![]() |
| Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Thabit Mwambungu |
Na Albano Midelo
“TANESCO wanakata na kurudisha umeme bila
taarifa na hata ratiba ya mgao haijulikani hali inasababisha hasara kubwa kwa
wananchi ikiwemo kuungua vifaa vya umeme na vyakula vinavyohifadhiwa kwenye
majokofu kuharibika’’,anasema diwani wa kata ya mjini manispaa ya Songea Joseph
Fuime.
Fuime alidai kuwa tatizo la umeme Songea
haliwezi kupatiwa ufumbuzi wa kudumu kwa kuendelea kutumia mashine chakavu za kufua umeme ambazo vipuri
vyake vinaharibika mara kwa mara badala yake alishauri serikali kuunganisha
mkoa wa Ruvuma na umeme wa giridi ya Taifa.
“Serikali iliahidi mara baada ya kuanza
kuchimbwa makaa ya mawe ya Ngaka wilayani Mbinga kutajengwa kinu cha kufua
umeme katika mji wa Songea hata hivyo tangu mwekezaji ameanza kuchimba makaa ya
mawe hadi sasa hakuna dalili za kufungwa kinu hicho pia mwekezaji ameshindwa
hata kuwalipa fidia wananchi wanaoishi
katika eneo la mgodi’’,alidai Fuime ambaye pia ni katibu wa CHADEMA mkoa wa
Ruvuma.
Uchunguzi uliofanywa katika maeneo mengi ya mji wa Songea umebaini kuwa vibaka wakati
wa usiku wameongezeka na kusababisha nyumba nyingi kukatwa nyanya za
madirishani na wengine kuibiwa vitu mbalimbali zikiwemo simu za mikononi,mavazi,kompyuta
za mkononi na samani mbalimbali.
Waandishi wanakwama kutuma habari zao kwa
haraka na hata vituo vya matangazo vilivyopo mjini Songea vikiwemo Redio
Maria,radio Jogoo,TBC Taifa, vinashindwa kurusha matangazo kwa wananchi
kutokana na kukatika kwa umeme mara kwa mara.
John Mapunda mfanyabiashara soko kuu la Songea
anasema Kukatika kwa umeme na kuwaka bila taarifa katika mji wa Songea kunawasababishia
hasara kubwa wafanya biashara wa vyakula hasa wanaouza samaki wabichi kutoka
ziwa Viktoria, Tanganyika, Nyasa na bwawa la Mtera ,wao wanatunza samaki hao
katika makojofu ambayo yanatumia umeme wa TANESCO hivyo samaki wengi wanaoza.
“TANESCO
katika manispaa ya Songea inaonyesha
dhahiri kuwa mashine zao haziwezi kufua umeme wa kukidhi hata katika mji wa
Songea,wananchi tunahoji kwanini umeme huo umesambazwa hadi mji mdogo wa
Peramiho badala ya kusubiri umeme gridi
ya Taifa’’,alihoji Mapunda. Frank Mbunda
mkazi wa Mahenge mjini Songea anadai kuwa TANESCO wameshindwa kumaliza tatizo
sugu la umeme ambalo linachangia
umasikini kwa wakazi wa Songea ambao wanashindwa kufanyakazi zao za kiuchumi.
Mwanaharakati
Mohamed Kudeka mkazi wa Songea anatoa wito kwa serikali kuachana na umeme wa
majenereta ambao matatizo yake ya kuharibika kwa vipuri yamekuwa
yanajirudiarudia na kusababisha kero kubwa kwa wakazi wa mji wa Songea ambao
wanashindwa kufanya kazi za kiuchumi na kusababisha umaskini.
“Mchawi ni
ugonjwa wa majenereta ambayo vipuli vyake vimechoka na kuchakaa,tumechoka na
kero hii kama sio ubovu wa vipuri
utasikia mafuta ya kuendeshea mitambo yamekwisha,mara fundi wa kufunga
vipuri anatoka nje ya nchi TANESCO tuambieni ukweli tumechoka’,anasisitiza.
Brighton Mwandata
mmiliki wa studio ya kurekodi muziki Matarawe mjini Songea anasema umeme katika
mji wa Songea haujapatiwa ufumbuzi wa kudumu anashindwa kurekodi kutokana na
tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara wakati mwingine inamgharimu
kukodisha jenereta kwa gharama kubwa.
Hassan Juma
mwanachuo katika chuo kikuu cha mtakatifu Joseph Songea anasema tatizo la umeme
limechangia kuathiri masomo katika kozi yao ya shahada ya sayansi ya kompyuta
ambayo inahitaji matumizi ya kompyuta ambayo haiwezi kufanya kazi bila nishati
ya umeme.
“Mji wa Songea
umebahatika kuwa na vyuo vikuu karibu vitano hivyo serikali inatakiwa
kujitahidi kutafutia ufumbuzi wa kudumu tatizo la umeme ambalo linaathiri
maendeleo ya elimu na uchumi kwa ujumla’’,alisisitiza.
RAIS Jakaya
Kikwete mwezi Agosti 2009 alifanya ziara katika mkoa wa Ruvuma kwa lengo la
kuangalia shughuli za kimaendeleo pamoja na changamoto zinazowakabili wananchi
wa mkoa huo.
Siku ya kwanza ya ziara yake Rais wakati
anapita barabarani akitokea uwanja wa ndege wa Songea wananchi walikuwa
wakipiga kelele na kudai umeme huku wamewasha taa mchana kutokana na hali
halisi ya tatizo sugu la umeme katika mji wa Songea ambalo linakwamisha
shughuli za kijamii na kiuchumi.
