Na Albano Midelo
Takwimu zinaonesha uvuvi usiokuwa endelevu
unaofanywa kwenye ziwa Victoria umesababisha kutoweka kwa aina 300 za samaki
waliokuwa wanapatikana mwanzoni mwa miaka ya 1960 hadi 1970.
Uvuvi usiokuwa endelevu unafanyika pia
katika ziwa Nyasa pamoja na uchafuzi wa mito inayoingia kwenye ziwa hilo na
kusababisha samaki waliokuwepo katika ziwa hilo kuendelea kutoweka na kwamba
endapo hatua za makusudi hazitachukuliwa na wadau hususani wizara ya maliasili
na utalii kuna hatari samaki wa aina mbalimbali wakatoweka.
Ziwa Nyasa limezungukwa na nchi tatu ambazo
ni Tanzania,Malawi na Msumbuji.Ziwa hilo lipo kwenye usawa wa meta 500 toka
usawa wa bahari ambapo kina cha ziwa hilo ni karibu meta 750,urefu wake ni
karibu kilometa 1000 na upana mkubwa ni
kilometa 80 ambapo upana mdogo ni kilometa 15.
Kutoweka kwa baadhi ya samaki katika ziwa
Nyasa kumesababisha baadhi ya samaki kutopatikana kwa urahisi hali ambayo
imesababisha bei za samaki wanaovuliwa katika ziwa hilo kuuzwa kwa bei mbaya na hivyo wananchi
wengi kushindwa kumudu kununua kitoweo hicho.
Ukitembelea kwenye mapitio ya mto Ruhuhu ambao unamwaga maji yake ziwa
Nyasa utabaini uvuvi ambao hauruhusiwi kisheria ukiendelea kufanya jambo ambalo
watalaamu wanasema kumechangia kutoweka kwa samaki kwenye mto Ruhuhu na ziwa
Nyasa.
Mto Ruhuhu umechafuliwa na maji yake
yanaonekana kuwa na tope kwa mwaka mzima kutokana na shughuli za kilimo na
uchimbaji wa madini ambao ufanywa na wakazi ambao wanaishi kando kando mwa mto
huo unaoanzia kwenye milima ya Matogoro wilayani Songea.
Mtendaji
wa kata ya Lituhi wilayani Nyasa Joseph Chawala anasema hadi kufikia miaka ya
2000 maji ya mto Ruhuhu yalikuwa hayajachafuliwa ambapo samaki wa aina mbalimbali
hasa mbasa na mbelele walipatikana kwa wingi lakini hivi sasa samaki wametoweka
na mto ni mchafu kwa mwaka mzima.
Anabainisha zaidi kuwa kilimo na usafishaji
wa udongo wa madini aina ya dhahabu kwa
kutumia zebaki kumechangia kuharibu mazialia ya samaki na hata samaki kuhama
kwa kuwa maji ya mto huo hivi sasa radha yake imebadilika na yanatoa harufu
mbaya kwa viumbe hai kama samaki.
“Hivi sasa wavuvi wanaweza kukesha kwenye
mto Ruhuhu na wasiambulie samaki hata mmoja hali ni mbaya,jambo la hatari zaidi
ni kwamba wavuvi wanavua kwenye maingilio ya mto Ruhuhu na ziwa Nyasa sehemu
ambayo kisheria hairuhusiwi kufanya
uvuvui kwa kuwa ni mazalio ya samaki hivyo wanaharibu mazalia ya
samaki’’,anasisitiza.
Chawala anabainisha kuwa uchafuzi huo wa mto Ruhuhu umeleta athari
kubwa kwa wakazi wa kata ya Lituhi yenye vijiji vya
Lituhi, Ngingama, Nkaya,Litumbakuhamba,Kihuru na Mwelampya ambapo zaidi ya watu
12,000 wanaathirika na hali hiyo kwa kuwa wanaishi kwa kutegemea uvuvi.
John Mpangala mkazi wa Liuli anasema kwa miaka mingi
walizoea kupata samaki aina ya mbasa na mbelele kutoka mto Ruhuhu lakini hivi
sasa hakuna samaki wa aina hiyo na kusisitiza kuwa watu wa mwambao wamezoea kula samaki kwa
ugali wa mhogo hivyo kutokana na kupungua kwa samaki inawawia vigumu kupata
kitoweo.
