Na
Albano Midelo
Kila
saa watu 10 wanakufa kwa malaria
UGONJWA
wa malaria umeuwa watu 652 katika mkoa
wa Ruvuma mwaka 2011 kati ya wagonjwa
zaidi ya 43,000 waliougua ugonjwa huo katika kipindi hicho.
Mratibu wa malaria mkoani Ruvuma Kibua Kakolwa anabainisha kuwa kati ya wagonjwa waliopoteza maisha watoto chini ya umri wa miaka mitano walikuwa 334 na wenye umri wa zaidi ya miaka mitano
walikuwa 318.
Kwa
mujibu wa mratibu huyo wa malaria katika mwaka huo pekee mkoa ulilaza wagonjwa
wenye umri chini ya miaka mitano wapatao 21,940 na walio zaidi ya umri huo
walikuwa 21,819.
“Katika
mkoa wa Ruvuma ugonjwa wa malaria bado ni tishio katika wilaya zote tano za
Songea,Mbinga,Nyasa,Namtumbo na Tunduru na unaoongoza kwa kusababisha vifo
vingi ukilinganisha na magonjwa mengine kwa mfano katika kipindi cha kuanzia
mwaka 2008 hadi 2011 malaria imeuwa watu 3,451’’,alisema.
Takwimu za
mwaka jana za mkoa zinaonyesha kuwa idadi ya wagonjwa wa nje wa malaria wenye umri
chini ya miaka mitano walikuwa 216,311
ambao ni sawa na asilimia 45 ya wagonjwa waliopokelewa na wagonjwa wenye umri
zaidi ya miaka mitano walikuwa 207,664
sawa asilimia 40 ya wagonjwa
wote.
Hata
hivyo Kakolwa alisema katika miaka mitatu mfululizo takwimu zinaonesha wagonjwa
wa malaria wamepungua kwa wastani wa asilimia 6.5 na vifo vitokanavyo na
ugonjwa huo vimeweza kupungua kwa wastani wa asilimia 15.4 na kwamba vyandarua 706,219 vilivyogawiwa kwa wananchi
vimechangia kupunguza ugonjwa wa malaria.
Takwimu za kitaifa zinaonyesha kuwa ugonjwa wa malaria bado ni tatizo
kubwa hapa nchini kwa kuwa ugonjwa
huo ndiyo unaoongoza kwa kusababisha
idadi kubwa ya vifo ambapo watanzania kati ya 60,000 hadi 80,000 wanakufa
kutokana na ugonjwa huo kila mwaka.
Kwa mujibu wa takwimu hizo kila siku watu 291
wanapoteza maisha kutokana na ugonjwa wa
malaria wengi wao ni watoto chini ya miaka mitano, kwa maneno mengine katika
kila saa moja wanakufa watu zaidi ya 10 kwa ugonjwa wa malaria.
Kati ya vifo vinavyotokea kila mwaka
kutokana na ugonjwa huo asilimia 90 ni vifo vya watoto chini ya umri wa miaka
mitano na kwamba ugonjwa huo huleta athari nyingi za kiuchumi na kusababisha
kupunguza pato la taifa la ndani kwa asilimia 3.4 kila mwaka.
Asilimia
93 ya watanzania wanaugua malaria
Inakadiriwa kuwa zaidi ya asilimia 93 ya watanzania wanaokadiriwa
kufikia zaidi ya milioni 45 wapo katika hatari ya kuambukizwa malaria na hivyo
kuifanya Tanzania kuwa nchi ya tatu duniani kuwa na idadi kubwa ya watu wengi
walio katika hali hatarishi ya kuambukizwa malaria.
Takwimu zinaonesha kuwa ugonjwa wa
malaria unasababisha zaidi ya asilimia 33 ya vifo vya watoto chini ya umri wa
miaka mitano na vifo zaidi ya asilimia 20 vya akinamama wajawazito.
Hata hivyo takwimu hizo zinaonesha
kuwa karibu asilimia 80 ya vifo vya watoto chini ya miaka mitano vilitokana na
ugonjwa wa malaria na kwamba inakadiriwa kiwango cha vifo vya watoto 165 kati
ya kila vizazi hai 100,000 kila mwaka vinatokana na ugonjwa wa malaria.
Takwimu kutoka wizara ya afya na ustawi
wa jamii zinaonesha kuwa kila mwaka watanzania wapatao milioni 18 wanaugua
ugonjwa wa malaria hali ambayo inalifanya taifa kupoteza mapato mengi ambapo
inakadiriwa kila mwaka zaidi ya sh. milioni 350 zinapotea kwa ajili ya malaria.
Kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Afya na
Ustawi wa Jamii, ugonjwa wa malaria ndio unaoongoza kwa mahudhurio ya wagonjwa
wanaofika kwenye vituo vya kutolea huduma za Afya, na kwamba matukio takriban
12 milioni ya malaria hutolewa taarifa.
Juhudi zinaendelea kufanywa na serikali kwa
zaidi ya miaka 10 sasa kupitia wizara ya afya na ustawi wa jamii kwa
kushirikiana na mashirika mengine yasiyokuwa ya kiserikali na juhudi hizo zimeanza kuzaa matunda kutokana na takwimu
kuonyesha kuwa idadi ya vifo imepungua
ambapo takwimu za awali zilizionesha kuwa watu zaidi ya 100,000 walikufa kila
mwaka kutokana na malaria.
Serikali inayoongozwa na Rais Jakaya
Kikwete imeanzisha kampeni kubwa ya
kuwafahamisha na kuwaelimisha wananchi katika nchi nzima ya kuhakikisha kuwa
ugonjwa wa malaria unatokomezwa.
Moja ya fursa kubwa ambayo imefanywa
na serikali kupitia wizara ya afya na ustawi wa jamii ni kugawa vyandarua zaidi
ya milioni 20 vyenye dawa ambapo ugawaji huo ulianza kwa kuwapatia watoto chini
ya miaka mitano.
Serikali kupitia wizara ya afya na
ustawi wa jamii inatekeleza mpango kuanzia mwaka 2008 hadi 2015 ambapo lengo kuu
la mpango huo ni kuhakikisha kuwa vifo vinavyotokana na ugonjwa wa malaria
vinapungua kwa asilimia 80 katika idadi
ya wagonjwa na vifo.
.
Sera ya afya ya mwaka 2007 katika ukurasa wa
16 inatamka wazi kuwa Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali zikiwemo
jumuiya za
kimataifa itaendelea kuandaa na kuboresha sheria, miongozo na mikakati ya
kudhibiti magonjwa ya kuambukiza, milipuko pamoja na yale yanayojirudia na
mapya kwa wakati muafaka.
Dalili
za malaria hizi hapa
Watalaamu wa malaria wanasema tiba ya mapema
na sahihi dhidi ya ugonjwa huo ni jawabu katika kupunguza idadi kubwa ya vifo
na wagonjwa hususani kwa watoto.
Kwa mujibu wa Mpango wa Taifa wa
kudhibiti malaria dalili za jumla za malaria ni pamoja na ,homa,maumivu ya
kichwa, tumbo kuuma, kuharisha, kichefuchefu, kizunguzungu, kutokwa jasho, kutetemeka,kukosa
hamu ya kula, uchovu, kupoteza fahamu,degedege,kutapika,kupoteza fahamu, kupumua
kwa shida na kukojoa mkojo wenye rangi kahawia au nyeusi.
Rais Jakaya Kikwete akizungumza wakati
anazindua kampeni za kupambana na malaria alisema malaria ni vita ambayo ni
lazima kupigana nayo na kuishinda kwa sababu serikali ina uwezo wa kuutokomeza
ugonjwa huo hivyo kukifanya kizazi cha
sasa kuwa cha mwisho kuugua na kufa na malaria.
Watalaamu wa afya wanasema kuna njia
tatu za kupambana na hata kuutokomeza ugonjwa wa malaria ambao ni kuhakikisha
kuwa watu wote wanaougua malaria wanapata tiba sahihi ambayo ni dawa yenye nguvu ya kuuwa wadudu
wanaosababisha ugonjwa wa malaria ambao wamejenga tabia ya kubadilika
kimaumbile.
Njia ya pili ya kutokomeza malaria ni
kuhakikisha kuwa watu wasiumwe na mbu wa malaria kwa kuhakikisha kuwa wanatumia
vyandarua vilivyotiwa dawa ya kuuwa mbu
hali ambayo itamwezesha mtu
asipate malaria.Akinamama wote wajawazito na watoto wanatakiwa kulala katika
vyandarua vyenye dawa kwa kuwa malaria ni chanzo kikuu cha vifo vya wajawazito
na watoto chini ya miaka mitano nchini.
Tanzania imepatiwa vyandarua zaidi ya
milioni tano kutoka serikali ya marekani
na Global Fund ambapo serikali
inasimamia kuhakikisha kuwa kila kaya angalau imepata vyandarua viwili vilivyotiwa dawa hivyo
kufanya idadi ya mbu wanaokufa kuwa wengi na wananchi angalau watakuwa wamekingwa na malaria.
