Ni kutokana na unyanyasaji wa polisi
Na Albano
Midelo
WAKAZI wa Bonde la
Songwe wilayani Chunya mkoani Mbeya wametoa mwito kwa mkuu wa wilaya na mbunge
wa jimbo hilo kusaidia kupambana na askari polisi ambao wamekuwa wanadaiwa kuyanyanyasa
makampuni ya mabasi yanayotoa huduma za usafiri wa abiria.
![]() |
| Mbunge wa jimbo la Songwe Philipo Mulugo |
Askari polisi wanaopangwa barabara ya Mbalizi wilayani Mbeya na wa kituo kidogo cha Galula
wilayani Chunya wamekuwa wanadaiwa kuomba rushwa waziwazi kwa makampuni ya
usafirishaji wa abiria katika barabara ya
Mbalizi,Galula hadi Mbuyuni na Mbalizi hadi Mkwajuni hali ambayo imekuwa kero
kubwa kwa wafanyakazi wa makampuni ya usafirishaji wa abiria katika barabara
hizo.
Makampuni ya mabasi
ya abiria ambayo yanakumbwa na kero ya askari kuwaomba pesa tena bila
kuandikiwa risiti ni pamoja na BOY SASA
EXPRESS,G.M SAFARIS na Kampuni ya KANYEGELE ambapo imekuwa ni jambo la kawaida
kwa wafanyakazi wa mabasi hayo kutenga fedha kwa ajili ya askari wa barabarani
kila siku.
![]() |
| Mkuu wa wilaya ya Chunya Deodatus Kinawiro |
Wafanyakazi wa
kampuni ya mabasi ya abiria ya GM Safaris ambayo inasafirisha abiria kila siku
kutoka Mbalizi hadi Mbuyuni wilayani Chunya wametishia kusitisha safari katika
barabara hiyo kutokana na kero kubwa inayofanywa na polisi kudai rushwa ambapo
kila siku wanatumia kati ya shilingi
50,000 hadi 100,000 kuwapa askari polisi
wanakuwa katika barabara hiyo.
Uchunguzi umebaini
kuwa makampuni mengine ya mabasi ya abiria kwa miaka ya nyuma katika barabara hiyo
yaliamua kusitisha kutoa huduma kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ya askari
polisi kudaiwa kuwatoza pesa nyingi za rushwa bila kuandikiwa risiti hivyo
mabasi kufanya biashara ya usafiri kwa hasara kubwa hali iliyosababisha
kusimamisha huduma na wananchi kuendelea kuteseka kwa miaka mingi kusafiri kwa
kutumia magari ya mizigo.
Wafanyakazi wa Kampuni
hiyo ambayo imeanza kusafirisha abiria katika barabara hiyo kwa takribani wiki
mbili sasa,wamedai kuwa hawawezi kuendelea kutoa huduma katika barabara hiyo
kutokana na askari polisi kila siku wanadai kiwango kikubwa cha pesa tena bila
kosa na kwamba fedha hizo wanachukua bila kuandikiwa risiti yeyote.
Mwandishi wa habari
hizi ambaye siku ya Juni saba mwaka huu alipanda basi la kampuni hiyo lenye
namba za usajiri T.793 BNF akiwa amekaa kiti cha kwanza alishuhudia askari
polisi wakimtaka kondakta wa basi hilo kuwapa kiwango cha pesa walichapanga wao
wenyewe tena bila kuandikiwa risiti wala kuambiwa pesa hiyo wanatoa kwa kosa
gani.
Hali hiyo imewafanya
wafanyakazi wa basi hilo kudai kuwa wakati wowote wanatarajia kuacha kutoa
huduma ya usafiri wa abiria katika barabara hiyo ambayo kabla ya kampuni hiyo
wananchi walikuwa wanasafiri kwa kutumia magari ya mizigo hivyo kuwa kero kubwa
kwa wananchi na kuhatarisha maisha yao.
John Tarimo
mfanyakazi wa basi hilo alisema kabla ya kuanza safari katika barabara
hiyo,walikuwa wanatoa huduma kutoka mjini Njombe hadi Ludewa na kwamba askari
polisi wa huko hawakuwa wanadai rushwa kubwa kama ilivyo kwa polisi na Mbeya
ambao wanadai rushwa bila aibu wala kuogopa.
“Haiwezekani sisi
tuendelee kutoa pesa ambayo haina jasho kwa askari ambao wanalipwa mishahara
kila mwezi,pesa yote tunamaliza kuwapa askari,wafanyakazi tutawalipa nini, matengenezo
ya gari tutafanyia nini kwa kweli polisi wa barabara hii ni kero kubwa sana
hali ikiendelea hivi kwa wiki moja
tutasimamisha kutoa huduma ya usafiri wa abiria,wananchi waendelee
kutumia magari ya mizigo’’,alisisitiza Tarimo.
“Kero kubwa
inayotukabili kila siku barabarani ni pale tunapokutana na trafiki ambao mbaya
zaidi wanaomba pesa kwa kujipangia kiwango anachotaka mwenyewe,sasa nauli kiasi
gani utawatoza wananchi ili kutimiza mgawo kwa askari hao,gari linadai
matengenezo,mafuta,matairi na kuwalipa wafanyakazi mishahara, tangu asubuhi tunajinyima
lakini wenzetu wanachukua pesa kiulaini,tulitaka kuleta basi la pili lakini
sasa tunaona hii biashara itatushinda’’,alisisitiza Tarimo.