Mvuvi Martin Challe wa kijiji cha Lituhi
anadai miaka ya nyuma samaki katika mto Ruhuhu na ziwa Nyasa walikuwa wanapatikana kirahisi tofauti kubwa
na hali ya hivi sasa ambapo wavuvi wanakesha usiku kucha hadi asubuhi na
kuambulia samaki wachache sana au wakati mwingine wanakosa kabisa samaki.
“Bei
ya samaki aina ya mbasa,kambale,mbelele na ngumbo haikamatiki kutokana na
kuuzwa samaki mmoja kati 10,000 hadi 15,000,kwa kweli aina hizo za samaki wanaoweza
kula ni watu wenye uwezo tu hivyo kufanya maisha katika mwambao mwa ziwa Nyasa
kuwa magumu’,alisisitiza Mary Haule mkazi wa Lituhi.
“Huku mwambao mwa ziwa Nyasa hakuna mifugo
mingi kama ilivyo katika maeneo mengine nchini,sisi tegemeo letu kubwa ni
samaki wa ziwa Nyasa hivyo hali hii ya kutoweka kwa samaki au samaki kupatikana
kwa msimu ni balaa”,anasisitiza Victor Komba mkazi wa Liuli.
Komba anabainisha zaidi kuwa ziwa Nyasa
linapochafuka huwa kunakuwa na dhoruba kali na hivyo kuhatarisha maisha ya
wavuvi ambapo baadhi yao hupoteza maisha kutokana na kushindwa kujiokoa baada
ya kutumia vifaa duni.
Stephano Vumu mfanyabiashara wa samaki wa
Liuli anadai amewahi kwenda nchini Malawi
kujionea uvuvi wa samaki anadai kuwa kuna samaki wengi kwa sababu
wananchi wa Malawi wanatengeneza vyakula viwandani na kuwalisha samaki hao
jambo ambalo linafanya waendelee kuzaana kwa wingi.
Hata hivyo anadai kutokana na kutoweka kwa
samaki ziwa Nyasa upande wa Tanzania hivi sasa wavuvi na wachuuzi wa samaki
wamekimbilia upande wa Malawi wakidai upande huo kuna samaki wengi kuliko hapa
nchini .
Anasisitiza kuwa nchini Malawi wamekuwa
wakitumia vifaa vya kisasa kuvua samaki pamoja na kupiga marufuku uvuvi haramu
ambao umekuwa ukiendelea kufanyika upande wa Tanzania hasa kutokana na wavuvi
kutumia vifaa duni na ambavyo haviruhusiwi kisheria.
“Natoa wito kwa wadau wa uvuvi kuliangalia
ziwa Nyasa na mito inayoingiza maji ziwa Nyasa ukiwemo mto Ruhuhu ili kuboresha
uvuvi katika ziwa Nyasa ili sekta hiyo iweze kuwa endelevu na kuwafanya
wananchi wa mwambao mwa ziwa Nyasa kuendeleza uchumi wao na kuachana uvuvi
ambao haukubaliki”,anasema.
Barnabas Ruhumbi aliyekuwa afisa tarafa ya
Ruwekei mwambao mwa ziwa Nyasa anasema takwimu zinaonesha kuwa mavuno ya samaki
katika bandari ya Mbambabay ni chini ya tani
100 kwa mwaka mavuno ambayo ni
kidogo mno ukilinganisha na idadi ya samaki waliopo katika ziwa hilo.
Kwa upande wake mbunge wa Mbinga magharibi
Kapten John Komba anasema sekta ya uvuvi
bado ina nafasi kubwa ya kuwaendeleza wananchi wa mwambao wa ziwa Nyasa ambao kwa
kiwango kikubwa wanategemea uvuvi katika maisha yao.
Komba anasema hivi sasa amekusudia kuvalia
njuga changamoto zote ambazo zinakabili sekta ya uvuvi katika ziwa Nyasa ikwemo
kuweka mikakati ya kupata vifaa vya kisasa vya uvuvi sanjari na kupiga vita
uvuvi haramu ambao unasababisha kutoweka kwa aina mbalimbali za samaki
zilizokuwepo miaka ya nyuma.
