Tuesday, May 31, 2016

Tanzania inaongoza kwa ukatili dhidi ya wazee-Utafiti

Mzee kwanza,alikuwa kama wewe,utakuwa kama yeye

Na Albano Midelo

UTAFITI uliofanywa kwa miaka mitatu mfululizo katika nchi mbalimbali Duniani zinaonesha kuwa Tanzania ni miongoni mwa nchi tano zinazoongoza kwa ukatili dhidi ya wazee.
Bibi aliyeamua kujitengenezea jeneza lake

Takwimu zinaonesha kuwa kumekuwa na ukiukwaji mkubwa wa  Haki za binadamu ambapo wazee wamekuwa wahanga wa mauaji na manyanyaso yanayotokana na tuhuma za kishirikina ambapo wazee 2866 wameuawa kwa imani za kishirikina katika mikoa kumi katika kipindi cha miaka mitano iliyopita ikiwa ni wastani wa mauaji ya wazee 573 kila mwaka.


Matokeo ya tafiti tatu zilizofanywa duniani  kuanzia mwaka 2013 hadi 2015 na Shirika la Kimataifa la Help Age International (HAI) ambalo limeendesha utafiti katika nchi zipatazo 96 duniani  kuangalia hali ya usalama wa maisha ya wazee  duniani yanaonesha kuwa Tanzania sio mahali salama pa kuishi wazee.

Utafiti ambao umefanywa na Help Age International katika nchi 91 ambazo shirika hili linafanya kazi ambapo kwa mwaka 2013 nchi ya kwanza kwa usalama wa wazee kuishi Duniani  ilikuwa Sweden na ya pili ni Norway zinaonesha wazi kuwa wazee wa Tanzania wanaishi katika mazingira ambayo sio salama.

Katika utafiti huo Tanzania ilikuwa nchi ya 90  kati ya nchi 91 zilizofanyiwa utafiti huo hali ambayo inathibitisha kuwa Tanzania sio mahali salama kuishi wazee.Katika utafiti huo Nchi ya Afghanistan imetajwa kuwa ni nchi ya mwisho yaani ya 91 kwa usalama wa wazee kuishi,Tanzania ikikamata nafasi ya pili kwa ukatili wa wazee Duniani.

Hata hivyo utafiti huo wa kimataifa kwa Upande wa afya  mwaka 2013 ulionesha kuwa nchi ya Tanzania ilikuwa  ya 73 kati ya nchi 91 takwimu ambazo zinaonesha kuwa angalau kwa upande wa sekta ya afya kwa huduma za wazee kuna maendeleo kidogo.

Kwa mwaka 2014 nchi ya kwanza kwa usalama wa wazee kuishi ilikuwa Norway na ya pili ni Sweden wakati Tanzania ilikuwa nchi ya 92  kati ya nchi 96 zilizofanyiwa utafiti huo.Matokeo ya utafiti huo yanaonesha wazi bado Tanzania sio nchi salama kuishi wazee. Nchi ya Afghanistan katika mwaka 2014 imeendelea kuwa  nchi ya mwisho (96) kwa vitendo vya ukatili dhidi ya wazee Duniani.

 Licha ya Tanzania kuwa katika nafasi mbaya kwa usalama wa kuishi wazee Upande wa afya Tanzania katika utafiti wa mwaka 2014 imeendelea kupanda na kushika nafasi  ya 69 ukilinganisha nafasi ya 73 katika afya mwaka 2013.

Katika utafiti wa  mwaka 2015 nchi ya kwanza kwa usalama wa wazee kuishi ilikuwa Switzerland na ya pili ni Norway   wakati Tanzania ilikuwa nchi ya 91 kwa usalama wa wazee kuishi kati ya nchi 96 zilizofanyiwa utafiti huo.


 Nchi ya Afghanistan  bado imeendelea kushika mkia na kuwa  nchi ya 96 kwa usalama wa wazee kuishi Duniani ambapo Tanzania katika utafiti huo kwa upande wa  Afya imeendelea kuwa nchi ya 69 kati ya nchi 96 Ulimwenguni zilizofanyiwa utafiti huo.

Mkurugenzi mtendaji wa shirika linalohudumia wazee la PADI Isikaka Msigwa anasema kutokana na takwimu hizo Tanzania bado ni nchi ambayo wazee hawatendewi haki ndiyo maana wazee katika baadhi ya mikoa wamekuwa wanauawa kwa visingizio mbalimbali.

“Katika Sekta ya Afya licha ya Tanzania kupanda katika huduma za afya kwa wazee , juhudi zaidi zinahitajika, lakini matokeo chanya  ya juhudi hiyo yameanza kuonekana  ni kutokna na nia dhati ya serikali kutamka kuwa tiba bure kwa wazee wote licha ya changamoto zilizopo za upungufu na wakati mwingine kukosa kabisa dawa’’,alisema Msigwa.

Hata hivyo Msigwa amesisitiza kuwa Tanzania Kimataifa imeonesha  kupiga hatua katika kutoa huduma bora kwa wazee kwa kuzishinda nchi 18 kwa mwaka 2013, nchi 27 kwa mwaka 2014 na nchi 27 kwa mwaka 2015 kati ya nchi zaidi ya 90 zilizofanyiwa utafiti huu.

“Tanzania ili iweze kujiondoa katika nafasi karibu ya mwisho ni lazima serikali itafutie ufumbuzi wa mauaji ya wazee pamoja na kukabiliana na umaskini wa kipato ikiwa ni pamoja na kuanzisha Pensheni kwa wazee wote kunaweza kuipandisha nchi kuwa miongoni mwa nchi zenye mazingira rafiki kwa wazee kama ilivyo kwa nchi za barani Ulaya’’,alisisitiza.

Ameiasa jamii kurudisha upendo kwa wazee hatimaye  kupungua au kumaliza kabisa  kwa mauaji yanayotokana na kutowapenda wazee  kwa baadhi ya familia kutokana na Umasikini wao na kwamba sera ya mzee kwanza inatakiwa kuenezwa kila kona ya Tanzania ili jamii yote iweze kubadilika kifikra na kimtazamo kuhusu wazee.

Kwa Mujibu wa sensa ya watu na makazi ya 2012, Wazee miaka 60 na kuendelea waliopo Tanzania ni asilimia 5.6 ya watanzania wote ambao ni zaidi ya milioni 45  sawa na wazee zaidi ya 2.5 Kati yao 1,307,358 ni wana wake na 1,200,210 wanaume.

Idadi hiyo inakadiriwa kuongezeka na kufikia wazee milioni 8.3 sawa na asilimia 10 ya watanzania wote ifikapo mwaka 2050 na kwamba mwaka 2050 duniani kunakadiriwa kuwa na wazee wengi zaidi kuliko wale vijana wenye umri chini ya 14.

Katika bara la Afrika peke yake inakadiriwa kuwa na wazee zaidi ya milioni 38 kwa sasa na ifikapo mwaka 2050 kunatarajiwa kuwa na wazee zaidi ya milioni 212.
albano.midelo@gmail.com,simu 0784765917

No comments:

Post a Comment