Friday, June 3, 2016

Nyasa walilia kituo cha mafuta

Wilaya nzima haina kituo hata kimoja cha mafuta

Na Albano Midelo

"Boti ya doria ilishindwa kuwaokoa waliozama ziwa Nyasa  baada ya  wilaya nzima kukosa kituo hata kimoja cha mafuta hivyo boti ilishindwa kusafiri'' anasema mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Nyasa.


Wakazi wa wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma wameendelea kutoa wito kwa serikali kuharakisha mchakato wa ujenzi wa kituo cha mafuta ili kusogeza huduma hiyo  jirani na wilaya.

Wilaya ya Nyasa yenye kata 20 haina kituo hata kimoja cha mafuta hali ambayo inasababisha changamoto kubwa pale inapotokea dharura ya mahitaji ya mafuta ambayo yanapatikana kwenye vituo vya mafuta vilivyopo wilayani Mbinga takribani umbali wa zaidi ya kilometa 60.


Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Nyasa Jabir Shekimweri amesema mahitaji ya kituo cha mafuta katika  wilaya ya Nyasa na hasa mji wa Mbambabay ambayo ndiyo makao makuu ya wilaya hiyo ni makubwa  kutokana vyombo vya usafiri vya nchi kavu na majini kuhitaji mafuta ya petroli na dizeli.

“Hivi karibu kutokana na boti la doria la serikali kukosa mafuta,tumeshindwa kuwaokoa watanzania  karibu 11 ambao walipata ajali ya kuzama na boti wakati wanatoka Mbambabay kwenda nchini Malawi,boti ingekuwa na mafuta pengine tungeweza kuwaokoa’’,alisema mkurugenzi huyo.

Kuna taarifa kuwa mwanamke mmoja akiwa katika boti hilo alimpigia simu mumewe kuwa endapo wangefika katika eneo ambalo walipata ajali kabla ya saa mbili kupita wanaweza kuokolewa lakini walishindwa kwenda huku baada ya boti la doria kukosa mafuta hivyo abiria wote ambao walikuwa katika boti hiyo waliangamia katika ziwa Nyasa.

Kamanda wa polisi wa mkoa wa Ruvuma kamishina msaidizi wa polisi Zuberi Mwombeji amethibitisha abiria wote 11 waliokuwa  katika boti ya MV.Mapenza  walifariki Dunia ambapo hadi sasa ni mati wawili tu wamepatikana na kazi ya kutafuta maiti wengine inaendelea .

Mkurugenzi wa wilaya ya Nyasa ametoa wito kwa serikali kuharakisha ujenzi wa meli ya kubeba abiria na mizigo katika bandari ya Itungi wilayani Kyela mkoani Mbeya kwa kuwa kukamilika kwa meli hiyo kutawezesha wakazi wa mwambao mwa ziwa Nyasa kusafiri kwa meli badala ya boti ambazo hazina uwezo wa kukabiliana na dhoruba ndani ya ziwa hilo.

“Watu wanaposafiri au kusafirisha mizigo kutoka Mbambabay hadi nchini jirani ya Malawi au kusafiri ndani ya wilaya ya Nyasa wamekuwa wanapata maafa makubwa kutokana na kukithiri kwa dhoruba katika ziwa Nyasa hasa kuanzia mwezi Mei hadi Agosti kila mwaka’’,alisema Jabir.

Kuchelewa kufungwa kituo cha mafuta katika eneo la Kilosa wilaya ya Nyasa kunatokana na taarifa potofu   ambazo zilisambazwa na kituo kimoja cha luninga kuwa eneo la ujenzi wa kituo hicho lina mgogoro jambo ambalo limekwamisha mchakato mzima wa ujenzi wa kituo hicho ambao umekwama hadi sasa huku wananchi wakiendelea kuteseka na kuangamia kwa kukosa huduma ya kituo cha mafuta.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Nyasa Alto Komba amekemea tabia ya baadhi ya waandishi wa habari kuandika habari potofu ambazo zinasababisha kudidimiza maendeleo na amependekeza waandishi wanaoandika habari potofu ili zionekane kuwa sahihi waache tabia hiyo  badala yake wafuate sheria,kanuni na weledi wa kazi zao.

Halmashauri ya wilaya ya Nyasa tangu Julai mosi,2013 haina kituo hata kimoja cha mafuta ingawa Halmashauri hiyo inakabiliwa na changamoto nyingi zikiwemo za kufuata mafuta ya petroli na dizeli wilaya jirani ya Mbinga kwa ajili ya shughuli za maendeleo pamoja na huduma kwa wananchi.

Komba anasema  wilaya hiyo inakabiliwa na ongezeko kubwa la watu ambalo linakwenda sanjari na mahitaji makubwa ya mafuta kwa ajili ya magari,pikipiki na vyombo vya majini hivyo kufungwa kituo cha mafuta walau kimoja ni jambo ambalo halina mjadala.

“Halmashauri ya Nyasa inakusudia kutwaa ardhi katika eneo la Kilosa Juu lenye mchoro wa  mipango miji wenye namba TP DRG namba 09/NYS/ 29/04/2014 kwa ajili ya ujenzi wa  kituo cha mafuta,mfano tarehe 19/9/2013  ulifanyika mkutano na wananchi wa Kilosa kwa ajili ya ushirikishwaji katika kuandaa mchoro huu’’,alisema.

