Thursday, April 5, 2012

Songea Girls waathirika na sumu ya wadudu

Afisa elimu wa mkoa wa Ruvuma Paulina Mkonongo
Na Albano Midelo,Songea
WANAFUNZI wa shule ya sekondari ya wasichana Songea mkoani Ruvuma wameathirika na sumu inayotolewa  na wadudu waitwao Nairobi flies hali iliyosababisha kutokwa na vidonda sehemu mbalimbali za mwili.
Risala ya jumuiya ya shule hiyo iliyosomwa katika sherehe ya mahafali ya 13 ya kidato cha sita ilieleza kuwa  wadudu hao wenye sumu wamekuwa  ni tatizo hasa katika kipindi cha kuanzia mwezi Desemba hadi Mei kila mwaka na kusababisha  vidonda baada ya kutua hasa sehemu za uso za wanafunzi.
Risala hiyo ilizitaja changamoto nyingine ambazo inawasumbua wanafunzi hao kuwa ni kuharibika kwa miundo mbinu ya maji safi na maji taka kutokana na uchakavu,uchakavu wa majengo mbalimbali yakiwemo bwalo la chakula, mabweni, adarasa,vyoo na madarasa na ukosefu wa maktaba inayokidhi mahitaji ya kitalaaluma.

Naye mwakilishi wa mkuu wa shule hiyo Weaner Likiliwike  alibainisha  shule hiyo kongwe iliyoanzishwa mwaka 1974 yenye wanafunzi wa kidato cha tano na sita inakabiliwa na ukosefu wa walimu wa masomo ya Sayansi yakiwemo Biolojia,Kemia na Fizikia.
“Hali ya taaluma katika shule yetu imekuwa ya kupanda na kushuka ,hii ni kutokana na upungufu wa walimu katika masomo ya Sayansi,wanafunzi wengi wanaofeli  ni wanaosoma masomo ya Sayansi,pia vifaa katika maabara ni duni’’,alisistiza Likiliwike.
Jumla ya wanafunzi 295 walipewa vyeti vya kuhitimu kidato cha sita kwenye mahafali hayo ambayo mgeni rasmi alikuwa mstahiki meya wa manispaa ya Songea Charles Mhagama.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129



No comments:

Post a Comment