Saturday, October 26, 2013

Askofu ashauri kuhusu miito


Na Albano Midelo
Askofu wa jimbo la Tunduru-Masasi Castory Msemwa

ASKOFU wa jimbo la Tunduru-Masasi mhashamu Castory Msemwa ametoa rai kwa waumini wa kanisa katoliki  nchini kuomba kwa ajili ya miito mitakatifu kutokana na idadi ya wanaojiunga kuendelea kupungua kwa kasi.
Mhashamu Msemwa alitoa rai hiyo wakati anahubiri katika adhimisho la misa ya shukrani ya jubilei ya miaka 25 ya upadre,miaka tisa ya uaskofu na miaka 58 ya kuzaliwa iliyofanyika katika kigango cha Mtulila parokia ya Matola jimboni Njombe .
Akionyesha namna tatizo la miito mitakatifu linavyoendelea kukua,mhashamu Msemwa anasema wakati anatimiza miaka 25 ya upadre katika kigango chake cha Mtulila na parokia nzima ya Matola  hakuna hata mseminari mmoja ambaye yupo seminari kuu  hivyo  inahitajika kuendelea kuungana  kuomba kwa ajili ya miito.

“Siamini kama kweli hakuna vijana wanaoweza kujiunga na mito mitakatifu katika ngazi ya kigango na parokia,tunahitaji sala katika familia zetu,kama hatufanyi hivyo tuelewe wazi kuwa tunamkosea mwenyezi Mungu,kila mmoja wetu amesalimiwa na Mungu lakini hatutaki kuongea na Mungu,maana yake hatutaki kusali katika familia zetu,hatutapata mapadre wala watawa’’,alisisitiza.
Amewatahadharisha waumini katika parokia ya Matola yenye waumini zaidi ya 11,000  kutosahau alama zinazowafanya kuwa wakristo zikiwemo kushindwa kutoa hadithi za Mungu na kutosali ndani ya familia hali ambayo imesababisha watoto kutojua hata ishara ya msalaba hadi wanapopata mafundisho katika shule za msingi hali inayosababisha miito kuwa migumu.
Kwa mujibu wa Askofu Msemwa,wakati anapewa daraja takatifu mwaka 1987 katika kigango cha Kitulila pekee kulikuwa na watawa wa kike na wa kiume 27 na kwamba watawa waliongezeka toka mwaka huo hadi sasa hawazidi watawa 10 licha ya takwimu kuonyesha kuwa kuwa katika familia kuna ongezeko kubwa la vijana.
Akizungumzia sababu za waumini wa kanisa katoliki kuhamia madhehebu mengine yakiwemo ya kilokole,mhashamu Msemwa aliitaja sababu kubwa inayochangia kuongezeka kwa tatizo hilo kuwa ni wazazi na walezi katika familia wameanza kuzembea kusali kuacha kulea familia zao katika misingi ya kanisa katoliki hivyo vijana kuamua kufuata yale wanayoyaona yanapendeza katika masikio yao na kuamua kuokoka.
Ameshauri wazazi na walezi kuhakikisha kuwa mizizi ya imani ya kanisa inaingia sawasawa kwa watoto wao ili waweze kuimarishwa zaidi katika imani kwa kuwa ni vigumu kuingia mbinguni bila kuwa na imani iliyokomaa ambayo inanzia katika ngazi ya familia na kwamba wazazi na walezi waache kuwategemea makatekista kuimarisha imani.
 Xavery Mlelwa paroko wa parokia ya Madunda ambaye apewahi pia kuwa paroko katika kigango cha Mtulila anasema sehemu kubwa ya jimbo la Njombe ikiwemo parokia ya Matola yenye waumini zaidi ya 11,000 asilimia kubwa ya watu ni wakristo hivyo ameshauri kwa lengo la kufufua imani ni vema kuanzia ngazi ya familia.
“Ni kweli sisi tumelegea katika imani kwa kuwa hatuna changamoto nyingine kama maeneo mengine ambayo yana waumini wa kiislamu,kumbe ukiishi na mtu ambaye mmetofautiana kifikra au imani unaweza kujiimarisha zaidi hivyo kwa kuwa tupo watu wa aina moja tumejisahau na kushindwa kuilinda imani’’,alisema padre Mlelwa.
Baadhi ya waumini na wanafamilia wa mhashamu Askofu Msemwa wametoa maoni tofauti kuhusu jubilei ya miaka 25 ya upadre na miaka tisa ya uaskofu ambapo dada yake askofu Msemwa  ambaye ni mtawa wa shirika la Vinsent Sr.Lucia Msemwa alisema kaka yake alionekana mapema kuwa anaweza kuwa mchungaji wa watu.
“Kaka yangu Askofu Msemwa ambaye ni mtoto wa nne kati ya watoto kumi katika familia yetu,alikuwa anamsaidia baba kuchunga mifugo mbalimbali  tangu akiwa shule ya msingi na aliendelea kuchunga hadi alipofikia seminari kuu akirudi likizo alipenda kumsaidia baba kuchunga nadhani alikuwa anaandaliwa kuwa mchungaji wa watu’’,alisema Sr.Lucia Msemwa dada yake Askofu.