Kulingana na utafiti ambao ulifanywa na
jumuiya ya nchi zilizo kusini mwa Afrika(SADC) kwa kushirikiana na nchi ya Uingereza kwenye ziwa Nyasa,ulionesha
kuwa ziwa hilo lina kiasi cha tani 165,000 za samaki na kati ya kiasi hicho
tani 35,000 za samaki ni jamii ya samaki wa maji ya juu ambao wanaweza kuvuliwa
bila kuathiri uvuvi kila mwaka.
Hata hivyo ofisa wa maliasili na uvuvi
katika wilaya ya Mbinga Peter Mdaki anasema kuna uwezekano wa kuongeza mapato
ya uvuvi katika ziwa Nyasa hadi kufikia tani 81,000 iwapo njia za uvuvi zitaboreshwa.
Anabainisha kuwa uvuvi ambao unaendeshwa
katika ziwa Nyasa ni ule ambao unafanyika katika maeneo yenye maji mafupi umbali
usiozidi kilometa mbili kutoka ufukweni kwa kutumia mitumbwi ya kuchongwa.
“Wavuvi katika maeneo hayo wamekuwa
wakiendesha uvuvi usio kuwa endelevu kwa
kutumia makokoro wanayoyatega ziwani kwa kutumia nyavu zenye macho chini ya
inchi tatu na kutega nyavu hizo kukinga mto Ruhuhu hivyo kuharibu mazalia ya
samaki nawaomba wananchi waachane na
uvuvi huu ambao pia sio endelevu”,alisisitiza.
Mdaki anabainisha kuwa uvuvi huo haramu
umesababisha samaki aina ya mbasa na
mbelele kuelekea kutoweka hali ambayo inadidimiza uchumi wa wakazi wa
mwambao mwa ziwa Nyasa ambao wanategemea uvuvi kuendesha maisha yao.
Amesisitiza kuwa uvuvi ambao unafanywa
ufukweni mwa ziwa hilo kwa kutumia nyavu
za kokoro,vyandarua vya kuzamia na kutega nyavu ambazo zina macho chini ya
inchi tatu sio uvuvi endelevu kwa kuwa zinaharibu mazalia ya samaki na kuua
samaki wenye umri mdogo.
Anasema pamoja na elimu kutolewa mara kwa
mara kwa wananchi kuhusu kuepukana na uvuvi usiokuwa endelevu,bado wananchi
mwambao mwa ziwa hilo wanaendelea na uvuvi haramu hali ambayo inaharibu mazalio
ya samaki na kusababisha aina mbalimbali za samaki kuanza kutoweka kwa kasi.
Uchunguzi umebaini kuwa wavuvi wanaokamatawa
kwa kuendesha uvuvi usiokuwa endelevu wamekuwa wakimudu kulipa faini ambazo
zinatozwa na serikali kupitia
mahakama na kuonekana kuwa na hatia hali
ambayo inafanya wavuvi hao kuendeleza
aina hiyo ya uvuvi licha ya kupigwa marufuku na kisheria.
Baadhi ya mambo ambayo yanaendeleza uvuvi
usiokuwa endelevu kuwa ni pamoja na
utoaji wa rushwa kwa maofisa uvuvi wasiokuwa waaminifu hivyo kuruhusu wavuvi
haramu kuendelea kulihujumu taifa hali ambayo inaangamiza mazalio ya samaki na
kuhatarisha samaki kutoweka.
Uvuvi haramu unaathiri kizazi cha sasa na
kijacho hivyo inatakiwa watu wote ambao wanaendesha uvuvi haramu kufichuliwa
ikiwa ni pamoja na watumishi wa maliasli na utalii ambao wanashikiliana na
wavuvi haramu haona hivyo kuokoa maisha ya samaki ambao wataendelea kuzaana kwa
wingi na hivyo kuboresha maisha ya wavuvi na taifa kwa ujumla wake.
albano.midelo@gmail.com,simu
0766463129



Duh! itakuwa tatizo kubwa sana kwa kweli kwa sisi wanyasa tunakula samaji tu....
ReplyDelete