Mito inayomwaga maji imechafuliwa
MADINI ya mkaa wa mawe yaliolundikwa na Kampuni ya TANCOAL katika Kijiji
cha Ndumbi Wilaya ya Nyasa Mkoa wa Ruvuma bado
yanaendelea kuingia ziwa Nyasa hali ambayo inasababisha uchafuzi wa maji
katika ziwa hilo.
Kaimu Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Ndumbi Rajabu Abdallah anasema licha
ya kampuni hiyo binafsi ya uchimbaji madini kuyaweka madini hayo mbali na eneo
la ziwa bado wakati wa mvua za masika chembechembe za madini hayo zinasombwa na
maji kupitia mfereji uliopo jirani na
kuingia hadi ziwa Nyasa.
Abdallah anasisitiza kuwa bado wananchi zaidi ya 2000
wa kijiji hicho wanatumia maji ya ziwa Nyasa licha ya kwamba serikali imeanza mchakato wa kuchimba visima viwili ambavyo bado havijaanza kutumika na wakazi hao wa mwambao mwa ziwa.
wa kijiji hicho wanatumia maji ya ziwa Nyasa licha ya kwamba serikali imeanza mchakato wa kuchimba visima viwili ambavyo bado havijaanza kutumika na wakazi hao wa mwambao mwa ziwa.
Anasema Kampuni hiyo iliahidi kuweka bomba ili wananchi wa Kijiji cha
Ndumbi wasiendelee kutumia maji ya ziwa Nyasa,hata hivyo mchakato wa kuweka
maji ya bomba umeshindikana baada ya
utafiti kubaini vyanzo vya maji vilivyopo havina maji ya kutosha.
Hata hivyo Abdallah anasema serikali ya Kijiji hicho inaendelea kufanya
mawasiliano na uongozi wa Kampuni ya
TANCOAL ambayo imeahidi kuwachimbia visima wananchi ili wasiendelee kutumia maji ya ziwa
Nyasa.
Afisa Mazingira wa Wilaya
ya Mbinga Gordon Nkondora anasema Halmashauri iliuagiza uongozi wa Kampuni ya
TANCOAL kuondoa madini yote ya mkaa wa mawe
katika kijiji cha Ndumbi na kusisitiza kuwa iwapo bado hawajaondoa,wanafanya
makosa kwa kuwa muda waliopewa kuyaondoa ulimalizika na eneo hilo linatakiwa
kuwa wazi.
Kampuni hiyo imekuwa ikitumia bandari ya Ndumbi kusafirishia mkaa wa
mawe kupitia ziwa Nyasa kwenda Malawi,Afrika
ya kusini na bandari ya Itungi iliyopo Kyela mkoani Mbeya tangu kipindi cha
utafiti hadi uchimbaji wa madini hayo.
“Kwa miaka minne mfululizo kuanzia 2011 hadi 2014 maelfu ya tani za mkaa
wa mawe umekuwa unasombwa na maji toka
katika eneo jirani na bandari ya Ndumbi hadi ndani ya ziwa Nyasa…’’,anasema
mwenyekiti mstaafu wa Kijiji cha Ndumbi,
James Mbawala.
Mary Komba,Jeska Haule na Magreth Challe ni wakazi wa Kijiji cha Ndumbi,wanasema
katika kijiji hicho hawana huduma ya maji ya bomba,hivyo wanatumia maji ya ziwa
Nyasa kwa matumizi mbalimbali.
Msimamizi wa Kampuni ya TANCOAL katika bandari ya Ndumbi Deo Mapunda anasema mwaka 2015,Kampuni hiyo iliondoa madini
hayo kutoka kando mwa bandari ya Ndumbi na kuyaweka mbali kidogo na eneo la ziwa ili kukabiliana na mvua za
masika ambazo zimekuwa zinayasomba madini hayo hadi ndani ya ziwa na kuleta
uchafuzi wa maji.
Baadhi ya wavuvi katika Kijiji cha Ndumbi wanasema
kuwa mwaka 2013 kulitokea vifo vya samaki ambavyo wanaamini vilisababishwa na
athari za madini ya mkaa wa mawe kuingia katika ziwa Nyasa kupitia bandari ya
Ndumbi.
Frank Challe mvuvi wa Kijiji cha Ndumbi anasema
samaki wana tabia ya kula takataka zikiwemo chembechembe za madini ya mkaa wa mawe ambazo zinaingia ndani ya ziwa
Nyasa na kwamba anaamini samaki waliokufa waliathirika na sumu za mabaki ya madini hayo.
Fransis Chuwi mvuvi wa Ndumbi anasema
wavuvi walibaini kuwa vifo vya samaki vilivyotokea mwaka 2013 vilianzia ukanda wa Ndumbi ambako maji ya ziwa yalikuwa
yamechafuliwa na madini ya mkaa wa mawe kisha kuenea eneo la Lituhi na maeneo mengine
ya mwambao mwa ziwa Nyasa.
Afisa Uvuvi Tarafa ya
Ruhuhu Wilaya ya Nyasa Joseph Mwingira
anasema utafiti wa awali ulibaini kuwa samaki waliokufa na kuelea juu ya maji walionekana kuwa na
majeraha ya kubabuka katika sehemu za mwili zikiwemo
usoni,tumboni,kichwani,mkiani na mgongoni.
