Na
Albano Midelo
WAKAZI wa kijiji cha
Lipokela wilayani Songea mkoani Ruvuma
wanamuomba waziri wa ardhi,nyumba na maendeleo ya makazi Profesa Anna Tibaijuka kuwasaidia kuirejea
ardhi yao eneo la Luchili yenye ekari 4000
inayodaiwa kupewa mwekezaji.
Wakizungumza na mwandishi
wa habari katika kijiji hicho baadhi ya wananchi walidai kuwa mwekezaji mwenye asili ya Asia Khalim Meraly tangu mwaka 1985 alipewa ardhi kinyemela bila
Baraka za wananchi na kusababisha ardhi hiyo kuingia kwenye mgogoro mkubwa.
Hata hivyo walikiri
kuwa mwekezaji huyo alipewa ardhi kwa
maamuzi ya wananchi yenye ukubwa wa eka 1000 tu mwaka 1984 na kwamba mwaka 1985
aliomba tena ardhi eka zaidi ya 4000 ambazo alipewa bila Baraka za wananchi na
kuleta mgogoro ambao unaendelea hadi sasa.
``Kuanzia mwaka 1985
wananchi wa kijiji cha Lipokela hawakujua kama ardhi yao ya ekari 4000 amepewa
mwekezaji hadi mwaka jana takriban miaka
25 ndipo ilipofahamika na kusababisha wananchi zaidi ya 200 wanaolima mashamba
pamoja na makazi kwenye eneo hilo kuambiwa kuwa eneo hilo ni mali ya mwekezaji ’’,walidai
wananchi hao.
Komba alisema
mwekezaji alipewa kisheria eka 1000 tu
upande wa kulia mwa barabara ya Songea - Mbinga na kwamba eneo lenye ekari
zaidi ya 4000 upande wa kushoto ambazo mwekezaji huyo anadai kupewa sio zake
kwa kuwa ni mali ya wananchi ambazo walipewa kihalali na serikali ya kijiji.
Wananchi wakiwemo
Gofrey Lupindu,Agustino Komba,Filbert Kinunda, Vestina Hyera, Bomba
Nchimbi wakizungumza kwa uchungu ,wanadai msimu huu hawana mashamba ya kulima
baada ya kuzuiwa kuendelea kulima katika mashamba yao na kwamba hivi sasa
hawana imani na mwenyekiti wa kijiji aliyopo madarakani John Nchimbi ambaye
anadaiwa kumsaidia mwekezaji badala ya kuwasaidia wananchi waliomweka
madarakani.
Mwenyekiti wa kijiji
hicho Nchimbi amekanusha kumsaidia mwekezaji bali amesema amepewa ekari hizo chini ya mihutasari halali ambayo walikaa
viongozi waliomtangulia na kusisitiza kuwa viongozi waliomtangulia ndiyo wenye
makosa kwa kuwa waliendelea kuwagawia wananchi mashamba wakitambua kuwa eneo
hilo ni mali halali ya mwekezaji.
“Wenyeviti wa
serikali za vijiji waliotapeli wananchi ardhi
wakiwa madarakani Faustine Komba, Regnad Komba,John Lupindu,Anton Komba
na Joseph Komba ambaye alikuwa mwenyekiti wa kwanza wa kijiji cha Lipokela
ndiye aliyeidhinisha wakati Meraly anapewa ardhi’’,anadai Nchimbi.
Muhtasari wa kwanza
unaonesha kuwa Mei 10,1984 ulifanyika
mkutano wa kijiji wenye wajumbe 25 waliokubali ombi la mwekezaji Meraly kupewa ekari 1000 na muhtasari wa pili
unaonesha kuwa ulifanyika mkutano wa Halmashauri ya kijiji cha Lipokela Marchi
26,1985 wenye wajumbe 24 ambao walikubali
maombi ya nyongeza ya ekari 4000 kwa mwekezaji ili kufikia ekari 5000
ambazo ndiyo mahitaji yake .
Hata hivyo afisa
mtendaji wa kijiji cha Lipokela Sabinus Nyoni
Oktoba 17 mwaka jana aliwaandikia barua yenye kumb.Nolvc/ARDH wanakijiji
wapatao 200 wanaoishi katika eneo la Luchiri
kusimamisha kufanya shughuli za kilimo katika eneo la Luchiri ambako
anadai ni eneo la mwekezaji Meraly ambaye anatumia jina la Southern Farm Ltd.
