TAHADHARI imetolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini (TMA) ya kuwepo
kwa Vipindi vya Mvua kubwa, Upepo Mkali na Mawimbi Makubwa .
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na
TMA jijini Dar es Salaam maeneo yatakayo athiriwa na hali hiyo ni
pamoja na mikoa ya Mbeya, Njombe, Ruvuma pamoja na kusini mwa mkoa wa Morogoro.
Ikifafanua zaidi taarifa hiyo
ilibainisha kuwa vipindi vya mvua kubwa zenye ujazo wa zaidi ya mm 50 ndani ya
saa 24 zitanyesha huku zikiambatana na hali ya Upepo mkali unaozidi kilomita 40
kwa saa pamoja na mawimbi makubwa zaidi ya mita 2.0.
“…Maeneo yanayotarajiwa kuathirika
na mvua kubwa ni Ukanda wa Pwani mikoa ya Tanga, Dar es Salaam, Pwani, Lindi,
Mtwara pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba. Upepo Mkali na Mawimbi Makubwa
yatavuma Pwani ya mikoa ya Tanga, Dar es Salaam, Pwani, Lindi, Mtwara pamoja na
visiwa vya Unguja na Pemba,” ilisema taarifa hiyo ya TMA.
“Hali hii inatokana na kuwepo kwa
kimbunga “FOBANE” kusini magharibi mwa Bahari ya Hindi. Mfumo huu unatarajiwa
kuvuta upepo kutoka Pwani ya Somalia na misitu ya Congo kuelekea maeneo ya nchi
yetu,” ilisema taarifa hiyo.
Hata hivyo angalizo limetolewa kwa
watumiaji wa bahari na wakazi wa maeneo hatarishi, hivyo wanashauriwa kuchukua
tahadhari. Imebainisha kuwa Mamlaka ya Hali ya Hewa inaendelea kufuatilia hali
hii na itatoa mrejeo pale itakapobidi.
MAMLAKA YA HALI YA HEWA NCHINI


No comments:
Post a Comment