Monday, June 27, 2016

Kwanini sekta ya madini haijawanufaisha watanzania?

Kila wilaya  ya Tanzania kuna aina mbalimbali za madini
 
Ramani mpya ya madini kutoka wizara ya nishati na madini inaonesha kuwa kila wilaya hapa nchini inakadiriwa kuwa na aina 30 za madini.
Maliasili tulizonazo za Madini,gesi na mafuta iwapo hazitasaidia kutatua matatizo na kuboresha huduma za kijamii kama afya,elimu umeme na barabara bora ni sawa na nchi kuwa na laana kwa kuwa rasilimali zilizopo zikisimamiwa kikamilifu zinaweza kuleta maendeleo endelevu kwa watanzania.

Utafiti umebaini kuwa zipo sababu mbalimbali zinazoendelea kusababisha madini kushindwa kuwanufaisha watanzania badala yake madini hayo yameendelea kuwa neema kwa wawekezaji.

Mwanasheria na mkurugenzi wa chama cha wanasheria watetezi wa mazingira Tanzania(LEAT) Dk.Nshala Rugemeleza anasema Sekta ya madini inashindwa kuwanufaisha watanzania kutokana na kumilikiwa na wawekezaji kutoka nje  ambao wanalindwa na sheria ya madini ya mwaka 2010 ambayo inafanya rasilimali ya madini kuendelea kumilikiwa na wageni.

Sheria ya madini ya 2010 ina vipengele vingi ambavyo vinawabeba wawekezaji kutokana na sheria mpya ya madini kunukuliwa kutoka mkakati wa Benki ya Dunia  uliodhamiria kuhakikisha kuwa sekta ya madini inaendelea kumilikiwa na wageni.

Mkakati madhubuti wa Benki ya Dunia wa mwaka 1992 ulikuwa ni kuhakikisha kuwa nchi za Afrika ikiwemo Tanzania zinaendelea kupoteza na kushindwa katika soko la dunia kwa madai kuwa serikali za nchi za Afrika hazina uwezo wa kumiliki mfumo wa uchimbaji madini badala yake mfumo huo umilikiwe na makampuni binafsi ya  nchi za magharibi.

Benki ya Dunia imeweka msukumo wa kuhakikisha nchi za magharibi zinaendelea kunufaika na sekta ya madini ya Afrika ambapo benki hiyo ilisimamia na kutoa mkopo wa dola za kimarekani sh.milioni 50 kwa ajili ya kuifanyia mabadiliko ya sheria ya madini ya mwaka 1998 na kuanzishwa kwa sheria mpya ya madini ya mwaka 2010.

Hata hivyo katika sheria hiyo mpya vifungu vingi vimenukuliwa kutoka mapendekezo ya Benki ya Dunia, mabadiliko ya sheria ya madini ya 2010 haijagusa mabadiliko katika kipengere cha kodi ili makampuni hayo yaendelee kukwepa kodi ambapo mfumo wa ulipaji kodi tangu mwaka 1992 hadi sasa bado unawabeba wawekezaji kulingana na mapendekezo ya Benki ya Dunia.

Mkakati wa Benki ya Dunia kuhusu madini ya Afrika umeshindwa kutoa jibu la moja kwa moja kwamba madini ya Afrika yanachimbwa na kuzinufaisha nchi za Afrika badala yake nchi za magharibi zinaendelea kutafuta vyanzo vipya vya madini ili kuweza kukidhi mahitaji ya madini katika nchi hizo kwa matumizi ya siku za baadaye.

Kulingana na Benki ya Dunia sekta ya madini ni ya kilimwengu na kwamba ili iweze kuwa ya kidunia ni lazima kampuni binafsi za uchimbaji zifanye kazi hiyo kwa kuwa zina mtazamo wa kiulimwengu katika utafutaji na uchimbaji wake,kampuni hizo zinatoka katika nchi za Australia, Canada, Afrika ya kusini,Ulaya na Marekani.

Mkakati huo wa Benki ya Dunia  umeeleza wazi kuwa haupo tayari kuwekeza katika serikali ambayo inachukua Hisa nyingi zaidi ya kampuni binafsi ambapo watu wenye  uwezo mkubwa wa kifedha ndiyo wanaotakiwa kuwekeza katika sekta ya madini,gesi na mafuta eti sekta ya madini inahitaji kuwa na mikataba migumu.

Mkakati mwingine wa kuhakikisha kuwa sekta ya madini inaendelea kuwanufaisha wawekezaji ni kuhakikisha utafutaji na uchimbaji wa madini unafanyika katika nchi za Afrika na kusababisha athari za kimazingira ambapo hatua za uchenjuaji, usafirishaji na utengenezaji wa bidhaa unafanyika katika nchi za wawekezaji ambako wanapata faida kuwazidi wenye raslimali hizo.

Sekta ya madini inaendelea kuwanufaisha wawekezaji badala ya wageni ni kutokana na  mfumo wa profit Transfering ambao unafanywa na makampuni ya uchimbaji,mfumo huu unaziwezesha kampuni hizo kufanya biashara kwa faida kubwa  baada ya kuhamishia faida toka nchi moja yenye kodi kubwa kwenda nchi zenye kodi ndogo.

Kwa mfano kampuni ya BAP Biliton ya Australia inafanyakazi katika nchi tisa na kusababisha kuongeza kiwango cha ukilitimba hadi katika kampuni nyingine ndogo ndogo zinazochimba madini ,mfano mwingine ni kampuni ya Anglo America mwaka 1970 ilimiliki zaidi ya kampuni 1000 nchini Afrika ya kusini.
Mkakati wa mataifa ya magharibi kuendelea kumiliki sekta ya madini katika nchi za Afrika walitumia mbinu mbalimbali ikiwemo mbinu ya kuwa na siri kubwa katika utoaji wa taarifa ambapo kampuni hizo hazitoi taarifa za kweli kuhusu utafutaji wa madini.
----Itaendelea-----
Makala hii imeandikwa na Albano Midelo mwandishi ambaye amesomea masuala ya mazingira,madini,mafuta na gesi.

No comments:

Post a Comment