Tuesday, December 24, 2013

Samaki wanaokufa ziwa Nyasa hawana madhara


Na Albano Midelo,Nyasa
 Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) Dk.Benjamin Ngatunga  amethibitisha utafiti kubaini kuwa samaki wanaokutwa wamekufa wenyewe katika ziwa Nyasa hawana madhara kwa walaji.
Akizungumza katika mahojiano na gazeti hili Dk.Ngatunga alisema utafiti uliofanyika hivi karibuni katika ziwa Nyasa upande wa Tanzania na Malawi umebaini kuwa tatizo la vifo vya samaki katika ziwa hilo vimekuwa  vinatokea na kusababishwa na mabadiliko ya mkondo wa maji ambao unatokea katika ziwa hilo kila baada ya kati ya miaka 15 na 20 .
“Miaka yote maji ya juu  na ya chini ya ziwa huwa hayachanganyiki, hata hivyo kila baada ya miaka kati ya 15 na 20  maji ya chini yanaweza kuwa  mita 600 na kuchanganyika na maji  ya juu yaliyopo mita 200 tu kwa hiyo maji ya chini ambayo hayana oksjeni  yanapofika  juu husababisha  samaki wakose hewa na hatimaye kufa’’,alisema.

Hata hivyo alibainisha kuwa samaki wanaokufa katika ziwa Nyasa wanaweza kuliwa, amewataka wananchi kuondoa utumbo katika samaki waliokufa wenyewe kabla ya kula na kwamba wanapokula samaki bila kutoa  utumbo  wanakuwa na radha ya chungu sana  na kusisitiza ukiachia uchungu hakuna madhara yanayoweza kutokea kiafya kwa walaji.
Aliongeza kuwa mwaka huu kati ya mwezi Machi hadi Mei tatizo la samaki kufa ovyo katika ziwa Nyasa lilitokea na idadi ya samaki waliokufa ilikuwa ni kubwa zaidi ukilinganisha na miaka 15 iliyopita ndiyo maana wananchi walikuwa na  hofu kubwa kwa kuwa waliona ni tukio jipya kwao.
Kulingana na Dk.Ngatunga vifo vya samaki katika ziwa Nyasa mwaka huu havikutokea upande wa Tanzania pekee,bali hata ziwa Nyasa nchini Malawi  vifo vya samaki vilikuwa ni vingi zaidi ya vile vilivyotokea  upande wa Tanzania hali ambayo ilizua hofu kubwa kwa wakazi wa Malawi kuanzia mwezi Februari mwaka huu.
Amewashauri watafiti na wataalamu kuendelea kutoa elimu sahihi kuhusiana na vifo vya samaki vinavyotokea katika ziwa Nyasa na kuwaasa wanasiasa kuacha kueneza taarifa ambazo sio za kisayansi kuhusiana na vifo vya samaki hali ambayo inawatia hofu wananchi wa pande zote za ziwa  Nyasa Tanzania na Malawi.
Kwa upande wake waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Dk.Teresa Huvisa, akizungumza na wananchi mwambao mwa ziwa Nyasa alikiri kupata taarifa kuwa samaki wanaokufa katika Ziwa Nyasa wamekuwa wanaleta hofu kwa wananchi wa nchi zote mbili Tanzania na Malawi, na kwamba wizara yake imetuma wataalamu kufanya uchunguzi  wa vifo vya samaki ili kubaini kiini cha tatizo hilo iwapo linachangiwa na uchafuzi wa mazingira katika ziwa Nyasa.  

Hata hivyo alisema kuna baadhi ya wavuvi wanatumia majani yanayoitwa mtunungu kuvulia samaki ambayo ukimwaga ziwani au mtoni samaki wanakufa, na kuwatahadharisha wavuvi waache kutumia njia haramu za uvuvi ili kutoharibu mazalia na kuuwa samaki.

Hata hivyo kuanzia mwezi Septemba mwaka huu idadi ya vifo vya samaki wanaokufa wenyewe katika ziwa Nyasa imepungua na baadhi ya maeneo hakuna samaki wanaokufa kabisa.Uchunguzi umebaini vifo vya samaki bado vinatokea katika maeneo ya Ndumbi na Lituhi.

