huu pekee zinaonyesha kuwa matukio ya mauaji ya kutisha yanaendelea
kutokea takribani kila mwezi yakitokana na imani za kishirikina zinazochangiwa
na idadi kubwa ya waganga wa kienyeji ambao wameweka makazi katika tarafa hizo.
Miongoni
mwa matukio mazito ya mauaji yanayotokana na imani za kishirikina ni lile
ambalo lilitokea mwezi Aprili mwaka huu Katekisita katika Kigango cha Kanisa Katoliki kitongoji
cha Maweni Kijiji cha Mkwajuni, Florian Mwachiluwi (70) alikufa baada ya
kuzikwa akiwa hai katika kaburi moja na mtu anayedaiwa kumuua kwa njia ya
kishirikina Peter Robert.
Marehemu
Mwachiluwi alikuwa akituhumiwa kwa uchawi kwa muda mrefu, hivyo alipofika
makaburini ndipo alipoombwa aingie kaburini baada ya kuingia kaburini akiwa na watu
wengine watatu wenzake walitoka kwa haraka na kumwacha Mwachiluwi peke yake
ndipo kundi la watu waliokuwa eneo hilo la makaburi walianza kumshambulia kwa
kumpiga mawe na fimbo hadi alizirai ndani ya kaburi.
Walianza
kumfukia na alipofukiwa nusu ya mwili wake waliingiza jeneza la marehemu Peter
Robert na kuliweka juu yake na kuanza kulifukia kaburi hilo kwa udongo na baadaye wakachukua jeneza la
marehemu na kuliweka juu yake, kisha kumfukia kwa udongo na kisha taratibu
za mazishi ziliendelea kwa ajili ya marehemu Peter.
Katika
tukio jingine kikongwe aliyefahamika kwa jina la Janeth Nenje(80), alinusurika kifo baada ya
kucharangwa na mapanga na mtu aliyefahamika kwa jina la Pato Lwiza Mkazi wa
Kitongoji cha Chang'ombe,Kijiji cha Mbuyuni Wilaya ya Chunya Mkoani Mbeya.
Inadaiwa
mtuhumiwa alimfuata kikongwe huyo nyumbani kwake na kuanza kumcharanga kwa
mapanga na kisha kumjeruhi vibaya hali iliyopelekea kukimbizwa katika Kituo cha
afya kilichopo kijijini hapo.Mtuhumiwa Lwiza alimtuhumu ajuza huyo kuwa ni
mshirikina hali iliyomfanya kuingiwa na hasira na kumtendea ukatili huo.
Katika tukio jingine Watu
watatu wakiwemo wanaume wawili na mwanamke mmoja walipigwa kwa mapanga na
kuchomwa moto hadi kufa katika kijiji cha Mbala wilayani Chunya.Msemaji wa
familia hizo tatu Mzee Crispin Katoto alidai kuwa mauaji hayo yanahusishwa na imani za kishirikina.
Mauaji ya kishirikina yanayofanana na ya kitongoji cha Maweni wilayani Chunya pia
mwaka huu yalitokea katika kijiji cha Kalungu kata ya Ivuna tarafa ya Kamsamba
wilayani Mbozi baada ya Kifo cha Mzee
Nongwa Hussein ambacho kinadaiwa kilitokana na uchawi, vijana wenye hasira kali
walihusishwa kwa kusababisha vifo vya watu wawili kati ya
watatu kuzikwa hai.
Walioshutumiwa
na kuhusika na kifo cha mzee Nongwa kwa imani za kishirikina ni pamoja na kaka
wa marehemu George Hussein, Ernest Molela na Bi. Miziana Nachela wote
wakazi wa kijiji hicho.
Wakati
mazishi yakiendelea vijana hao walianza kumtafuta kaka wa marehemu na
kufanikiwa kuwakamata Bwana Molela na Bi. Nachela na kisha kuanza
kuwaporomoshea kipigo na kuwazika hai katika kaburi moja na marehemu
Nongwa na hivyo kuzikwa watu watatu katika kaburi moja.