Katika barua hiyo
Nyoni aliwakumbusha wakulima hao kuwa eneo hilo ni mali ya Southern Farm Ltd na
kwamba lina hatimiliki ya kisheria yenye shamba namba 40 na kwamba kwa serikali itamtuma mtaalam wa kuthamini
shughuli zilizofanyika kwa miaka 23 ili wananchi wapate fidia.
“Endapo mwananchi
yeyote atakiuka na kuendelea kufanya kazi kwenye eneo hilo atachukuliwa hatua
kali za kisheria kwa kuwa atakuwa ni mvamizi wa eneo la Southern Farm Ltd na
atakuwa amekosa fidia ambayo alistahili kupata’’,anasisitiza Nyoni katika barua
yake ambayo nakala amepewa mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya
Songea.
Kwa upande wao wakazi
wa eneo hilo baada ya kupata barua ya afisa mtendaji walijibu barua hiyo kwa
kupinga amri ya kusimama kufanyakazi za kilimo katika eneo hilo kwa madai ya
kutotambua uhalali wa kupata eneo ambalo wao wamelitumia kwa zaidi ya miaka 18
na kwamba eneo hilo wamepewa na kijiji kisheria tangu mwaka 1993.
“Eneo hili
hatukuvamia,tulipewa kwa kutekeleza hatua zote za maombi katika serikali ya
kijiji,tulipewa kwa kujadiliwa na kupimiwa,wananchi tunatambua suala hili lipo
ngazi za juu, tumeshindwa kulima hadi sasa hatujui familia zetu mwaka huu
tutaishi vipi bila kuwa na chakula’’,wanadai wananchi hao.
Juma Thomas ni wakili
wa kujitegemea anasema sheria inasema mtu akitumia ardhi ambayo sio mali yake
kwa miaka zaidi ya 12 ,mtumiaji ana haki ya kumilikishwa hivyo kwa kuwa
wananchi hao wametumia ardhi hiyo kwa miaka 18 wana haki ya kumilikishwa
kisheria.
Mwekezaji wa Southern Farm Company ana hati ya kumiliki eneo hilo shamba namba
40 iliyotolewa Februari 25,1988,lakini nao wananchi wanazo hati na risiti ambazo wamelipia katika
serikali ya kijiji cha Lipokela kuanzia mwaka 1993 hadi wanapoambiwa kuwa eneo
ni la mwekezaji.
Mwekezaji Bwana
Meraly kwa upande wake kuanzia msimu huu tayari ameanza kuendeleza shamba lake ekari 1000 kwa kuanzisha shamba
kubwa la kahawa ambalo amepanda miche
laki tano ya kahawa.
Meneja wa shamba hilo
Ally Said akizungumza kwa niaba ya mwekezaji wa Southern Farm anasema shamba
hilo litatoa ajira kwa watu 6000 na
kwamba tayari watanzania 600 wamepata
ajira kwenye shamba hilo.
“Mwekezaji amepania
kufanya mapinduzi ya kilimo cha kahawa anawatumia wataalamu wa kilimo cha umwagiliaji
wa matone kutoka nchini Israel na Somalia lengo likiwa ni kuwekeza kwa miaka
100’’,anasisitiza.
Afisa wa ardhi wa
Halmashauri ya wilaya ya Songea Japhet Mungashwa amekiri kwamba mwekezaji huyo amemilikishwa eneo la eka 5000
kihalali kwa kipindi cha miaka 99 kwa sheria ya ardhi ya mwaka 1923 ambayo
inawaruhusu wajumbe wa kijiji kupitisha maamuzi bila kushirikisha maamuzi ya
wananchi wote kama ilivyo katika sheria mpya ya ardhi ya mwaka 1999.
Sheria ya ardhi ya
vijiji namba tano kifungu cha tano ya
mwaka 1999 inasema kuwa Halmashauri ya kijiji haitagawa ardhi au kutoa
hakimiliki ya kimila bila ya kwanza kupata idhini ya mkutano wa kijiji ambapo katika kifungu cha sita
katika sheria hiyo kinaeleza Halmashauri
ya kijiji italazimika kutoa taarifa na kuzingatia maoni ya mkutano wa kijiji
kuhusu uendeshaji na usimamizi wa ardhi ya kijiji.
albano.midelo@gmail.com,simu
0766463129

No comments:
Post a Comment