Na
Livingston Benson-OUT
Baadhi ya wakazi wa
kata tano katika wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma ambazo zimezungukwa na mradi
wa uchimbaji wa madini ya uranium(urani) wamelipongeza shirika la CARITAS kwa
kutoa elimu ya madhara ya madini hayo kiafya na kimazingira.
Wakazi hao walitoa
pongezi hizo wakati wa ufungaji wa mafunzo ya uelewa wa madini ya uranium
awamu ya pili yaliofanyika katika ukumbi wa CARITAS jimbo kuu la Songea.
awamu ya pili yaliofanyika katika ukumbi wa CARITAS jimbo kuu la Songea.
Mwezeshaji wa mafunzo
hayo Leonard Mgaya alisema mafunzo hayo yalianza Novemba mwaka 2014 hadi Desemba mwaka 2015 ambayo yalishirikisha
wawakilishi 30 kutoka kata zinazozunguka mradi wa urani wilayani Namtumbo
ambazo ni kata za Likuyuseka, Mgombasi,Mchomolo,Kitanda na Lwinga.
Mgaya alibainisha
matokeo ya mradi wa mafunzo hayo ambayo pia yalishirikisha waandishi wa habari
30 kutoka mkoani Ruvuma yamewezesha wakazi wanaozunguka mradi kuelewa madhara
ya madini ya urani na kuchukua tahadhari pale wanapofanyakazi mgodini ili
wasipate madhara.
Hata hivyo mmoja wa
washiriki ambaye pia ni mwenyekiti wa asasi ya Tanzania mineral mining Trust
Fund Wilbert Mahundi ambaye pia ni
diwani wa kata ya Ruhuwiko,alitaja changamoto kubwa iliyojitokeza katika mradi
huo ni vitisho kutoka serikalini kwa kuwa inapinga madhara ambayo yanatajwa na
wataalam ambayo yanaweza kupatikana kutokana
na madini ya uranium.
Wakizungumza katika
hitimisho la mafunzo hayo baadhi ya washiriki wamependekeza kuundwa na
kuimarisha mtandao wa urani katika ngazi ya vijiji na kata ili kuendelea
kujenga ufahamu wa madhara yanayoweza kuletwa na madini ya urani.
Washiriki hao pia
wamependekeza kuwepo na usaidizi wa kisheria kwa wananchi wote ambao
watathibitika wameathirika na madini ya urani kwa sababu kwa mujibu wa sheria
kila mtanzania anatakiwa kuishi katika mazingira safi na salama.
Utafiti wa
mradi wa Urani wilayani Namtumbo umekamilika
ambapo Mradi wa madini hayo
katika Mto Mkuju wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma unaomilikiwa na Kampuni ya
Mantra Tanzania Limited na Kampuni tanzu ya URMZ ya Urusi unatarajiwa kuanza
wakati wowote.
Mradi wa
Mto Mkuju upo ndani ya pori la akiba la
Selous (Selous Game Reserve).Eneo hilo ni Sehemu ya Urithi wa Dunia
(World Heritage Site) tangu mwaka 1980.
Mwezi
Julai, 2012,Tume ya urithi wa Dunia yaani World Heritage Committee iliyoko
chini ya UNESCO ilitoa idhini ya kuondoa eneo la Mradi wa Mto Mkuju lenye
ukubwa wa kilometa 345 kati ya kilometa 50,000 kwenye Eneo la Urithi wa Dunia
ili uchimbaji wa Urani uweze kufanyika.
Hata hivyo mwezi Agosti mwaka 2015 aliyekuwa Naibu
waziri wa Nishati na madini Charles Kitwanga alitembelea eneo la mradi la mto
mkuju litakalochimbwa madini ya urani katika wilaya ya Namtumbo na kuwaahidi
wananchi kuanzia mwezi Aprili mwaka 2016
mradi wa uchimbaji wa uranium unatarajia kuanza uzalishaji.
Kitwanga alisisitiza wizara ya nishati na madini
ipo kwenye hatua za mwisho kukamilisha makubaliano ya kuanza rasmi uzalishaji
ifikapo Aprili 2016.
Utafiti wa madini ya urani katika eneo la mto mkuju
lenye ukubwa wa kilomita za mraba 20,000 unasimamiwa na kampuni ya Mantra
Tanzania, tangu mwaka 2007 tayari umeshafanya uwekezaji wa dola za kimarekani
milioni 200.
Kwa muda mrefu wataalam wa mazingira,madaktari
pamoja na wanasheria wamekuwa wanaionya serikali kusimamisha mradi wa uchimbaji
wa madini ya uranium kutokana na kutajwa kuwa na madhara makubwa kuliko faida.
Mradi huo unatarajiwa utadumu kwa miaka 12 tu.
Mradi wa mafunzo ya uelewa wa madini ya urani
katika afya na mazingira wilayani Namtumbo yalifanyikwa kwa kuhusisha mashirika
matatu yasiyokuwa ya kiserikali ambayo ni CARITAS, TMMTF na MVIWATA.
Mwisho

No comments:
Post a Comment