![]() |
| Kaimu afisa elimu msingi wilayani Tunduru Flavian Nchimbi |
Na Albano Midelo
KILIMO cha kuhamahama
ndiyo chanzo kikuu cha utoro wa kudumu na rejereja kwa wanafunzi wa shule za
msingi na sekondari wilayani Tunduru mkoani Ruvuma.
Wakazi wa wilaya ya Tunduru
wengi wao ni kabila la wayao,ambao wanaendesha maisha kwa kutegemea zaidi Shughuli za kilimo, cha korosho,mihogo na
mpunga na sasa wamejikita zaidi katika kilimo cha kuhamahama cha zao
la Mpunga,hali hiyo imewafanya wananchi wa Tunduru kuwa nyuma katika maendeleo ya elimu.
Utafiti
ambao umefanyika katika baadhi ya shule za msingi na sekondari wilayani humo
kwa kuzungumza na wanafunzi,walimu, wazazi,walezi na wadau wa elimu kwa ujumla
wamekiri kuwa kilimo cha kuhamahama kinachangia tatizo la utoro kwa zaidi ya asilimia 90.
Hassan Musa mkuu wa
shule ya Frankweston anasema katika wilaya ya Tunduru wazazi wengi katika
kipindi cha kilimo kuanzia mwezi Desemba hadi Juni wanahama katika makazi yao
ya kudumu na kuhamia mashambani umbali wa kati ya kilometa 25 hadi 30 na kuacha
familia zao kwenye makazi yao kwa muda mrefu.
Hali hiyo kwa mujibu
wa mkuu huyo wa shule ndiyo chanzo cha utoro na mimba za utotoni kwa kuwa
watoto wao katika kipindi chote wanakuwa huru kutokana na kuishi bila wazazi
huku watoto wakubwa wakifanya kazi ya kuwalea watoto wenzao kwa kujiingiza
kwenye vitendo vya utoro shuleni na kufanya ngono zinazosababisha mimba
zisizotarajiwa.
“Watoto wanaachwa
wanajitegemea wenyewe,shuleni wanakwenda wanavyotaka,watoto wa kike
wanashawishika katika ngono ambazo sio salama hivyo kuwapa mwanya wa kujiingiza
kwenye mimba za utotoni na utoro wa kudumu,watoto wengi Tunduru wana watoto wao
kwa mfano mimi mwaka huu watoto 30 ni
watoro kati ya watoto 203 waliotakiwa kuanza kidato cha kwanza hata hivyo majina ya wazazi yao yamepelekwa mahakamani’’,alisema.
Kulingana na mkuu
huyo wa shule wazazi wengi katika wilaya ya Tunduru ni maskini kiasi kwamba
wanashindwa hata kulipa ada kwa wanafunzi wao wanaosoma sekondari za kata
ambayo ni shilingi 20,000 tu na kwamba hali inasababisha wanafunzi hao kuwa
watoro na wengine kujiingiza kwenye vitendo viovu.
Neema Mwakila na Edmund
Ndunguru ni walimu shule ya sekondari Frankweston wanasema malezi mabaya ya
kuwaacha watoto wajitunze wenyewe yamechangia utoro wa wanafunzi katika shule
nyingi na wengine kuamua kuolewa hali ambayo inachangia kushusha taaluma
wilayani Tunduru.
Ally Chilova mwalimu
wa sekondari ya Frankweston anasema umaskini ndiyo chanzo kikubwa cha
utoro na kwamba familia nyingi za
Tunduru ni maskini hali ambayo inawafanya wanafunzi kushiriki katika mapenzi
ili kujipatia kipato kwa familia yake na amesisitiza kuwa vijiji vingi vya Tunduru mtoto wake anakuwa
ni kitega uchumi cha kuhakikisha familia inapata pesa kwa kufanya mapenzi.