Rais Kikwete kwa namna ya pekee aliguswa na alisikitishwa na kasi ndogo ya kushughulikia
ufumbuzi wa tatizo la vipuri vya mashine za kufulia umeme katika mji wa Songea hali liyosababisha
kumwagiza meneja wa TANESCO mkoa wa Ruvuma wakati huo injinia Monica
Kebara kufuatilia ili kujua vipuli vya mashine hizo vipo wapi na alitaka
kupata ripoti ya vipuri hivyo na mwenendo mzima wa matengenezo ili
wananchi wafahamu kila hatua.
Rais Kikwete
hakuishia hapo,badala yake aliahidi kuileta mashine mpya ya kufua umeme ambayo
aliamini ingeweza kumaliza tatizo la mgawo mkali wa umeme katika mji wa Songea
makao makuu ya mkoa wa Ruvuma hivyo mgawo mkali wa umeme kubakia kuwa historia.
Baada ya kufungwa
mashine mpya ya Rais Kikwete aina ya ABC yenye uwezo wa
kuzalisha megawati 1.6 angalau tatizo la mgawo mkali katika mji wa
Songea lilipungua kwa miaka takribani miaka mitatu,ingawa matatizo ya mafuta na
vipuri yaliendelea na kuathiri umeme katika mji wa Songea.
Hata hivyo tatizo
la mgawo mkali wa umeme limeongezeka mwaka huu kutokana na kile ambacho
kinatajwa na TANESCO kuwa ni kuharibika kwa mashine kutokana na vipuri
kuharibika.
Kutokana
na tatizo la umeme kuongezeka katika mji wa Songea kaimu mkurugenzi wa shirika
la umeme nchini Mhandisi Felchesmi
Mramba wiki iliyopita alilazimika kufanya ziara ya siku moja mjini Songea ili
kujionea hali halisi ya tatizo la umeme katika Manispaa ya Songea ambao alisema
unatokana na kuharibika kwa vipuri vya mashine ya kufua umeme aina ya
ABC.
Hata
hivyo Mramba alithibitisha kuwa vipuri vipya vya mtambo huo vimeshafika
nchini kutoka nchini uholanzi na kwamba mwishoni mwa juma hili ufungaji wa
vipuri hivyo ulitarajiwa kukamilika katika mji wa Songea.
Meneja wa TANESCO mkoa wa Ruvuma
mwandisi Fransis Maze amekiri kuwa vipuri vipya kutoka Uholanzi tayari
vimewasili mjini Songea na wiki hii mafundi wamemaliza kazi ya kuvifunga katika
mashine za kuzalishia umeme aina ya ABC.
“Hivi sasa tunasubiri kipuri kimoja
aina ya turbo charger ambacho kimekwama Dar es salaam kutokana na taratibu za
uwanja wa ndege kutokamilika,tunatarajia hadi mwisho wa mwezi huu Oktoba kifaa
hicho kitakuwa kimefika Songea kazi ya kukifunga itachukua takribani masaa
mawili hivyo mwanzoni mwa mwezi ujao tatizo la mgawo mkali wa umeme Songea
litakuwa limepatiwa ufumbuzi’’,alisema.
Hata hivyo meneja huyo wa TANESCO mkoa
wa Ruvuma alibainisha kuwa mahitaji ya
umeme katika mji wa Songea ni kilowatts 4300 na kwamba umeme unaozalishwa hivi
sasa ni kilowatts 3050 hali
inayosababisha mgawo mkali wa umeme hasa katika maeneo pembezoni mwa mji.
“Hakuna mgawo mkali katikati ya mji
ambako kuna taasisi muhimu ambazo zinahitaji umeme kama vile benki, hospitali,
viwanda vidogo,ofisi za serikali,mgawo mkali upo maeneo ya pembezoni mwa
mji’’,alisema Maze.
Wakati wakazi wa
Songea wanalia na umeme,waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhungo
amesema tatizo la umeme nchini lazima litoweke,ndiyo maana serikali inafanya
jitihada mbalimbali za kuongeza uzalishaji wa umeme,ukiwemo mradi wa Kinyelezi
ambao utazalisha Megawati 330 na utagharimu
dola za Marekani milioni 350.
TANESCO kwa
kushirikiana na ufadhili wa serikali ya Sweden chini ya shirika lake la SIDA,inaanza
utekelezaji wa mradi wa umeme kutoka Makambako mpaka Songea ambapo awali
kulikuwa na mpango wa kuweka mradi wa kujenga njia ya umeme wa kilovolti 220
mpaka Madaba na kilovolti 132 kutoka Madaba mpaka Songea.
Taarifa ya wizara ya nishati na madini
inaeleza kuwa ujenzi wa mradi wa njia kuu ya kusafirisha umeme wa gridi kutoka
Makambako hadi Songea ambao utahusisha pia kujenga mifumo ya kusambaza umeme
vijijini katika Wilaya za Ludewa, Namtumbo na Mbinga ni hatua muhimu ya kuleta
maendeleo endelevu katika mikoa ya Kusini
Wizara
ya nishati na madini imedhamiria kupunguza utegemezi wa umeme wa maji kwa
kuendeleza vyanzo mbalimbali ikiwa ni pamoja na umeme utakaozalishwa kwa
kutumia makaa ya mawe kupitia miradi ya Kiwira (Megawati 200) na Mchuchuma
(Megawati 400).
Sera
ya Serikali katika umeme ni kuhakikisha wananchi wengi wanapata nishati ya
umeme,ingawa takwimu hivi sasa zinaonesha kuwa wananchi wanaopata nishati ya
umeme haizidi asilimia 10 ya wananchi wote nchini na kati ya asilimia 10, ni
asilimia moja tu ya wananchi wanaoishi vijijini ndio wanaopata nishati ya
umeme.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:
Post a Comment