Na Albano Midelo,Natumbo
ASKOFU mstaafu wa jimbo la Bukoba Mhashamu Gervas Nkalanga amevunja rekodi kwa maaskofu wa kanisa katoliki nchini baada ya kuwa Askofu pekee kuadhimisha jubilee ya miaka 50 ya uaskofu akiwa hai.
Askofu Nkalanga ameadhimisha jubilee ya miaka 50 katika Abasia ya Hanga jimbo kuu katoliki ya Songea Juni 7 mwaka huu ambapo mgeni rasmi alikuwa ni Rais mstaafu wa awamu ya tatu Benjamin Mkapa.
Rais wa Baraza la maaskofu katoliki Tanzania TEC mhashamu Yuda Thadei Ruwaichi akitoa salamu za Baraza hilo kwenye jubilee hiyo iliyohudhuriwa na maaskofu karibu wote wa kanisa katoliki nchini alisema askofu mstaafu Nkalanga mwenye umri wa miaka 92 anakuwa ni askofu wa kwanza nchini kufanya jubilee ya miaka 50 akiwa hai.
Rais huyo alibainisha kuwa TEC inatambua mchango mkubwa ambao ulifanywa na Askofu mstaafu Nkaranga katika kipindi chake chote cha uaskofu akiwa madarakani na baada ya kustaafu na kutoa rai kwa maaskofu wengine kuiga mema yote ya askofu huyo.
Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo Rais Mstaafu wa awamu ya tatu Benjamin Mkapa akizungumza kwenye maadhimisho hayo alimpongeza Askofu mstaafu Gervas Nkaranga kwa kufanya jubilee ya miaka 50 akiwa hai na kusisitiza kuwa ni jambo jema mtu kupongezwa akiwa hai kwa kuwa imezoelea watu wengi wanasifiwa baada ya kufa.
Rais mstaafu Mkapa ambaye anajiita kuwa ni mseminari mshindwa kutokana na ukweli kuwa alisoma katika seminari ya Kigonsera wilayani Mbinga,alikiri kuwa nafasi zote ambazo amepewa hapa nchini zimetokana na malezi mazuri ya kiroho na kimwili ambayo alipewa na shirika la watawa wabenedikitini akiwa Kigonsera na Ndanda chini ya kanisa katoliki jimbo kuu la Songea.
“Shirika la wabenedikitini siku zote wanazingatia kauli mbiu yao ya sala na kazi,bila kazi hakuna maisha wala heshima, vijana wetu siku hizi hawataki kufanyakazi wanataka kufanyiwa kazi na sisi wazee tusisahau sala na kazi”,alisisitiza Rais mstaafu Mkapa.
Hata hivyo Rais mstaafu mkapa alisema watu wengi wanapenda kuonekana kwa jamii pale wanapofanya mambo mbalimbali ambapo alibainisha kuwa Askofu mstaafu Nkalanga kuacha jimbo lake la Bukoba na kuamua kuishi katika Abasia ya Hanga jimbo kuu la Songea ni jambo la kupongezwa.
“Mimi binafsi hivi sasa sipendi kuoneka onekana ndiyo maana hata mliponialika kuja kuwa mgeni rasmi katika jubilee hii nilitafakari sana na nilisita,kwa kweli nimeguswa sana na ucha Mungu na uongozi wa Askofu mstaafu Nkalanga naomba mwenyezi Mungu amzidishie maisha marefu Askofu mstaafu Nkalanga”,alisisitiza Mkapa.
No comments:
Post a Comment