Thursday, June 23, 2016

Manispaa ya Songea yatoa zaidi ya milioni 52 kusaidia wajasirimali

Ni mkopo wa kuendeleza miradi yao,sio kuanzisha miradi mipya

NA KWIRINUS MAPUNDA,SONGEA

HALMASHAURI ya manispaa ya Songea mkoani Ruvuma imetoa mkopo wa zaidi ya shilingi milioni 52 katika vikundi 107 vya wajasiriamali ili kuendeleza miradi yao.
Jenifer Omolo mkurugenzi wa manispaa ya Songea

Akizungumza wakati anafungua mafunzo hayo,mkurugenzi wa manispaa ya Songea Jenifer Omolo amewaasa wanakikundi kukopo fedha hizo zenye riba nafuu na kuacha kwenda kukopa katika asasi za kibenki ambazo zinatoza riba kubwa kwa mkopaji.

“Sisi manispaa tunatoa riba ya asilimia kumi tu kwa mkopo wa mwaka mmoja
,asasi nyingi za kifedha zinatoa riba kubwa yenye makato mengi hali inayosababisha wakopaji kushindwa kufikia malengo yao,hata hivyo ili mfuko uimarike ni lazima mrejeshe mikopo tunayowapatia kwa wakati’’,alisisitiza Omolo.

Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo mwaka jana wakopaji hawajarejesha shilingi milioni 30 ambazo walikopeshwa na Halmashauri hiyo na kuwaagiza wote ambao hawajarejesha warudishe mikopo hiyo na kwamba katika urejeshaji wa fedha za serikali au mkopo hakuna hadithi zaidi ya kurudisha mikopo kabla ya hatua kuchukuliwa.

Kwa upande wake mchumi wa manispaa hiyo Raphael Kimary aliwaasa wajasiriamli hao kuwa na nidhamu katika mikopo  na kuhakikisha wanarejesha kwa wakati.

Kimary alibainisha kuwa mkopo huo wa fedha umetolewa na manispaa kwa lengo kusaidia vikundi vya wajasirimali  katika shughuli za uwekezaji  na kuhakikisha wanarejesha ili kusaidia vikundi vingine  vya wajasirimali katika manispaa hiyo.

“Zingatieni taratibu zote za mafunzo ambayo mmepewa kabla ya kupewa mkopo,fedha hizo zisifanye mambo ambayo hayapo katika mradi huo,muwe wajasirimali wa kweli ili muweze kuondokana na umaskini,kumbukeni fedha tunazowakopesha  zitafuatiliwa  na mnatakiwa kurejesha mkopo kwa wakati ili tuendelee kuwakopesha wajasirimali wengine’’,alisisitiza Kimary.
Baadhi ya vikundi vya wajasirimali wakipata mafunzo

Kwa upande wake afisa maendeleo ya jamii wa manispaa hiyo  Naftali  Saiyoloi alisema mkopo huo unatolewa kwa vikundi vya wanawake na vijana na kwamba lengo ni kuinua hali ya uchumi katika makundi hayo mawili.

Kwa mujibu wa afisa maendeleo huyo,mfuko wa kukopesha wanawake na vijana ulianzishwa mwaka 1993 na kwamba mfuko huo licha ya kuwa na fedha kidogo ,umelenga kuongeza ajira,kuinua uchumi wa mwananchi wa kawaida na hasa vijana na wanawake.

“Masharti yanayomwezesha mjasiriamali kupata mkopo huo,awe  mwanamke au kijana mwenye umri wa kuanzia miaka 18 na kuendelea,awe amejiunga kwenye vikundi vya kuanzia watu watano,kikundi kiwe na katiba,mkopo unalipwa ndani ya mwaka mmoja kwa riba ya asilimia 10 tu’’,alisema.

Akitoa mada ya kanuni za kikundi,akiba ya pamoja na umuhimu wake,afisa maendeleo ya jamii Scholastica Gowele aliwatahadharisha wajasirimali hao kuwa lengo la mkopo huo sio kuanzisha mradi au biashara mpya badala yake ni kuendeleza biashara ambazo wamezianzisha ili ziweze kuwaletea faida zaidi.

Naye afisa biashara wa manispaa hiyo Raymund Raphael aliwataka wanavikundi kuhakikisha kuwa wanafanya biashara ambayo itawapatia faida hivyo kabla ya kuendeleza biashara zao ni vema kwanza kufanya utafiti wa  ili kufahamu wateja wao na masoko ya biashara zao.

Mada ambazo zimefundishwa katika mafunzo hayo ni  historia fupi ya mfuko wa maendeleo ya wanawake na vijana,taratibu na masharti ya mkopo,usimamizi na ulipaji wa mikopo,namna ya kuunda vikundi,uendeshaji na usimamizi wa miradi ya vikundi,soko la biashara,mahusiano ya biashara,utunzaji wa kumbukumbu na ujazaji wa mikataba.

Mwisho.

No comments:

Post a Comment