Saturday, June 22, 2013

Kijiji chabakiwa na wanawake na watoto pekee


Baadhi ya watoto katika kitongoji cha Maweni wakiwa hawana mlezi

  Na Albano Midelo
KITONGOJI cha Maweni katika kijiji cha Mkwajuni wilayani Chunya mkoani Mbeya kimebakiwa na wanawake pekee baada ya wanaume karibu wote kukimbia kwa takribani mwezi mmoja na nusu kuhofia kukamatwa na polisi kwa tuhuma za mauaji.
Katika hali isiyokuwa ya kawaida wanaume vijana zaidi ya 600 katika kitongoji hicho chenye  jumla ya watu 4500 wamekimbia na kuacha wake zao na watoto  wanaangaika kwa kukosa malezi bora kutoka kwa wazazi wote wawili na wengine wakiwa wamebakia yatima baada ya kufiwa na mama zao .
Kitongoji hicho kimebakiwa na wanawake,watoto na wazee wachache wanaume kufuatia operesheni inayoendelea kufanywa usiku na mchana na jeshi la polisi kuwatafuta vijana wanaotuhumiwa kumua kikatili katekista wa kigango cha Maweni Amosi Mwachiluwi(70).

Mkuu wa wilaya ya Chunya Deodatus Kinawiro
 Aprili 27 mwaka huu  Katekisita Mwachiluwi katika kitongoji hicho alikamatwa kupigwa na   kuzikwa akiwa hai katika kaburi moja na mtu anayedaiwa kumuua kwa njia ya kishirikina aliyefahamika kwa jina la Peter Robert.
 Inadaiwa baada ya kuingia kaburini akiwa na watu wengine watatu wenzake walitoka kwa haraka na kumwacha Mwachiluwi peke yake ndipo kundi la vijana waliokuwa eneo hilo la makaburi walianza kumshambulia kwa kumpiga mawe huku wakimwamuru akae chini kisha walianza kumfukia na alipofukiwa nusu ya mwili wake waliingiza jeneza la marehemu Peter Robert na kuliweka juu yake na kuanza kulifukia kaburi hilo hivyo kumsababishia kifo.
Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya Diwani Athuman
Uchunguzi ambao umefanywa katika kitongoji hicho umebaini kuwa baada ya vijana kukimbia kusikojulikana  nyumba karibu zote zimeachwa na kuongozwa na wanawake na nyumba nyingine watoto wanajiongoza wenyewe  hali ambayo inaongeza umaskini katika familia kutokana na ukweli kuwa baba ambaye ni kichwa cha familia hayupo hivyo watoto wengi wanashindwa kupata hata mlo mmoja katika familia.
Mwenyekiti wa serikali ya kitongoji hicho Felix Kayanda alisema  vijana karibu wote walipoamua kuondoka katika kitongoji hicho kuhofia kukamatwa na polisi,maisha yamekuwa magumu ambapo hivi sasa kila mara inapotokea tatizo la msiba katika kijiji hicho huwalazimu kwenda kuwakodi vijana kutoka kijiji cha Mkwajuni kwa kuwalipa kwa ajili ya kuchimba kaburi na shughuli za mazishi kwa ujumla.
“Leo hapa kijijini kuna msiba,hakuna kijana aliyerudi hapa,hivyo nimepita kukusanya michango kutoka kwa akinamama kwa ajili ya kwenda kukodi gari la kubeba msiba na kuwalipa vijana ambao watachimba kaburi,kwa kweli hali ni mbaya sana haijawahi kutokea hali kama hii mimi kama kiongozi nipo katika wakati mgumu sana’’,alisisitiza.
Matrida Jeremia mama wa watoto watano ambaye mume wake amekamatwa kwa tuhuma za kuhusika na mauaji alidai kuwa mumewe hausiki na mauji na kwamba siku ya msiba hakuwepo hata aliposikia anatumiwa kwa mauaji hakuweza kuamini.
Alisema anapata shida ya kuleta watoto wake watano ambao ameachiwa na mumewe ambaye yupo mahabusu na kusisitiza kuwa kuna watoto wameacha shule na wengine ni watoro kwa kuwa yeye pekee yake hawezi kumudu malezi ya watoto kwa kuwa hana kazi ya maana zaidi ya kilimo.
Joyce Mwanambilimbi mkazi wa kitongoji hicho alidai kuwa mumewe ambaye amemwachia watoto wanne ametoroka kuhofia kukamatwa na polisi hivyo amemuacha anapata shida ya kulea watoto kati yao ambao mmoja anasoma sekondari na wengine wapo shule za msingi.
Leya Mathias akihojiwa na mwandishi wa makala haya
“Baadhi ya wanawake wameamua kujiingiza katika ngono ili angalau kujipatia kipato cha kuendesha maisha na watoto wao,wengine wameolewa na wanaume wengine,naamini tatizo hili lisipopatiwa ufumbuzi kwa miezi sita ijayo ndoa zitavunjika na watoto wanakuwa katika mazingira magumu hivyo kuwaathiri katika maisha’’alisema Joyce
Leya Mathias mama wa watoto watatu mkazi wa Maweni akizungumza huku anatokwa na machozi,alidai kuwa mume ambaye amekamatwa na polisi kwa tuhuma za mauaji hausiki na mauaji hayo alikamatwa kwa kuonea na kusisitiza kuwa hata siku ya mazishi hakuwepo .
“Tangu mume wangu amekamatwa na kuniacha na watoto watatu maisha yamekuwa magumu,watoto wangu walikuwa wanafanya vizuri shuleni,walikamata nafasi ya kwanza hadi ya tatu lakini mtihani wa muhula wa mwezi huu wa sita wote wamekamata nafasi ya mwisho kwenye mitihani yao kwa kuwa walikuwa watoro,muda mwingi nilikuwa nakwenda nao shambani kwa kuwa sina msaidizi yeyote’’,alidai mama huyo.
Mwanamke huyo ameshauri kuwa njia pekee inayowezesha vijana hao kurudi katika kijiji hicho ni jeshi la polisi kuwaachia vijana waliokamatwa kwa tuhuma za mauaji na kuwakamata vijana waliohusika na tukio hilo ambao bado hawajakamatwa hadi sasa licha ya kufahamika kwa majina.
Mwenyekiti wa kijiji cha Mkwajuni Credo Kayanza alikiri kuwa watuhumiwa karibu wote waliokamatwa na polisi hawakuhusika na tukio hilo na kwamba serikali ya kijiji tayari imepata majina sahihi ya wote ambao walipanga na kuhusika moja kwa moja na tukio hilo la kinyama ambalo alifanyiwa katekista Mwachiluwi.
“Kuna vijana wamekamatwa na hivi sasa wapo mahabusu katika gereza la Ruanda Mbeya,hata hivyo wengi waliokamatwa sio walengwa wanatakiwa waondolewe,walengwa wenyewe bado wapo hapa kijijini wanafahamika na majina tunayo,hivyo mimi kama mwenyekiti wa kijiji nilikwenda kwa OCD kushughulikia tatizo hilo’’,alisema Kayanza.
Diwani wa kata ya Mkwajuni Chesco Ngairo alisema tukio hilo la mauaji limeharibu sifa ya kijiji cha Mkwajuni na kwamba kamati ya ulinzi na usalama katika kata imejipanga kuhakikisha kuwa watuhumiwa wote halali wa mauaji hayo wanakamatwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria.
Alisema kutokana na asilimia kubwa ya wanaume kukimbia katika kitongoji hicho yeye kwa kushirikiana na mwenyekiti wa kijiji waliitisha mkutano wa kuwataka vijana ambao hawakuhusika na kitendo cha mauaji warudi kijijini kwa kuwa sio vijana wote katika kitongoji cha Maweni walihusika katika mauaji hayo.
Hata hivyo Ngairo alisema hadi sasa hakuna kijana hata mmoja ambaye amerudi katika kitongoji hicho,hivyo kuleta athari kubwa katika jamii inayohusika ambapo amemuomba mkuu wa kituo cha polisi cha Mkwajuni kupunguza operesheni ya kukamata ovyo badala yake kuwatafuta walengwa ambao majina yao yapo .
Mwenyekiti wa kijiji cha Mkwajuni  Kayanza amekiri kukimbia kwa wanaume katika kitongoji hicho kumesababisha athari nyingi zikiwemo watoto kulelea na mzazi mmoja yaani mama na wengine kujiletea wenyewe kutokana na kukosa wazazi wote wawili na kwamba umaskini katika eneo hilo unaongezeka kwa kuwa nguvu kazi ambayo ni wanaume hawapo hali inayosababisha mwanamke kupata kazi ya kulea watoto pekee yake.
“Athari ni nyingi mno kwa mfano hivi sasa kila unapotokea msiba hawawezi kuzika hadi mimi nimehudhuria katika mazishi hayo,wananchi hivi sasa hawana imani na  usalama,ndoa nyingi zinaweza kuvunjika muda sio mrefu kwa sababu wanawake wanaweza kuolewa na wanaume wengine na hata waume zao huko walikokimbilia wanaweza kuoa na kuanzisha familia nyingine’’,alisema.
Mkuu wa wilaya ya Chunya Deodatus Kinawiro ametaka madiwani katika kata zote kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kuwa wanatembelea katika kata zao na kuongea na wananchi kuelimisha madhara ya kuamini ushirikina ambayo mpaka sasa yamekuwa kero kubwa na hata kuwafanya wananchi waishi kwa hofu .