Kwa mujibu wa Komba Aprili pili,2014 rasimu ya michoro hiyo iliwasilishwa kwenye kikao cha kamati ya huduma za uchumi na  mazingira kilichokaa katika ukumbi wa shule ya msingi Mbambambay na hatimaye kwenye Baraza la madiwani la Aprili 24,2014.

Amesema baada ya kupitia mchakato huo Aprili 22,2014 rasimu ya michoro  hiyo ilipitishwa katika ofisi ya mkuu wa mkoa wa Ruvuma na hatimaye Aprili 30,2016 rasimu ya mchoro huo iliidhinishwa na mkurugenzi wa mipango miji wizara ya ardhi,nyumba na maendeleo ya makazi na kukoma kuwa rasimu na badala yake  kuwa sheria.

Hata hivyo katika kusudio la kutwaa ardhi  ya Kilosa yenye ukubwa wa ekari moja na nusu kwa ajili ya matumizi ya kituo cha mafuta,ushirikishwaji wananchi ulikuwepo ambapo Machi tisa mwaka huu ulifanyika mkutano na wananchi kueleza azma ya Halmashauri kuhitaji kulipa fidia eneo la Kilosa ili kujenga kituo cha mafuta.

“Wananchi walikubali lakini Machi 19,2016 wananchi hao walionekana kwenye chombo cha habari cha ITV kupitia mwandishi wake anayewakilisha Ruvuma wakidai wameingiliwa kwenye maeneo yao kinguvu na kuwataka wahame ndani ya siku 14 jambo ambalo ulikuwa upotoshaji mkubwa’’,alisema Komba.

Mwenyekiti huyo wa Halmashauri ya Nyasa ameyataja madhara ambayo yamesababishwa na taarifa potofu katika chombo hicho cha habari kuwa ni  hali ambayo inakwamisha mchakato wa kufunga kituo cha mafuta katika eneo la Kilosa hivyo wananchi wa wilaya ya Nyasa kuendelea kuteseka.

Ametolea mfano wananchi wa Likwilu juu kata ya Kilosa walikubali eneo lao kuandaliwa ramani ya mipango miji kwa ajili ya kituo cha mafuta,hata hivyo baada ya habari hiyo potofu  baadhi ya wananchi  walishawishika kusema kuwa  wataalam wa ramani walifukuzwa Kilosa na wameamua kukimbilia kitongoji cha Likwilu hivyo wanasambaza taarifa zinazowafanya wananchi wengine wasikubali maeneo ya kuandaliwa ramani.

Amesisitiza kuwa taarifa potofu  kwa wananchi wa Kilosa zimesababisha wananchi kukosa imani na serikali yao katika mambo ambayo ni uzushi.

Kikao cha Baraza la madiwani katika Halmashauri ya Nyasa kilipitisha maazimio ya kuchukuliwa hatua  na kufikishwa  kwenye kamati ya maadili diwani yeyote ambaye atabainika kushiriki katika uchochezi uliosababisha kuchelewa mchakato wa kukamilisha eneo la kufungwa kituo cha mafuta Kilosa.

Makamu mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Nyasa Charles Chawila ameshauri mgogoro huo upatiwe ufumbuzi haraka ili kituo cha mafuta katika eneo la Kilosa ufanyike haraka kwa kuwa mchakato ulifikia hatua nzuri ikiwemo ya  kuwalipa fidia wananchi ili kupisha ujenzi wa kituo hicho.

Diwani wa kata ya Lipingo Halmashauri ya Nyasa  Cathbert Ngwata  amesema madiwani wa kata zote wanaunga mkono ujenzi wa kituo cha mafuta Kilosa ili kukabiliana na kero ya mafuta inayowakabili wakazi wa wilaya hiyo tangu mwaka 2013.

Kwa upande wake mbunge wa jimbo la Nyasa na Naibu waziri wa elimu,sayansi,teknolojia na ufundi Injinia Stella Manyanya amewaasa wenyeji wa wilaya hiyo kuacha kuweka masharti magumu kwa wawekezaji kama ilivyo kwa mwekezaji wa kituo cha mafuta Kilosa.

“Mazingira ya uwekezaji katika wilaya ya Nyasa bado ni magumu,nawaomba wakazi wa nyasa kuwapa ushirikiano wa kutosha wawekezaji wanaojitolea kuwekeza katika mazingira magumu ,serikali itaendelea kutoa mafunzo ya uwekezaji kwa  katika vijiji vya kata zote za Nyasa ili kuepusha migogoro  dhidi ya wawekezaji’’,alisema Manyanya.

Hata hivyo Manyanya ambaye pia ni diwani alisema taratibu zote zimefuatwa katika mchakato wa ujenzi wa kituo cha mafuta  na kuwaasa wananchi kutambua kuwa ardhi sio mali ya mtu binafsi hivyo ameshauri hatua za kisheria zichukuliwe kwa wote wanaokataa kulipwa fidia ili kupitisha ujenzi wa kituo hicho cha mafuta.

“Natoa mwito kwa Halmashauri wakati mwingine fanyeni maamuzi magumu ili kusimamia sheria zilizopo na hasa kuwabana wananchi wanaouza mafuta kwenye ndoo kwa kuwa sheria ya EWURA hairuhusu kabisa kuuza mafuta kwenye vidumu au ndoo badala yake waunge mkono mchakato wa kufungua kituo cha mafuta katika wilaya ya Nyasa ambacho kitakuwa mkombozi wa wananchi wote’’,alisisitiza Manyanya.

Mwisho

No comments:

Post a Comment