Baada
ya sakata hilo vijana hao waliondoka makaburini na taarifa kumfikia Afisa
Mtendaji wa Kata hiyo Joseph Silwimba, ambaye alifika eneo la tukio na kukuta
kitendo hicho cha kikatili kimekwisha tendeka na yeye kuchukua jukumu la
kulitaarifu Jeshi la Polisi ambao siku ya pili walilifika eneo la tukio na
kuifukua miili hiyo ya watu waliozikwa hai. Miili hiyo ilikabidhiwa kwa ndugu
ili kuzikwa upya katika makaburi mengine huku wakiuacha mwili wa marehemu
Nongwa katika kabuli la awali
Uchunguzi
uliofanywa katika baadhi ya vijiji vya tarafa hizo tatu umebaini kuwa wakazi wengi katika maeneo hayo
ni wa kabila la wanyamwanga na wafipa waliotokea wilayani Mbozi na Sumbawanga na kuhamia wilayani Chunya katika tarafa za
Songwe na Kwimba ambao kwa asili wanaendekeza imani za kishirikina.
Mwenyekiti wa kitongoji cha Maweni kijiji cha
Mkwajuni Felix Kayanda anabainisha kuwa wakazi wa kitongoji hicho wanaendekeza
imani za kishirikina ambapo katika kitongoji hicho kuna waganga wa jadi zaidi ya 15 ambao
wamekuwa wanafanyakazi ya kuagua na kufanya uchochezi wa kishirikina na kudai
kuwa hata tukio la kuuwawa kikatili katekista Mwachiluwi lilichochewa na mganga
mmoja wa jadi.
Uchunguzi umebaini kuwa matukio haya ya
mauaji ya kishirikina katika wilaya za Mbozi na
Chunya mkoani Mbeya yanahusiana moja
kwa moja kwa kuwa wakazi wake ni wa kabila moja la wanyamwanga ambao baadhi yao
wametoka wilaya ya Mbozi na kuhamia wilayani Chunya.
Kufuatia mauaji ya kishirikina
yanayoendelea kuibuka kwa kasi katika wilaya ya Chunya ,mkuu wa Wilaya ya hiyo Deodatusi Kinawiro amewataka Madiwani wa Halmashauri
hiyo kukemea maovu yanayosababisha na imani za kishirikina kwa kuwa yameanza
kuonyesha sura mbaya ya wilaya hiyo kwa watu wa ndani ya nchi na nje ya nchi.
“Kwa
ujumla hivi sasa wilaya imekuwa na viashirio vya mauaji mengi sana yanayohusishwa
na ushirikina wa ajabu, ambao unasababisha vifo katika wilaya mfano huyu mzee mstaafu wa
kanisa aliyeuwawa hivi karibuni kwa visa tu na kuanza kumtuhumu uchawi kwa
kuanza kumpiga mawe na kisha kumfukia akiwa hai katika kaburi moja na marehemu
“alisema Mkuu huyo wa Wilaya.
Hata
hivyo Kinawiro amewataka madiwani katika kata zote zilizoshamiri vitendo hivyo
kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kuwa wanatembelea katika kata zao na
kuongea na wananchi kuelimisha madhara ya kuamini ushirikina ambayo mpaka sasa
yamekuwa kero kubwa na hata kuwafanya wananchi waishi kwa hofu .
Alisisitiza kuwa kuanzia mwezi Julai
anatarajia kufanya ziara katika vijiji vyote vya wilaya yake hasa katika tarafa
za Kwimba na Songwe ambazo zimeshamiri kwa wakazi wake kuwa na imani za
kishirikina na hivyo kuhatarisha amani na utulivu kwa kusababisha vifo na
uharibifu wa mali.
Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya Diwani Athuman
hivi karibuni akihojiwa katika vyombo vya habari,alisema jeshi lake litaendelea
kufanya tathimini ili kutambua uharifu
wa aina zote unaofanyika katika mkoa wa Mbeya na kusisitiza kuwa wananchi
waache tabia ya kujichukulia sheria mkononi badala yake washirikiane na jeshi la
polisi kwa kutumia ulinzi shirikishi.
“Vijana wale ambao
mnauwa wakongwe wenye macho mekundu kwa madai kuwa ni washirikina,mtambue kuwa
nanyi siku moja mtazeeka na kuwa na macho mekundu,waharifu wasiuwawe bali
wanatakiwa kupelekwa kwenye vyombo vya sheria,wote wauaji tukiwakamata
tutawafungulia kesi ya mauaji’’,alisisitiza.
albano.midelo@gmail.com,simu
0766463129


No comments:
Post a Comment