Hata hivyo Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi
ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) Dk.Benjamin Ngatunga alipinga madai ya wavuvi hao kwamba vumbi na
chembechembe za madini ya mkaa wa mawe husababisha vifo vya samaki.
Dk.Ngatunga alisisitiza kuwa wavuvi
wanaongea jambo ambalo halijafanyiwa utafiti wa kisayansi ambao TAFIRI
imechunguza katika nchi mbili za Tanzania na Malawi na kubaini tatizo la vifo
vya samaki katika ziwa Nyasa ni mabadiliko ya mkondo wa maji katika ziwa hilo
ambayo hujitokeza kila baada ya miaka kadhaa na sio vinginevyo.
Afisa wa Maji wa Bonde la Ziwa Nyasa Mhaidrojia Witgal Nkondora anasema
ziwa Nyasa linapokea tope, udongo na mchanga kutoka katika mito iliyochafuliwa
na shughuli za kibinadamu na kusababisha uchafuzi wa mazingira kwa viumbe waliomo
kwenye mito na ziwa hilo.
Utafiti umebaini aina mbalimbali za Samaki katika mto Ruhuhu na ziwa Nyasa wameanza kupungua kwa kuwa samaki
hawezi kutaga mayai na kuzaliana kwenye tope
au maji yaliochafuliwa na kemikali za madini yenye sumu.
Kwa mujibu wa Afisa huyo,utafiti uliofanyika mwaka 2007 katika mto
Songwe, unaonesha kuwa zaidi ya tani 700,000 za mchanga,udongo na tope
zilisombwa na kuingia katika ziwa Nyasa hali ambayo inatishia usalama wa ziwa
hilo.
“Ninaamini mwaka huu utafiti
mwingine ukifanyika katika mito inayomwaga maji ziwa Nyasa ukiwemo mto
Ruhuhu huenda mchanga na udongo ulioingia katika ziwa Nyasa utafikia mamilioni
ya tani,ikumbukwe utafiti wa awali ulifanyika katika mto mmoja tu bado hatujui
katika mito mingine mikubwa zaidi ya minane inayoingiza maji katika ziwa hilo
”,anasisitiza Nkondora.
Nkondora anaitaja mito
mitano inayoongoza kwa kusomba taka
zenye sumu,mchanga na tope na kumwaga ndani ya Ziwa Nyasa kuwa ni mto
Ruhuhu wenye ukubwa wa mita za mraba13,490,mto Songwe mita 3,550, mto Rufirio mita1,350, mto Kiwira mita 1,660 na mto
Lumbira mita 1,414.
“Mto Chiwindi uliopo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji ndiyo unaoongoza
kwa kuingiza takataka zenye sumu katika ziwa Nyasa kutokana na uchimbaji wa
madini hasa dhahabu ambao unaendelea kufanywa kwenye maeneo ya wilaya za Nyasa
na Mbinga’’,anasema Nkondora.
Kulingana na Nkondora, mto Ruhuhu ambao chanzo chake ni mkoa wa Ruvuma
na Njombe umechafuliwa katika kiwango
cha kutisha na maji yake yanaonekana
kuwa na tope kwa mwaka mzima kutokana na shughuli za kibinadamu.
Anabainisha uchafuzi wa maji ya mito na ziwa umechangia kuharibu mazalia
ya samaki,kuua viumbehai wa majini na
baadhi ya aina za samaki wameanza kutoweka.
Ili kuvitunza na kuvilinda vyanzo vya maji,Nkondora anashauri Baraza la
Taifa la Kusimamia Mazingira(NEMC) kutumia sheria mama ya mazingira kukabiliana
na Wachimbaji madini wanaozalisha taka
kwenye maji na kutumia kemikali za sumu kusafishia madini.
Julai 28,2010,Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa ulitoa
mkataba ambao ulitamka wazi kwa nchi wanachama ikiwemo Tanzania kuhakikisha
inatoa maji safi na salama katika kiwango cha juu kwa wananchi wake ili kulinda
afya za watu wake.
Mwanasheria na Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wanasheria Watetezi wa Mazingira
Tanzania (LEAT) Dk.Nshala Rugemeleza anasema sheria mama ya mazingira ya mwaka
2004 kifungu cha 21 inaonesha wazi
miradi yote mikubwa inatakiwa kufanyiwa tathmini ya mazingira (EIA) ili
kukabiliana na athari za kimazingira.
Hata hivyo Dk.Nshala anasema utafiti umebaini katika maeneo mengi
kampuni za uwekezaji zinashindwa kuzishirikisha serikali za vijiji katika hatua
zote za tathmini ya mazingira, utafutaji na uchimbaji wa rasilimali kama
madini,gesi na mafuta ambapo kisheria wanafanya makosa.
“Sheria inasema wazi wawekezaji hawaruhusiwi kuingia katika eneo la
kijiji hata kama wamepewa leseni na wizara, bila kibali cha serikali ya kijiji
husika,mwenyekiti wa serikali ya kijiji anatakiwa kutoa ruhusu kwa kampuni au mwekezaji kwa niaba ya
wanajiji’’,anasisitiza Dk.Nshala.
Anazitaja sheria ambazo zinampa uwezo Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji
kutoa kibali kwa mwekezaji anapofika kutafuta,kuchimba au kuwekeza kuwa ni
sheria ya madini ya mwaka 2010,sheria ya serikali za mitaa na mamlaka ya wilaya
sura ya 287 na sheria ya ardhi namba nne na tano ya mwaka 1999.

No comments:
Post a Comment