Uchunguzi umebaini kuwa familia ya Askofu Msemwa tangu awali imejengwa katika imani iliyokomaa,kutokana na ukweli kuwa kuanzia baba yake mzazi Askofu Msemwa  anayeitwa Paulonus Msemwa(93) bado yupo hai alizaliwa mwaka 1920 katika maisha yake alikuwa mwalimu wa dini (katekista) hivyo kuwalea watoto wake katika misingi ya imani.
Hali hiyo ilimfanya mtoto wa kwanza wa mzee Msemwa aliyezaliwa mwaka 1950 anayeitwa Menas Msemwa  kufanyakazi ya ukatekista ,pia dada yake Askofu Msemwa anayeitwa Sr.Lucia Msemwa ni mtawa wa shirika la Vincent lakini kubwa zaidi  familia hiyo kubahatika kutoa Askofu Desemba 7 mwaka 2004 baada ya Askofu Castory Msemwa kuteuliwa na Baba mtakatifu kuwa Askofu wa jimbo la Tunduru-Msasi.
“Katika familia yetu tulipata malezi bora baba yetu mzazi alikuwa ni mwalimu wa dini, mdogo wangu ni  Askofu  Msemwa,mimi mwenyewe nilikuwa  katekista hadi nilipostaafu,dada yangu alikuwa kiongozi wa kanisa katika parokia ya Matola,dada yangu mwingine ni sista katika shirika la Vincent hadi sasa’’,alisema Menasi Msemwa kaka yake Askofu Castory Msemwa.
Hata hivyo kaka huyo wa Askofu aliitaja siri kubwa iliyosababisha Askofu Msemwa kupanda kwa haraka kutoka daraja takatifu la upadre hadi kuteuliwa kuwa Askofu ni sala na maombi  na kwamba wazazi wao tangu wakiwa wadogo waliwawekea msingi wa kusali sala mbalimbali ikiwemo lozari kabla na baada ya kulala.
Baba mzazi wa Askofu Msemwa mzee Paulunus Msemwa anasema amefurahia sana jubilei ya miaka 25 ya upadre wa mtoto wake, na kwamba watoto wake aliwajenga katika misingi ya kiimani,hata hivyo alidai kilichomfurahisha zaidi ni kuhojiwa,kupigwa picha na mwandishi wa habari kwa kuwa katika maisha yake yote ya umri wa miaka 93 hajawahi kuandikwa katika chombo chochote cha habari.
“Sijawahi mimi kuandikwa na chombo cha habari,kwa mara ya kwanza ni leo tu,naona sasa wameona umuhimu wa familia hii kuandikwa na kuingia kwenye historia ili wengine watakaosoma au kusikia kuhusu familia hii waweze kujifunza hasa mambo ya  imani na kusali kuanzia ngazi ya familia’’,alisisitiza mzee Msemwa.
Askofu Castory Msemwa alizaliwa Februari 13,1955 katika kigango cha Kitulila parokia ya Matola jimbo la Njombe kwa wazazi Paulunus Msemwa na Yulina,alibatizwa Uwemba mwaka 1955,elimu ya msingi kuanzia mwaka 1968 hadi 1973 shule ya msingi Matola,kidato cha nne sekondari ya Mafinga kati ya mwaka 1974 hadi 1977,alijiunga seminari ndogo ya Likonde kidato cha tano na sita kati ya mwaka 1978 na 1980.
Mhashamu Msemwa mara baada ya kujiunga na mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa JKT ,alijiunga na seminari kuu Peramiho mwaka 1981,alipata daraja takatifu la upadre mwaka 1987 na kuteuliwa na Baba mtakatifu kuwa Askofu wa jimbo la Tunduru-Masasi mwaka 2004.
Mhashamu  Msemwa ambaye alifanya jubilei ya miaka 25 ya upadre mwaka jana, amehitimisha adhimisho la misa ya shukrani ya Jubilei ya miaka 25 ya upadre wake mwaka huu katika kigango cha Kitulila parokia ya Matola jimbo la Njombe ambako ni nyumbani kwake alikopatia daraja takatifu la upadre.
Mhashamu Msemwa kuanzia Oktba 9 hadi 20 alifanya ziara katika parokia saba kati ya 45 za jimbo la Njombe kwa lengo la kufanya misa za shukrani kwa ajili ya Jubilei ya miaka 25 ya upadre wake .
Katika ziara hiyo ya misa ya shukrani ya jubilei ya miaka 25 ya upadre mhashamu Msemwa ametoa sakramenti ya kipaimara kwa watoto 1258 kutoka parokia saba za jimbo la Njombe.
Kati ya watoto hao parokia ya makete watoto 146,Ikonda watoto 115,Matola 275,Madunda 334,Kifanya 270,kigango cha Boimanda watoto 62 na kigango cha Kitulila ambacho amezaliwa askofu Msemwa ametoa sakramenti ya kipaimara kwa watoto 56,amefungisha ndoa jozi tano na kutoa ubatizo kwa watoto kadhaa.
albano.midelo@gmail.com

No comments:

Post a Comment