Njia ya tatu ya kutokomeza malaria ni
kuhakikisha kuwa mbu wanaoambukiza malaria hawaendelei kuzaliana kwa kuwauwa
kwenye mazalia yao yote pamoja na sehemu zote ambazo wanatua ili kuwatokomeza
kabisa mbu wanaoeneza malaria.
Wizara imeshindwa kufikia malengo
Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Ugonjwa
wa Malaria wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, ulilenga kupunguza idadi
ya wagonjwa na vifo kwa asilimia 50 hadi kufika 2013. Kwa maneno mengine,
Wizara ililenga kuwapunguza wagonjwa wa malaria hadi kufikia milioni sita na
idadi ya vifo kufikia kati ya 30,000
hadi 40,000 mpango ambao bado
haujafanikiwa kwa kuwa idadi ya wagonjwa na vifo bado ni kubwa.
Mratibu wa asasi binafsi ya
ORES-Tanzania ambayo inashiriki katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa malaria
Dr.Hermengild Mayunga anasema ili kufanikisha mapambano dhidi ya ugonjwa huo
inatakiwa kuongezwa ushiriki wa wanasiasa,viongozi wa serikali na jumuiya
katika masuala mtambuka juu ya malaria.
“Nasisitiza muingiliano wa kisekta na
sekta zisizo za afya katika utekelezaji makini wa hatua au njia za kuzuia na
kudhibiti malaria kwa mfano miradi ya tathimini ya madhara ya malaria,mafunzo
ya kujenga uwezo kwa sekta za afya na zile zisizo za afya”anasisitiza
Dr.Mayunga.
Ikumbukwe kuwa ugonjwa wa malaria
hauna mipaka hivyo msisitizo katika
mapambano dhidi ya ugonjwa huo ni lazima kasi iongezwe kila mwaka ili siku moja
ugonjwa wa malaria utokomezwe,tuanze kuhesabu siku za ugonjwa wa malaria
kuwasumbua watanzania zinakwisha mbona wenzetu wameweza sisi tushindwe kuna
nini hapa”,anauliza Dr. Mayunga.
Dr.Mayunga anasisitiza kuwa hivi sasa
ni kipindi ambacho wanasayansi wanatakiwa kukumbuka kuibua mbinu mpya, mikakati
mipya na utalaamu mpya wa kitafiti katika kutokomeza malaria na kujifunza
kutoka katika nchi ambazo tayari zimetokomeza malaria.
Matokeo ya maazimio ya Maraisi mbalimbali duniani walipokutana mjini Abuja
nchini Nigeria Aprili 25 mwaka 2000 walikubaliana mikakati maalum ya miaka kumi
katika kuutokomeza ugonjwa wa malaria ambapo matokeo yake yalitakiwa yapimwe
mwaka 2010.
Matokeo hayo bado yanaonyesha kuwa
ugonjwa huo ni tishio katika maisha na kwamba inatakiwa kuongeza juhudi katika
mapambano dhidi ya malaria ili kufikia kiwango cha asilimia 100 hivyo kufikia idadi
sifuri ya vifo kufikia malengo ya
milenia 2025.
Watu
milioni 500 wanaugua malaria Duniani
Takwimu kutoka shirika la afya
ulimwenguni WHO za mwaka 2002 zinaonyesha kuwa kila mwaka watu kati ya milioni 300 hadi 500 duniani
wanapata ugonjwa wa malaria, kati yao watu milioni moja na nusu wanakufa
kutokana na ugonjwa huo.
Kulingana na takwimu hizo katika bara
la Afrika watoto wadogo wenye umri chini
ya miaka mitano ndiyo wanaathirika zaidi na ugonjwa wa malaria ambapo kila
mwaka watoto milioni tano wanakufa kwa ugonjwa huo barani Afrika.
Hata hivyo jambo la kutia moyo katika
mapambano dhidi ya ugonjwa wa malaria hapa nchini ni utafiti kuhusu chanjo ya
malaria ambao unaendelea kufanywa katika mikoa mbalimbali ukiwemo mkoa wa
Morogoro.
Utafiti huo hadi sasa unatia matumaini
makubwa ya kupatikana kwa chanjo dhidi ya ugonjwa wa malaria ambayo ikipatikana
hapana shaka utakuwa ndiyo mwisho wa ugonjwa huo ambao unaua watu wengi na
kudhoofisha uchumi wa taifa.
albano.midelo@gmail.com, simu
0784765917
No comments:
Post a Comment