“Kwa ujumla hivi sasa wilaya imekuwa na viashirio vya mauaji mengi sana yanayohusisha ushirikina wa ajabu ambao unasababisha vifo vingi  katika wilaya mfano huyu mzee mstaafu wa kanisa aliyeuwawa hivi karibuni kwa visa tu na kuanza kumtuhumu uchawi kwa kuanza kumpiga mawe na kisha kumzika akiwa hai kaburi moja na marehemu “alisema Mkuu huyo wa Wilaya.

Amewaasa wananchi kuacha tabia ya kujichukulia sheria mkononi ambapo athari zake wameziona katika tukio hilo ambapo vijana wamezihama nyumba zao na kuwaacha wake na watoto wao wanateseka kwa kukosa malezi ya wazazi wote wawili.

“Wananchi waache kucheza na dola kwa kufanya uharifu,hata hivyo kama kweli wana majina ambayo ni ya watuhumiwa halali ambao wameachwa watupe majina hayo ili kuwakamata watuhumiwa  wa mauaji wote halali,serikali haiwezi kukaa kimya inapowaona baadhi ya raia wanawauwa wenzao kwa imani za kishirikina ’’,alisisitiza.

 Kamanda wa polisi wa mkoa wa Mbeya Diwani Athumani alisema jeshi la polisi linaendelea na msako wa kuwatia mbaroni watuhumiwa  wote wa mauaji hivyo ametoa mwito kwa wananchi kutoa ushirikiano wa kuhakikisha watuhumiwa wote wanakamatwa na kufikishwa mahakamani.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129



No comments:

Post a Comment