Umaskini uliopo
katika wilaya ya Tunduru kwa kiasi kikubwa unachangiwa na mwamko duni wa elimu
ambao ulikuwepo tangu zamani ambapo mapokeo ya elimu yalikuwa kidogo kiasi
kwamba mzazi alikuwa anamshauri mtoto wake wa kike kuhakikisha kuwa asifaulu
mtihani katika shule za msingi ili aendelee kuwa nyumbani kutumika kama kipato
cha familia.
Hata hivyo amesema
hivi sasa mwamko wa elimu katika wilaya hiyo angalau umeanza kutokana na
mwingiliano wa watu kutoka mikoa mingine pamoja na jitihada za serikali
kukabiliana na changamoto zinazodidimiza elimu katika wilaya hiyo.
Telispholi Ngonyani
mwalimu wa sekondari ya Frankweston anasema mimba kwa shule za msingi na
sekondari wilayani Tunduru zinachangiwa na mwamko duni wa elimu unaosababishwa na utoro wa kudumu unaozaa mimba za utotoni na kwamba
elimu inaingia taratibu kwa wakazi wa wilaya ya Tunduru ambapo waislamu ni
asilimia 90.
Olivia Mapunda
mwalimu mkuu shule ya msingi Umoja wilayani Tunduru anasema utoro katika shule
za msingi na sekondari unachangiwa na wazazi kuhamia mashambani na kuwaacha
watoto nyumbani kwao bila chakula hivyo watoto wengi wanakuwa tegemezi kwa
kubeba majukumu ya familia hivyo kupata vishawishi mbalimbali ikiwemo kupata
mimba.
“Shule nyingi za
msingi wilayani Tunduru,wanafunzi wanatoroka kuanzia saa nne wengine wanaondoka
moja kwa moja na wengine wanarudi kwa kuchelewa kutokana na kukosa chakula kwa
kuwa wazazi wao wanakuwa mashambani ambako ni mbali kwa wiki nzima na kuwaacha
watoto pekee yao hali ndiyo inachangia utoro wa kudumu au rejereja tatizo hilo
huanzia mwezi Januari hadi Mei kila mwaka’’,alisema.
Mapunda anasema wazazi na walezi wakipatiwa
mashamba yaliokuwa karibu tatizo la kuwaacha watoto kwa muda mrefu linaweza
kumalizika kwa kuwa wazazi watakuwa
jirani na familia yao au sheria iwekwe mzazi mmoja abakie kuwalea watoto badala
ya wazazi wote wawili kuhamia mbali kwa ajili ya kutafuta mashamba yenye
rutuba.
Kaimu afisa elimu wa
wilaya ya Tunduru Flavian Nchimbi
amesisitiza kuwa tatizo la wazazi kuhama katika makazi yao na kwenda
kutafuta mashamba mbali ya kuwaacha watoto bila kuwa na mlezi kwa muda mrefu
yamechangia utoro wa wanafunzi kwa asilimia 80.
Hata
hivyo hatua za kukabiliana na hali hiyo zinachukuliwa na serikali kwa
kuwaelimisha wazazi umuhimu wa elimu kwa
watoto wao na wazazi wengine ambao watoto wao ni watoro wa kudumu wanachukuliwa
hatua za kisheria kupitia serikali za vijiji,kata,tarafa na wilaya ili
kukomesha utoro kwa wanafunzi.
Kwa mujibu wa Takwimu za Wizara ya Elimu na
Mafunzo ya Ufundi, wasichana 8000 kila mwaka huacha shule kutokana na ujauzito
Kati yao 3,000 ni wanafunzi wa shule za msingi.
Kila
siku, wanawake 24 hufariki dunia kutokana na mimba au wakati wa kujifungua.
Wanawake watano mpaka sita wanaofariki kati ya hao ni watoto wadogo, watoto hao
hufariki dunia kwa kuwa miili yao haijakomaa vya kutosha kwa ajili ya
kujifungua
albano.Midelo@gmail.com,simu
0766463129

No comments:
Post a Comment