Na Kwirinus Mapunda
HALMASHAURI ya
manispaa ya Songea mkoani Ruvuma imeweka mpango mkakati wa miaka mitatu kuanzia
mwaka 2016/2017 hadi 2019/2020 ili kuwa na mwelekeo wa utoaji wa huduma za
msingi za kuanzishwa kwa Halmashauri ya
jiji la Songea.
Ofisa habari wa
manispaa ya Songea Albano Midelo anasema mpango mkakati wa miaka mitatu katika
manispaa hiyo umetolewa na Baraza la
madiwani kwa kushirikiana na wataalam
mbalimbali wa manispaa hiyo.
Lengo la manispaa
hiyo ni kusimamia na kutekeleza kwa
ufanisi majukumu ya Halmashauri ambayo yameainishwa katika sheria namba nane ya
uanzishwaji wa serikali za mitaa, miji, manispaa na jiji ili
kutekeleza azma
yake ya safari ya kuelekea jiji la Songea kutoka manispaa.
Dira ya Halmashauri
ya manispaa ya Songea ni kuwa mji
uliopangika miundombinu ya kisasa na ongezeko la kipato pamoja na kuwa na
wananchi wenye maisha bora na endelevu kwa kudumisha ulinzi,usalama,usafi wa
mji,uadilifu,uwazi,uzalishaji bora hivyo
kukuza manispaa ya Songea na kuwa jiji
la Songea.
Mwelekeo wa
Halmashauri ya manispaa ya Songea ni kutoa huduma bora za kiuchumi na kijamii
kwa wananchi wake kwa kutumia fursa na rasilimali,kuhamasisha, kuendeleza,
kuimarisha na kusajirisha wananchi katika mazingira ya ushindani na
ubadilishaji rasilimali na huduma endelevu.
Mstahiki meya wa Manispaa
ya Songea Abdul Hassan Mshaweji anabainisha kuwa manispaa inatarajia kufikia
malengo ya kuwa jiji kwa kuzingatia Sayansi,teknolojia,utawandawazi na soko
huru kwa kufuata sheria,kanuni na taratibu na kuongeza ufanisi mkubwa kwa
kutumia utawala bora ili kuinua na kuboresha maisha ya wakazi wa manispaa hiyo.
Ili kuhakikisha
uchumi wa Halmashauri ya manispaa inakua,Mshaweji ameutaja mwelekeo ni kuongeza
uzalishaji na mauzo ya bidhaa, kukusanya mapato kwa njia ya kielektroniki
pamoja na kuwa na miradi ya uzalishaji yenye tija na utendaji wenye maadili na
nidhamu kwa kuzingatia kauli mbiu ya Hapa kazi tu ifikapo mwaka 2017.
“Manispaa ya Songea
imejiwekea malengo makuu na malengo mahususi ambayo yanatekelezwa kwa kufuata
shabaha zilizopangwa ili kufikia malengo shughuli mbalimbali zimepangwa kwa
kuzingatia ukomo wa bajeti na vipaumbele
vya kitaifa,hususuani kufuata ilani ya Chama tawala’’,anasema Mshaweji.
Malengo makuu
yatakayohakikisha manispaa inatekeleza mpango mkakati kikamilifu ni pamoja na
kupunguza maambukizi mapya ya virusi vya UKIMWI,kupambana na rushwa na
kuboresha huduma za kiuchumi pamoja na
kuimarisha miundombinu ya mji uliopangika ili uweze kuwa na hadhi ya jiji.
Malengo mengine ni
kuimarisha masuala ya utawala bora, elimu, afya,maji na ukusanyaji wa
mapato,kuwepo kwa usawa wa kijamii,kusimamia maliasili na mazingira,kuwepo
miundombinu bora na ya kisasa,kuwepo zana bora
za kufanyia kazi mbalimbali ili kuongeza mapato.
Manispaa pia imelenga
kuongeza ufanisi katika utendaji na kuacha kufanyakazi kwa mazoea,kuondoa kodi
na ushuru wenye usumbufu kwa wananchi,kupitia kero zote zinazosubiri maamuzi
husuasn sekta ya ardhi na kuendeleza njia za haraka za kumaliza kero za watumishi
wakiwemo walimu,waganga na wafanyabiashara ndogondogo.
Ili kuhakikisha
manispaa inakamilisha safari yake ya kuwa jiji Mstahiki Meya ameitaja moja ya
mikakati iliyopitishwa na manispaa hiyo kuwa ni kufungua barabara zote za mtaa
kwa mtaa, barabara za kata kwa kata na barabara zote za muingiliano na
Halmashauri jirani pamoja na kuhakikisha kuwa umeme wa uhakika unapatikana
katika mji wa Songea.
Katika kuhakikisha huduma za msingi zinatolewa kwa wananchi Halmashauri ya Manispaa ya Songea imeweka
mikakati na Malengo maalum ili kuboresha huduma hizo.Mikakati hiyo ni pamoja na
Kuchangia na kuhamasisha miradi inayoibuliwa
na kutekelezwa na jamii yenyewe na Kuendeleza kilimo masoko na kuboresha miundo mbinu ya kilimo na mifugo
sanjari na kutoa elimu kwa wakulima.
Manispaa ya Songea inatarajia Kujenga miundo mbinu ya miradi ya maji safi
na salama kwa wananchi,Kusimamia utoaji taaluma katika shule za msingi na
sekondari na kuwawezesha wanafunzi wa darasa la saba kufaulu mitihani ya
kuhitimu elimu ya msingi na kuongeza idadi ya wanafunzi wanaojiunga na kidato
cha kwanza.
Kuboresha huduma za afya kwa kukarabati na kujenga majengo ya kutolea
huduma za afya, kuboresha upatikanaji wa madawa na kuongeza wataalam wa kutoa
huduma ni miongoni mwa mikakati iliyowekwa na manispaa hiyo.
Mikakati mingine itakayokamilisha safari ya manispaa ya Songea kuwa jiji ni
Kuboresha miundo mbinu ya barabara kwa kufanyia matengenezo na kujenga madaraja
ya kudumu na kuimarisha shughuli za kiuchumi za wanawake, vijana wazee na sekta isiyo rasmi.
Katika kipindi safari ya kutoka manispaa hadi kuwa jiji la Songea manispaa
hiyo imepanga kuimarisha ushirikiano na wadau wa maendeleo (NGO),Mashirika ya
dini na vyama na vikundi vya kijamii (CBOs) na Kuhamasisha walipa kodi umuhimu
wa kulipa kodi,Kuimarisha na kuendeleza Vyama vya Ushirika vya Akiba na Mikopo
na vyama vya huduma za kifedha vingine.
Halmashauri ya Manispaa ya Songea ina zaidi ya watu 203,309 kulingana na
sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012.Manispaa ya Songea ina kata 21 na mitaa 95
ikiwa ndiyo makao makuu ya mkoa wa Ruvuma.
Halmashauri nyingine ambazo zinaunda mkoa wa Ruvuma ni Halmashauri ya
wilaya ya Songea, Namtumbo, Tunduru, Nyasa,Halmashauri ya wilaya ya Mbinga na
Halmashauri ya mji Mbinga.
kwirinusmapunda@yahoo.com


No comments:
Post a Comment