Wednesday, July 3, 2013

Mwamko duni wa elimu Chunya chanzo cha umasikini



Walimu wadaiwa kuhongwa mifugo kutowaandikisha wanafunzi
Na Albano Midelo
Baadhi ya watoto waliokutwa wanadhurura Mkwajuni
 Utafiti uliofanywa katika baadhi ya shule za msingi na sekondari katika tarafa za kwimba na Songwe wilayani Chunya mkoani Mbeya umebaini kuwa mwamko wa elimu katika maeneo mengi ni duni.


Katika maeneo hayo wazazi na walezi hawana mwamko wa kuwapeleka watoto wao shule na hata wanafunzi wanaosoma wengi wanaacha shule kwa utoro,mimba na kuolewa kutokana na mila na desturi zinazoendelezwa na wakazi wa wilaya hiyo  wengi wao wakiwa ni wafugaji,wachimba madini,wavuvi na wakulima.

Katika kijiji cha Mkwajuni wanafunzi katika shule za msingi wapo wengi ambao ni watoro wa rejereja na wengine ni watoro wa kudumu,ambapo ukitembea katika maeneo unakutana na watoto wa darasa la kwanza hadi la tano ambao wanazurura bila kwenda shuleni.


Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Mkwajuni Kredo Kayanza alisema wakazi wa kijiji hicho ni wagumu hata kuchangia michango mbalimbali ya elimu katika shule za msingi na sekondari hali ambayo inawafanya watoto wao kusoma katika mazingira magumu.

“Kijiji hiki kina shule za msingi tatu ,nusu ya wanafunzi katika shule hizo wanakaa chini kutokana na upungufu madawati,shule ya msingi Mkwajuni ina wanafunzi 980, shule ya Maweni ina wanafunzi zaidi ya 700 na shule ya msingi Osterbay ambayo haijafikia bado darasa la saba ina wanafunzi zaidi ya 400,shule zote zinakabiliwa na upungufu mkubwa wa vyumba vya kusomea  hivyo kuna mlundikano mkubwa wa wanafunzi katika chumba kimoja wanaofikia hadi 80’’,alisema.

Mkuu wa wilaya ya Chunya Deodatus Kinawiro
Baadhi ya wazazi walipohojiwa kwanini wanashindwa kuchangia michango mbalimbali ya elimu ,walidai kuwa ni kutokana na shule za msingi na sekondari kutoza michango mingi ambayo watanzania wengi masikini ambao hawana uhakika wa kula hata mlo mmoja wanashindwa kumudu hivyo watoto wao wanafukuzwa na kuwa watoro.

Leya Mathias mkazi wa kitongoji cha Maweni Mkwajuni aliitaja sababu kubwa ambayo inachangia utoro kwa wanafunzi katika kijiji cha Mkwajuni ni wazazi na walezi kushindwa kulipia michango mingi hivyo kuamua watoto wao kubakia nyumbani na kufanyakazi za shambani,uvuvi na uchimbaji madini.

“ Watoto wengi katika shule za msingi na sekondari hapa Mkwajuni wameacha shule kwa kuwa mzazi mmoja anashindwa kulipia michango mingi ya fedha za madawati,mlinzi,tofali mimi pekee yangu mwanamke nitatoa pesa zote hizo kutoka wapi,ndiyo maana watoto wanabakia kuwa watoro ’’,alisema.

Hata hivyo mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Mkwajuni Kayanza alikanusha madai hayo kuwa sio sahihi kwa kuwa michango yote inayotozwa imepitishwa na kukubaliwa na wananchi wenyewe kwenye vikao na kwamba sababu kubwa ni mwamko duni wa elimu walionao wazazi na walezi wengi katika wilaya ya Chunya.

Wafugaji wahamiaji kwenye bonde la Songwe wilayani Chunya  wanadaiwa wamewekeza zaidi kwenye mifugo kuliko elimu hali ambayo imesababisha watoto wao waliostahili kuanza shule ya msingi kuendelea na kazi za  uchungaji wa mifugo badala ya kusoma.

 Wafugaji hao wahamiaji wanaishi katika vijiji vya kata za   Galula, Mbuyuni na Totowe  ambapo  takwimu za mifugo katika Halmashauri ya wilaya ya Chunya zinaonesha kuwa wafugaji hao hadi kufikia Desemba 2010 walikuwa na  mifugo ya aina mbalimbali zaidi ya 800,000 wakiwemo ng’ombe,mbuzi,kondoo na punda.

Uchunguzi unaonesha kuwa familia za wafugaji wamewaachisha masomo watoto wao kwa lengo la kuchunga mifugo na hata wale ambao wanaendelea na masomo wanasoma kwa kufanya utoro wa mara kwa mara .Hali hiyo ndiyo iliyosababisha asilimia 90 ya wafugaji hao wahamiaji ambao walifika kwenye bonde hilo miaka ya 1980 kutojua kusoma,kuandika na kuhesabu.

