Wednesday, April 18, 2012

Tanzania ina wajinga milioni 5.5


Na Albano Midelo
TANGU  tupate uhuru,historia ya nchi yetu inaonesha kuna mambo mengi mazuri yaliowezwa kufanywa katika utekelezaji wa sera na mipango ya elimu ya watu wazima.

 Mwaka 1968 Tanzania ilikuwa ni miongoni mwa nchi 12 ulimwenguni zilizochaguliwa na shirika la umoja wa mataifa la Elimu,Sayansi na Utamaduni yaani UNESCO kufanya mradi wa majaribio ya kutumia mbinu mpya ya kisomo chenye manufaa katika kufundisha watu wazima kusoma,kuandika na kuhesabu.


Baba wa Taifa hayati mwalimu Julius Nyerere aliutangaza mwaka 1970 kuwa mwaka wa Elimu ya watu wazima,tangazo hilo la mkuu wa nchi wakati huo likaufanya mwaka huo kuwa mwanzo wa harakati za kufuta ujinga nchini .

Mwaka 1974 na mwaka 1975 Tanzania iliweza kuandikisha watu wasiojua kusoma wapatao milioni 4.5 kwenye madarasa ya kisomo cha watu wazima na hivyo baada ya muda mfupi Tanzania ilifanikiwa kufuta ujinga wa kutojua kusoma kutoka asilimia 69 mwaka 1970 hadi kufikia asilimia 39 mwaka 1975.

Kana kwamba haitoshi historia ya elimu ya watu wazima inaonesha kuwa ilipofika Agosti mwaka 1975 Tanzania ilikuwa ni nchi ya kwanza ulimwenguni kufanya mtihani wa kisomo kwa watu wazima wapatao zaidi ya milioni 3.8 ambao walikuwa ni asilimia 77 ya wote waliokuwa wanahudhuria kwenye madarasa ya kisomo.

Hata hivyo mwaka 1981 Tanzania ilikuwa ni ya kwanza katika nchi za ulimwengu wa tatu kuanzisha kampeni ya kitaifa ya kisomo cha kujiendeleza iliyohusisha watu wazima zaidi ya milioni 1.4 waliofuzu kisomo katika hatua ya nne.

Kwa mujibu wa taarifa ya kitaifa ya elimu ya watu wazima mnamo mwaka 1986 Tanzania ilifanikiwa kupunguza  idadi ya watu wazima wasiojua kusoma hadi kubakia zaidi ya milioni 1.36 ambao walikuwa sawa na asilimia 9.6.

Hata hivyo kutokana na kushuka kwa kwa hali ya uchumi na baadhi ya wafadhili kusitisha misaada ya kuendeleza elimu ya watu wazima,uwezo wa taifa uliyumba  kutekeleza mipango ya elimu ya watu wazima baada ya programu hiyo kukosa mafungu ya fedha,vifaa na nyenzo muhimu za uendeshaji.

Ingawa hivi sasa juhudi zimeanza upya na mipango thabiti imeandaliwa kufufua upya kisomo cha kujiendeleza,uchunguzi umebaini kuwa taifa letu limo katika tatizo kubwa la ujinga wa kutojua kusoma na kuandika kuliko wakati mwingine wowote katika historia ya Tanzania.
Kwa mujibu wa matokeo ya sensa iliyofanyika mwaka 2002 na matokeo ya tafiti mbalimbali,inakadiriwa kuna  watu wazima milioni 5.5  sawa na asilimia 32 ambao hawajui kusoma,kuandika na kuhesabu.

Tafiti hizo zinaonesha kuwa hivi sasa hatukabiliwi na tatizo la watu wazima wasiojua kusoma,kuandika na kuhesabu pekee bali pia kuna idadi kubwa ya vijana wa miaka kati ya 11 na 18 ambao ama hawakuandikishwa shuleni au wameacha shule hivyo hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu.

Kundi hili la vijana ni nguvukazi kubwa ya Taifa ambao wangeweza kuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi ,hata hivyo kutokana na kutojua kusoma,kuandika na kuhesabu vijana hao hawatatoa mchango wowote wa maana iwapo taifa litawaacha kuendelea kubakia katika hali ya ujinga.

Wataalamu uhusisha elimu hafifu na umasikini,upeo mkubwa wa elimu na utajiri.uchunguzi umebaini kuwa sehemu ambazo idadi kubwa ya watu wana elimu ndogo kiwango cha umasikini ni kikubwa na maeneo ambayo wananchi wengi wana elimu ya kutosha huwa na maendeleo mazuri.

 Serikali kupitia wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi inasisitiza na kuwahimiza wananchi kutokomeza tatizo la kutojua kusoma,kuandika na kuhesabu ili kuwaondoa katika hali duni inayotokana na ujinga na kuwawezesha kwenda katika hali nzuri zaidi ili kujikomboa kimaisha.

Huwezi kujinasua katika wimbi la umaskini bila kupata elimu bora hivyo njia pekee ya kujinasua katika tatizo la kukosa elimu  ni kwa mtu yeyote mwenye tatizo hilo kuamua kujiunga na darasa la kisomo cha watu wazima katika shule za msingi .

Licha ya wimbi kubwa la watanzania kutojua kusoma,kuhesabu na kuandika bado wananchi wanajua kusoma,kuandika na kuhesabu  wana mambo mengi wasiyoyajua ambayo ni muhimu kwa maisha yao ambayo wanapaswa kujifunza katika madarasa ya kisomo cha elimu ya watu wazima kutokana na ukweli kuwa elimu ni bahari na kuishi ni kujifunza.

Hivi sasa dunia  imepiga hatua kubwa katika maendeleo ya sayansi na teknolojia,ni wale tu ambao wana elimu ndio watakaoweza kufaidi matunda ya sayansi na teknolojia na wale ambao hawana elimu watabakia kuwa watazamaji tu hivyo basi kundi kubwa ambalo halijui kusoma,kuandika na kuhesabu lililopo hapa nchini lina kila sababu ya kujikomboa kutoka katika hali hiyo ili hatimaye waweze kufaidi matunda ya kuwa na elimu katika ulimwengu huu wa utandawazi.albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129








No comments:

Post a Comment