Dreva wa basi hilo
ambaye hakutaka jina lake kuandikwa gazetini alidai kuwa askari hao
wanabadilisha zamu za kuwa barabarani ambapo asubuhi anapotoka Mbuyuni kwenda
Mbalizi anawapa fedha askari wengine na
mchana anaporudi anatoa rushwa kwa askari wengine na kwamba hata kama gari
limebeba abiria ambao wote wamekaa kwenye viti askari hao wanadai kupewa pesa.
Baadhi ya abiria
waliokuwa wanasafiri katika basi hilo wamewalaani askari polisi hao kutokana na
kitendo cha kudai rushwa pesa nyingi hadharani kutoka kwa kampuni hiyo na
kwamba wametoa mwito kwa kamanda wa polisi wa mkoa wa Mbeya kuwawajibisha
askari hao ambao hawastahili kuwa askari.
“Kila mmoja katika
basi ameshuhudia namna askari hawa wanavyosimamisha basi hili kuanzia askari wa
kituo kidogo cha polisi cha Galula wilayani Chunya hadi askari polisi
waliokuwepo kuanzia eneo la Mshewe hadi
Mbalizi wilayani Mbeya ,hatuwezi kukubali basi hili lisimamishe huduma kwa
sababu ya tamaa ya kujipatia fedha haramu,ni lazima tutawachongea kwa wakubwa
wao’’,alisema John Shitindi mkazi wa Galula.
Joyce Malimali mkazi
wa Chang’ombe amemuomba mbunge wa jimbo Songwe Philipo Mlugo ambaye pia ni
Naibu waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi kuwasaidia ili askari hao waweze
kuwajibishwa kwa kuwa warudisha maendeleo nyuma kutokana na vitendo vyao vya
kudai rushwa vinavyowakatisha tamaa wawekezaji katika jimbo la Songwe.
| Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya Diwani Athuman |
“Sisi wanawake na
watoto ndiyo ambao tutapata shida kubwa endapo kweli kampuni hii itasitisha
kutoa huduma za usafiri wa abiria kwa kuwa hatuwezi kupanda kwenye magari ya
mizigo ambayo yanakuwa yamewekwa mizigo mingi kama vile mifugo na magunia
kuchanganywa na watu ni hatari kwa usalama’’,alisema Joyce.
Mkuu wa wilaya ya
Chunya Deodatusi Kinawiro ambaye pia ni
mwenyekiti wa ulinzi na usalama wa wilaya hiyo ameahidi kuhakikisha kuwa tatizo
hilo linatafutiwa ufumbuzi wa kudumu na kwamba kwa kuanzia atawasiliana na
kamanda wa polisi wa mkoa wa Mbeya Diwani Athumani kuwachukulia hatua vijana
wake ambao wanakiuka maadili ya jeshi la polisi.
“Haiwezekani polisi
kudai kupewa pesa bila kutoa risiti za kuonyesha wanatoa pesa kwa kosa gani na
shilingi ngapi,natambua changamoto za usafiri wa mabasi ya abiria katika bonde
la Songwe kampuni hiyo ya G.M Safari naitambua nawaomba wasikate tamaa
waendelee kutoa huduma hiyo muhimu,kama kuna tatizo tuwasiliane,serikali
tutachukua hatua dhidi ya askari wanaokwenda kinyume cha sheria’’,alisisitiza.
Katika hatua nyingine
baadhi ya madereva wa bodaboda katika vijiji vya
Galula,Ifuko,Magamba,Chang’ombe na Kanga wilayani Chunya wameelezea adha
wanayopata kutoka askari polisi wa kituo kidogo cha polisi cha Galula kuwadai
pesa kati ya shilingi 30,000 hadi 100,000 ambayo huwapatia askari hao tena bila
kuandikiwa risiti kwa madai kuwa pikipiki zao zina makosa ya barabarani.
Vijana hao ambao
hawakutaka majina yao kuwekwa mtandaoni ,walidai kuwa imekuwa ni jambo la
kawaida kwa askari hao kushika pikipiki zao kila siku na kwamba askari hao
wamefanya huo kuwa ni mradi wao kwa kuwa wanakusanya pesa nyingi ambazo
zinaishia kwenye matumbo yao kwa kuwa wanalipa bila kuandikiwa popote na kwamba
ukiuliza risiti unaishia kupigwa na pikipiki yako kushikiliwa .
Vitendo vya polisi kudai rushwa
vimekuwa vinadaiwa kufanyika karibu kila kona za nchi,hata hivyo ushahidi wa
kukiuka maadili ya jeshi la polisi kwa kudai rushwa unaweza kumfukuza kazi
polisi,isipokuwa inakuwa ni vigumu kumpeleka mahakamani bila ya ushahidi hali
hiyo ndiyo inachangia vitendo vya kudai
rushwa kwa polisi kuendelea.
Hivi karibuni Mkurugenzi Mkuu wa
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Dk Edward Hoseah, Akitoa
majumuisho katika Mkutano Mkuu wa Chama cha Wabunge Wanaopambana na Rushwa
nchini (APNAC),akataka itungwe sheria kali ya kutaka kiongozi au mtumishi wa
umma awajibike mara anapokuwa ametuhumiwa kwa jambo lolote aachie ngazi na
kupisha uchunguzi kama ilivyo kwa nchi zingine.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129


No comments:
Post a Comment