Thursday, June 2, 2016

Toeni habari kwa usahihi wake

Watu watakukumbuka kwa kazi sio elimu wala muonekano wako

NA KWIRINUS MAPUNDA,SONGEA

Katibu mkuu wa wizara ya habari,utamaduni,sanaa na michezo Profesa Elisante Ole Gabriel amewaasa wanahabari nchini  kutoa habari sahihi na kwa usahihi wake ili kuepusha madhara ya upotoshaji wa habari.


Profesa Gabriel ametoa wito huo mjini Songea  katika ziara yake ya  kawaida  ambapo amefanikiwa kufanya kikao na wadau mbalimbali wa habari kutoka katika Halmashauri za Mbinga, Nyasa, amtumbo,Tunduru,Madaba,manispaa ya Songea na Songea vijijini.

Amesema habari inaweza kuwa potofu  lakini ikatolewa vizuri na kwa usahihi na kwamba habari inaweza kuwa sahihi lakini ikashindwa kutolewa vizuri na kwa usahihi hivyo jambo muhimu kwa mwandishi ni kutoa habari sahihi na kwa usahihi wake
hali ambayo itasaidi kuelimisha jamii kutokana na habari kuwa sahihi.

“Sekta ya habari ikifanyika kwa weledi inaweza kuleta mabadiliko chanya kwa watanzania lakini ikitolewa kwa kupotoshwa inaweza kuleta madhara makubwa hata kusababisha kifo,nawaomba wadau wote wa habari fanyeni kazi kwa kufuata taratibu,kusimamia sheria na kanuni zilizopo’’,alisema Profesa Gabriel.

Hata hivyo amewakumbusha wadau wa habari kuacha urasimu katika kutoa habari sahihi kwa wadau  na kusisitiza kuwa jamii itakukumbuka kutokana na mchango ambao uliutoa kabla ya kustaafu na wala sio muonekano wako au elimu ulionayo.

Katika ziara hiyo  katika manispaa ya Songea katibu mkuu ametembelea  maeneo mbalimbali ambayo yapo chini ya wizara yake yakiwemo Makumbusho ya Taifa ya Majimaji ya Songea,kituo cha redio ya Taifa kanda ya kusini Songea pamoja na kituo cha redio binafsi cha Jogoo Fm cha mjini Songea.

Katibu mkuu pia amewakabidhi vifaa vya kisasa vya mawasiliano aina ya IPAD vilivyofadhiliwa na shirika la Startimes, maafisa habari wanne kutoka katika mkoa wa Ruvuma akiwemo afisa habari wa mkoa wa Ruvuma,afisa habari wa manispaa ya Songea,afisa habari wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo na afisa habari wa Halmashauri ya wilaya ya Tunduru.

Katika ziara hiyo ya siku moja katibu mkuu pia amekutana na wadau katika sekta za michezo,sanaa na utamaduni wakiwemo wenyeviti  na makatibu wa vyama vya michezo ngazi ya mkoa.

Katibu mkuu huyo anafanya ziara ya kikazi katika mikoa ya ukanda wa kusini  kwenye mikoa ya Iringa,Njombe,Ruvuma,Lindi na Mtwara  lengo likiwa ni kuipeleka wizara ya habari, utamaduni, sanaa na michezo kwa wadau mikoani.

Mwisho.




No comments:

Post a Comment