Monday, April 25, 2011

Askofu mkuu Mtega avitahadharisha vyombo vinavyosimamia haki


Askofu mkuu wa jimbo kuu katoliki la Songea mhashamu Dkt.Norbert Mtega picha na Albano Midelo
Na Albano Midelo,Songea.
 ASKOFU mkuu wa jimbo kuu katoliki la Songea  mhashamu Norbert Mtega ametoa rai vyombo ambavyo vinasimamia sheria kutenda haki  kwa watu wote ili ipatikane  haki na amani ya kweli alioicha Yesu Kristu  baada ya mateso, kifo na ufufuko wake.

Askofu mkuu Mtega alitoa rai hiyo  wakati anahubiri  kwa nyakati tofauti katika kanisa kuu la kiaskofu la mtakatifu Mathias Kalemba la mjini hapa pamoja na kanisa la parokia ya Bombambili jimbo kuu la Songea.

Mhashamu Mtega alibainisha kuwa misingi ya sheria isipofuatwa kikamilifu na vyombo vinavyotoa haki kama mahakama  vinaweza kuumiza jamii kwa kuwa haki itashindwa kupatikana matokea yake amani inaweza kuvunjika na kusababisha migogoro katika jamii.

“ Amani haiwezi kuwepo endapo haki haiwezi kutendeka ,natoa wito kwa wenye mamlaka na  vyombo vya haki  viache kupindisha sheria‘pasiwepo na upendeleo kwa sababu ya ukabila,kufahamiana,uwezo wa mtu,rangi ya mtu au kwa namna yeyote ile ,Yesu kristo alihukumiwa adhabu ya kifo bila ya kuwa na hatia yeyote ,Yesu alikuwa hana mtetezi yeyote,hata hivyo alishinda mauti na kutuletea amani ya kweli”,alisisitiza. 

Aliongeza kuwa sheria zimewekwa kwa ajili ya kutenda haki bila upendeleo pamoja na kupatikana kwa ulinzi kwa watu wote pamoja na mali zao,hivyo ametaka vyombo vyote vinavyosimamia haki na sheria kutimiza wajibu wao bila upendeleo ili viweze kuaminika katika jamii.

Waumini wakifuatilia adhimisho la misa takatifu siku ya sikukuu ya Pasaka kwenye kanisa kuu la kiaskofu la jimbo kuu la Songea.

Hata hivyo Askofu mkuu Mtega amewaasa waumini kuwaombea viongozi waliopo madarakani hivi sasa ili waweze kuliongoza Taifa katika misingi ya umoja,amani,utulivu na haki pamoja na  kuviombea vyombo vya sheria  ili viweze kutenda haki katika jamii inayowazunguka.

Askofu  mkuu  Mtega amerudia wito wake kwa watanzania kuhusu mchakato wa katiba mpya ambayo inatakiwa kuandikwa nchini ambapo ametahadharisha kuwa katiba iwe ile ambayo Mungu ataonekana ndani yake na itakayowanufaisha watanzania wote .

“ Tumeshuhudia yaliotokea Bungeni Dodoma hivi karibuni,ndugu zangu hivi sasa tunalilia kuandikwa katiba mpya ,lakini tunataka katiba ambayo ndani yake Mungu ataonekana ili tuunde taifa ambalo linatembea na Mungu, tunapofikisha ya jubilei miaka 50 ya uhuru wa Taifa letu hapo Desemba 9,2011 ni vema tuzaliwe upya ”anasema.

Alibainisha zaidi kuwa Taifa linapotimiza Jubilei ya miaka 50 linatakiwa kuzaliwa upya  kwa kuandikwa katiba ambayo itatenda   haki kwa watanzania wote,vyama vyote vya siasa ,rasilimali za taifa kama vile madini na maliasili zote ziwanufaishe watanzania wote na pasiwepo upendeleo wa aina yeyote.

                          








               

No comments:

Post a Comment