 Baadhi ya wavuvi waliohojiwa  katika  eneo la Ndumbi mwambao mwa ziwa Nyasa wamedai kuwa samaki wana tabia ya kula  vumbivumbi za makaa ya mawe ambazo zimetapaa katika bandari ya Ndumbi ambayo  inatumika kusafirishia makaa ya mawe.

 Fransis Chuwi mvuvi wa Ndumbi akizungumza kwa niaba ya wenzake alidai kuwa   wao kama wavuvi wamebaini kuwa vifo vya samaki vilianzia  ukanda wa Lituhi na Ndumbi kabla ya kuenea maeneo mengine kama Liuli na Mbambabay na kudai kuwa sababu kubwa ni vumbi la makaa ya  mawe  kuliwa na samaki katika bandari ya Ndumbi.

“Vumbivumbi la makaa ya mawe  ndiyo chanzo cha vifo vya samaki katika bandari ya Ndumbi,sisi kama  wavuvi tumegundua kuwa wanaposimamisha kupitisha makaa ya mawe katika bandari ya Ndumbi vifo vya samaki vinapungua,miezi mitatu iliyopita walipitisha makaa ya mawe kwa wingi na  samaki wengi walikufa,hivi sasa wametulia kidogo na samaki wamepumzika kufa hivyo sisi tumegundua tatizo ni makaa ya mawe’’,alidai mvuvi huyo.

Dk.Ngatunga mkurugenzi wa TAFIRI  nchini amepinga madai ya wavuvi hao kudai vumbi la makaa ya mawe kusababisha vifo vya samaki na kusisitiza kuwa wavuvi wanaongea jambo ambalo halijafanyiwa utafiti wa kisayansi ambao TAFIRI imechunguza katika nchi mbili na kubaini tatizo la vifo vya samaki ni mabadiliko ya mkondo wa maji katika ziwa na sio vinginevyo.
Mwaka huu kati ya mwezi Machina Mei  idadi kubwa ya samaki katika ziwa Nyasa walionekana kufa ovyo na  kuelea ndani ya ziwa Nyasa kwenye maeneo ya kata tano za Lituhi, Kihagara Liuli, Lipingo,Mtipwili hadi vijiji vya mpakani na nchi ya Msumbiji.
Samweli Kaseke na Isack Kamanga wavuvi wa forodha ya Hongi na Nkali kata ya Liuli waliwataja  aina ya samaki ambao walioongoza kufa kwa wingi kuwa ni pamoja na ligong’wa, njeringu ,likuku, vindongo, vigong’o, vituhi, hango, ngisi,mbufu,lihenji,magege na batazibi.
 Kaimu afisa Uvuvi wa wilaya ya Nyasa  Joseph Mwingira alisema utafiti wa awali ulibaini kuwa samaki wanaokufa  na kuelea juu ya maji walionekana kuwa na majeraha ya kubabuka katika sehemu mbalimbali za mwili zikiwemo usoni,tumboni,kichwani,mkiani na  mgongoni.
Kulingana na utafiti ambao ulifanywa na jumuiya ya nchi zilizo kusini mwa Afrika(SADC) kwa kushirikiana na  nchi ya Uingereza kwenye ziwa Nyasa kati ya mwaka 1991 hadi 1994 na mwaka 1996 hadi 2000,ulionesha kuwa ziwa hilo lina kiasi cha tani 165,000 za samaki na kati ya kiasi hicho tani 35,000 za samaki ni jamii ya samaki wa maji ya juu ambao wanaweza kuvuliwa bila kuathiri uvuvi kila mwaka.
 Ziwa Nyasa limezungukwa na nchi tatu ambazo ni Tanzania,Malawi na Msumbuji.Ziwa hilo lipo kwenye usawa wa meta 500 toka usawa wa bahari, kina cha ziwa hilo ni karibu meta 750,urefu wake ni karibu  kilometa 1000,upana mkubwa ni kilometa 80 na upana mdogo ni kilometa 15.

No comments:

Post a Comment