Baadhi ya wakazi wa mji wa Songea mkoani Ruvuma wakimiminika kwenye uwanja wa michezo wa Majimaji kuangalia banda la wizara ya maliasili na utalii ambalo lilikuwa limewekwa mnyama aina ya mamba ili kumtazama mnyama huyo aliyewavutia wengi waliomuona.
Na Albano Midelo.Nimewahi kuishi mwambao mwa ziwa Nyasa kwa takribani miaka minne wakati nasoma katika shule moja ya Sekondari inayoitwa shule ya mtakatifu Paulo iliyopo katika mji mdogo wa Liuli ziwa Nyasa.Nikiwa nasoma katika shule hiyo nimewahi kushuhudia matukio kadhaa ya mamba kukamata watu ndani ya ziwa Nyasa hali ambayo ilinifanya kumuogapa sana mnyama huyu.
Kwa kweli kwa miaka minne ambayo niliishi Nyasa sijawahi kuoga katika ziwa Nyasa kuhofia kukamatwa na mamba.Mamba katika ziwa Nyasa walidiriki kuwakamata raia wa kigeni yaani wazungu ambao walikuwa wanafanya uvuvi wa samaki wa mapambo katika ziwa hilo ,licha ya uvumi ambao ulikuwa umeenea awali kwamba mamba hawezi kukamata mzungu.
Kutokana na mamba wala watu katika eneo la Liuli kuwa kero ,walijitokeza wanaharakati ambao waliamua kutafuta mbinu za kukabiliana na mamba hao ambao walianza kurudisha nyuma shughuli za kiuchumi ndani ya ziwa Nyasa pamoja na wawekezaji kuanza kuogopa.
Miongoni mwa wazee ambao walijitokeza kupambana na mamba ni mzee mstaafu wa jeshi la wanaunchi wa Tanzania JWTZ ambaye kutokana na uhodari wake katika vita dhidi ya mamba wananchi wa mwambao mwa ziwa Nyasa waliamua kumpa jina la Mrema ambaye alifanikiwa kuangamiza mamba wapatao 640 baada ya kuwatega kwa kutumia ndoani maalum.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mzee Mrema ambaye hivi sasa ni marehemu ,alisema alifanikiwa katika vita hivyo kwa kumuomba mwen yezi Mungu kabla ya kuanza kuwatega mamba hao,ambao ilidaiwa walikuwa ni mamba wa watu ambao walikuwa wanatumika katika mambo ya kishirikina na kwamba alifanikiwa kuwamaliza kwa kuwatega kwa ndoana maalum iliyowekwa nyama ya mbwa.
“Nyama ya mbwa ni chakula ambacho mamba anakipenda sana,mkiwa wawili binadamu na mamba majini,mamba anaanza kumkata kwanza mbwa,hivyo mimi nilifanikiwa kuwanasa mamba wengi kwa kutumia nyama ya mbwa na kufanya idadi ambao niliwauwa walifikia 640 na tatizo la mamba wala watu ziwa Nyasa likabakia kuwa ni historia,ingawa hivi nimeanza kusikia wameanza kuonekana lakini hawajawahi kukamata tena mtu”,alidai mzee Mrema.
Katika sherehe za siku ya mazingira duniani ambazo kitaifa zimefanyika mkoani Ruvuma wizara ya maliasili na utalii katika mabanda yao ya maonyesho kulikuwa na vivutio vingi vya wanyama,lakini kubwa ambalo wakazi wa mji wa Songea walivutika ni kwenda kumuangalia mamba katika banda la mamba ambaye aliwavutia wengi ingawa pia kulikuwa na wanyama wengine kama nyungunyungu,nyani,ngozi za wanyama mbalimbali na mafuvu ya wanyama kama vile tembo.
Metson Mwakanyamale ni mkuu wa kikosi cha kuzuia ujangili kanda ya kusini ambaye alizitaja faida za mamba kuwa ni pamoja na utalii,chakula na mazao yake kama vile mayai na ngozi vina thamani kubwa kutokana kutumika kutengenezea mikanda,mabegi na viatu.
“Nyama ya mamba ni chakula ambacho kinapendwa na watu wengi ,baadhi ya makabila hapa nchini yanapenda kula nyama ya mamba,hata hivyo katika ulimwengu nchi ambayo inaongoza kwa ulaji wa nyama ya mamba ni Ujerumani,wageni ambao wanatoka katika nchi ambazo hazina mamba wananunua mayai na kwenda kutotoresha ili kupata mamba na kukuza utalii katika nchi zao”,anasisitiza Mwakanyamale.
Pamoja na faida ambazo zinatokana na mamba ,Mwakanyamale anayataja madhara ya mamba kuwa ni pamoja na mamba kuwa ni miongoni mwa wanyama hatari kwa binadamu na mifugo iwapo atapatikana mahali ambako sio hifadhi ya Taifa au majini.
Kutokana na hali hiyo Mwakanyamale anasema serikali kupitia wizara ya maliasili na utalii inafanya doria katika maeneo yaliotengwa na hasa majini ili kuhakikisha kuwa mamba hawaleti madhara ambapo ametahadharisha kuwa hairuhusiwi kuwauwa au kuwamiliki mazao ya wanyamapori kama vile ngozi na pembe bila kibali toka serikalini.
Baruapepe amidelo@yahoo.com
No comments:
Post a Comment