Imebainika baadhi ya maeneo katika bonde wafugaji wanawahonga mifugo baadhi ya walimu wakuu ili wawafute shule watoto wao na kuendelea kuchunga mifugo yao wakati wote,hali hiyo ndiyo moja ya sababu za wilaya hiyo kuwa nyuma katika elimu na kukabiliwa na umaskini wa kifkra na kiuchumi.

John Bedas mkazi wa kijiji cha Galula anadai kuwa umaskini wa kipato kwa wananchi wa Wilaya ya Chunya umesababisha wazazi na walezi kuwaficha watoto wao msituni wakati wa zoezi la kuandikishwa shule za msingi na baada ya kupita zoezi hilo huwapeleka kuvua samaki ,kuchimba dhahabu,kuchunga mifugo  pamoja na kilimo.

Imeelezwa kuwa kutokana na hali wilaya ya chunya imekuwa na watoto wengi ambao hawasomi kutokana na kujishughulisha na kazi hizo na  hivyo kusababisha wilaya hiyo kuwa nyuma katika elimu.

 Ofisa Elimu shule za Msingi Wilayani chunya Ally Mbawala alisema kuwa watoto walio wengi wa shule za msingi hawasomi na hata wazazi wa watoto hao wamekuwa hawana mwamko wa elimu,hivyo watoto wao wamekuwa wakiacha shule kabisa na kukimbilia kuvua samaki na kutafuta dhahabu na kuchunga mifugo .



“Tatizo hili kama wilaya linatuumiza  vichwa uongozi wa wilaya unafanya jitihada kwa kushirikisha wazazi na walezi ili kuweza kulimaliza tatizo hilo la utoro kwa wanafunzi wa shule za msingi ambalo kwa kiasi kikubwa limeweza kuathiri kiwango cha elimu kwa watoto hao’’,alisisitiza.



Uchunguzi pia umebaini kuwa zaidi ya wanafunzi 500 waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza katika Shule mbali mbali za Sekondari Wilayani Chunya msimu huu wameshindwa kuripoti Mashuleni kutokana na sababu mbali mbali ikiwemo kujiingiza katika biashara za uchimbaji wa Madini,kuchunga mifugo na Uvuvi.



Kutokana na hali hiyo Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Deodatus Kinawiro, amewataka Wazazi wa Wanafunzi hao kuhakikisha wanawapeleka watoto wao Shuleni haraka kabla ya kuchukuliwa kwa hatua za kisheria kwa mzazi atakayekaidi agizo hilo.



Taarifa kutoka kwa Afisa elimu wa Wilaya hiyo inaonyesha  kukithiri kwa utoro wa wanafunzi mashuleni,na kuifanya Serikali kushindwa kufikia malengo yake ya kufuta ujinga miongoni mwa wananchi.



Kinawiro alibainisha kuwa Wilaya ya Chunya inakabiliwa na Wimbi kubwa la wafugaji wenye tabia ya kuhamahama jambo ambalo husababisha kuwakatisha masomo wanafunzi ili hali wengine wakijikita kwenye shughuli za uchimbaji wa madini na uvuvi katika Ziwa Rukwa.



Alisema operesheni ya kuwasaka wazazi na walezi wanaoshindwa kuwapeleka watoto wao shule itakuwa ni ya kudumu na kusisitiza kuwa mzazi yeyote ambaye hatampeleka Mwanaye Shule bila kujali kisingizio cha aina yoyote atakamatwa na kufikishwa mahakamani kujibu mashtaka ya kumwachisha masomo mwanafunzi na kumpatia ajira kinyume cha Sheria.



Mkuu huyo wa Wilaya alisema Idadi ya watoto 500 ni kubwa sana hivyo hali hiyo ikiachwa itazalisha Wajinga wengi jambo ambalo litakuwa mzigo kwa taifa na kwamba vijana wengine wanaweza katika uhalifu baada ya kukosa fedha kutokana na ajira walizojiingiza katika umri mdogo.

Hata hivyo Kinawiro alisema  Wilaya ya Chunya kitaaluma inafanya Vizuri katika ngazi ya Mkoa ukilinganisha na Wilaya zingine za mkoa wa Mbeya na kwamba hayupo tayari kuona sifa hiyo inapotea kutokana na wazazi wachache kuzembea na kutokujua umuhimu wa kumsomesha mtoto, na kuongeza kuwa Halmashauri inaunga mkono juhudi za Serikali kwa kuimarisha ujenzi wa Mabweni ili kuhakikisha watoto wa kike hawakatizwi masomo kutokana na mimba zisizotarajiwa.

 Kwa mujibu wa Takwimu za Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, wasichana 8000 kila mwaka huacha shule kutokana na ujauzito. Kati yao 3,000 ni wanafunzi wa shule za msingi.











No comments:

Post a Comment