Waziri wa nchi ofisi ya makamu wa Rais mazingira Dk.Terezya Luoga Huvisa akiwa mstari wa mbele katika operesheni ya kusitukiza ya kuwaondoa wafanyabiashara ndogo ndogo maarufu kama wamachinga ambao wamejaza bidhaa zao kila upande kando kando ya barabara kuu ya Sokoine mjini Songea na kusababisha barabara kuwa finyu hivyo kuhatarisha maisha ya watembea kwa miguu pia ni uchafuzi wa mazingira.
Na Albano Midelo.
WAZIRI wa nchi ofisi ya makamu wa Rais Mazingira Dk.Terezya Luoga Huvisa ameendesha operesheni kabambe ya kusafisha mji wa Songea kwa kuwaondoa wafanyabiashara ndogo ndogo yaani wamachinga katika barabara kuu ya Sokoine ya mjini hapa.
Waziri Dk.Huvisa Jumapili amefanya ziara ya kushitukiza katika barabara kuu ya Sokoine ambayo ndiyo kioo cha mji wa Songea ambayo alikuta kila upande wamejaa wamachinga ambao walitandaza bidhaa zao hadi hifadhi ya barabara kuu na kuhatarisha maisha ya wananchi pamoja na kuleta kero kubwa kwa watumiaji wa barabara hiyo mjini Songea.
Kutokana na hali hiyo waziri huyo akiwa ameongozana na mstahiki Meya wa manispaa ya Songea Ally Manya,mkurugenzi wa manispaa hiyo,pamoja na mwakilishi wa mkuu wa mkoa wa Ruvuma walianza operesheni kabambe iliyodumu kwa dakika 80 ya kuwasimamia wafanyabiashara hao kuondoa bidhaa zao zote walizopanga barabarani.
“Nakuagiza mkurugenzi wa manispaa ya Songea kwa kushirikiana na mstahiki meya hakikisheni kuanzia kesho meza zote za biashara ziondolewe pia hakikisheni kuwa wafanyabiashara hawa harudi tena kufanya biashara kando kando ya barabara kuu kwa kuwa licha ya kuwa hatari katika maisha lakini pia ni uchafuzi wa mazingira,waelekezeni waende sehemu ambazo zimeandaliwa rasmi kwa ajili yao”,alisisitiza.
Picha wafanyabiashara ndogo ndogo wakiondoa bidhaa zao ambazo wamezipanga chini katika barabara kuu ya Sokoine mjini Songea picha na Albano Midelo
Hata hivyo waziri huyo anayeshughulikia mazingira ambaye pia ni mwenyeji wa Songea, anabainisha kuwa zoezi la kuwaondoa wafanyabiashara wadogo wadogo kando kando mwa barabara kuu linafanyika katika nchi nzima hivyo amewaagiza wakurugenzi kusimamia usafi wa mazingira ili kuboresha mandhari ya miji yote nchini .
“Mstahiki meya pamoja na Baraza zima la madiwani simamieni sheria za barabarani kuwabana wote ambao wataendelea kufanyabiashara katika barabara kuu hii ili wananchi wanaotumia wasiwe hatarini kwa kuwa wanaweza kugongwa na vyombo vya moto,serikali inapenda wananchi wafanye biashara lakini katika maeneo yaliotengwa,tunafanya hivi kwa nia njema kabisa”,anasema.
Mstahiki Meya wa manispaa ya Songea Ally Manya ameahidi kusimamia suala hilo pamoja na usafi wa mazingira katika mji wa Songea ili mji huo uweze kurudi katika sifa ya kuongoza kwa usafi kitaifa pamoja na kuhakikisha kuwa afya za wananchi wa mji huo zinakuwa salama bila kupata magonjwa ya kuambukiza kama kipindupindu kutokana na uchafu uliokithiri.
Baadhi ya wananchi waliozungumza na mwandishi wa habari hizi wamempongeza waziri huyo wa mazingira kwa hatua ambazo amezichukua kuusafisha mji wa Songea ambapo kwa kuanzia amewaondoa wafanyabiashara wa barabarani ambao walikuwa wametanda barabara kuu ya Sokoine mjini hapa wakifanyabiashara zao bila kuchukuliwa hatua zozote.
Hata hivyo wananchi hao Mhamed Kudeka,John Mapunda na Ezabela Komba wametoa ombi kwa waziri huyo kutoa agizo la kuyaondoa pia magari makubwa na madogo ambayo yamekuwa yakiegeshwa kila siku katika barabara kuu hiyo na kuhatarisha maisha ya wananchi .
Mwenyekiti wa Chama cha wafanyabiashara wenye viwanda na kilimo TCCI mkoani Ruvuma Mays Mkwembe alisema kuwa mji wa Songea una pikipiki zaidi ya 4000 ambazo zinatumia katika barabara kuu hiyo hali ambayo imesababisha wananchi kugongwa na wengine kupoteza maisha kutokana na ufinyu wa barabara unaochangiwa na magari kuegeshwa kando kando hivyo ameshauri wahusika kuchukua hatua za kumuunga mkono waziri wa mazingira kwa kuyaondoa magari hayo na kwenda kuyaegesha katika maeneo maalum kisheria.
Naye Joseph Mbano mkazi wa mjini hapa alimwomba waziri huyo wa mazingira kutembelea katika stendi kuu ya mabasi ya Songea ambayo walidai kuwa haina hadhi ya kuwa stendi ya mkoa ambapo hivi sasa katika maeneo ya kuegesha mabasi wamejitokeza wafanyabiashara ndogo ndogo ambao wamekuwa wakiweka bidhaa zao kama samaki chini hali ambayo inataharisha afya kutokana na mazingira machafu kwa kuwa vumbi za magari yanayoingia katika stendi hiyo zinaishia kwenye vyakula hivyo ambavyo vinaliwa na walaji na kuhatarisha afya zao.
Baruapepe amidelo@yahoo.com
Simu 0766463129
No comments:
Post a Comment