Na Albano
Midelo
HATIMAYE waumini wote
sasa wanaruhusiwa kugusa na kufanya maombezi kwenye masalia ya mtumishi wa
Mungu Sr.Bernadeta Mbawala baada ya masalia hayo kuhifadhiwa ndani ya kanisa
kuu la mtakatifu Mathias Kalemba mjini hapa.
Zoezi la kuyahamisha
masalia hayo kutoka katika kanisa la Askofu mkuu uaskofuni jimbo kuu la Songea
ambako yalihifadhiwa kwa muda na kuyapeleka katika sehemu maalum ndani ya
kanisa kuu la kiaskofu kulifanywa Jumapili hii na Askofu
mkuu wa jimbo kuu la Songea mhashamu Norbert Mtega.
Askofu mkuu Mtega
alifanya zoezi hilo baada ya adhimisho takatifu la misa ya tatu kwenye kanisa
kuu hilo ambapo waumini walijipanga kwenye mistari hadi ndani ya kanisa dogo la
kiaskofu ambako mhashamu Mtega aliongoza waumini kutoa heshima nakugusa sanduku la masalia ya
mtumishi wa Mungu Sr.Bernadeta kisha waumini walianza kubeba sanduku hilo
katika maandamano kurudi ndani ya kanisa kuu.
Akizungumza mara
baada ya zoezi la kuhamisha masalia hayo kukamilika na kuhifadhiwa katika jengo maalumu ndani ya kanisa kuu,mhashamu
Mtega alibainisha kuwa sasa waumini wote wanaruhusiwa kufika katika eneo hilo
na kugusa mahali yalipohifadhiwa masalia
hayo pamoja na kufanya sala za maombezi kupitia mtumishi huyo waMungu.
“Sasa tumekwisha
kuweka masalia ya mtumishi wa Mungu hapa kanisani hadharani,tangu sasa tutaanza
kutoa heshima kwake na yeyote ambaye ataingia hapa kanisani anataka kusali
katika masalia haya atakuja hapa wakati wowote ambapo tutaacha wazi ili muumini
siku yeyote anaweza kugusa na kusali katika masalia ya Sr.Bernadeta Mbawala.
Askofu mkuu mtega
katika nafasi hiyo amewashukuru waumini wa kanisa kuu hilo kujitolea kujenga
eneo maalumu ndani ya kanisa kwa kutumia sadaka za waumini wenyewe kwa ajili ya
kuhifadhi masalia ya mtumishi wa Mungu Sr.Bernadeta.
“Tangu sasa mtumishi
wa Mungu Sr.Bernadeta Mbawala atakuwa nanyi ndani ya kanisa hili akiwaombea na
kuweza kusali na kumutuza Mungu pamoja nanyi,atawaombea katika shida zenu zote yakiwemo
mateso na magonjwa mbalimbali kupitia maombezi yake ‘’,alisema askofu mkuu
Mtega. Uzinduzi wa mchakato wa kumtangaza
mtumishi wa Mungu Sr.Bernadeta Mbawala kuwa Mwenyeheri ulizinduliwa
rasmi na Askofu mkuu wa jimbo kuu
katoliki la Songea mhashamu Norbert Mtega katika kanisa kuu la kiaskofu la
mjini Songea mapema mwaka huu.
Mwenyekiti wa parokia
ya Songea John Komba alisema jengo hilo maalum la kuhifadhia masalia ya
mtumishi wa Mungu Sr.Bernadeta Mbawala lililojengwa ndani ya kanisa kuu la
mtakatifu Mathias Kalemba limegharimu shilingi milioni mbili ambazo ni sadaka
za waumini pamoja na kazi za kujitolea hadi kukamilisha ujenzi huo kwa muda
mfupi.
Padre Joseph Mgaya wa
seminari kuu Peramiho msemaji wa mchakato huo amethibitisha masalia ya mtumishi
wa Mungu Sr.Bernadeta Mbawala kuhamishiwa katika sehemu ya wazi ndani ya kanisa
kuu la mtakatifu Mathias Kalemba na kusisitiza kuwa sasa waumini watakuwa na
fursa nzuri ya kugusa na kufanya maombi.
“Siku ya Jumamosi
yaani siku moja kabla ya kuhamisha masalia hayo toka kanisa dogo la uaskofuni
ambako yalikuwa yamehifadhiwa kwa muda,baadhi ya wanakamati wa mchakato tulifanya ukaguzi katika eneo
ambalo kimejengwa kibanda maalum ndani ya kanisa tuliridhika na kuidhinisha
masalia hayo kuwekwa hap kanisani mahali pa wazi’’,alisisitiza.
Hata hivyo padre
Mgaya ametoa wito kwa waumini ambao wanataka kutoa ushuhuda wa mtumishi wa
Mungu Sr.Bernadeta kuendelea kujiandikisha kwa maparoko katika ofisi zote za parokia na kwamba kamati inaendelea kukutana na watoa ushuhuda
na kufanya mahojiano ya ana kwa ana.
Baadhi ya waumini
ambao walishiriki katika misa maalum ya kuhamisha masalia hayo hadi mahali pa
wazi ndani ya kanisa kuu la mtakatifu Mathias Kalemba wamefurahisha na kitendo
cha kanisa kuyaweka masalia hayo mahali ambapo kila mmoja anapata fursa ya
kugusa na kufanya maombezi.
Agnela
Kimanga,Christina Kayombo na Editha
Sangana wakazi wa Lizabon mjini hapa
wamesema walikuwa wanatamani kugusa na kufanya maombi kwenye sanduku la
Sr.Bernadeta lilipohifadhiwa katika kanisa la uaskofuni ,lakini walikuwa
wanaogopa na kwamba sasa wanaweza kugusa wakati wowote kwa kuwa masalia hayo
yapo mahali pa wazi kanisani.
Kiongozi limeshuhudia
waumini wakimiminika katika kanisa kuu la mtakatifu Mathias Kalemba kila siku
kanisa linapokuwa wazi kwa lengo la kugusa na kufanya maombezi kwenye sanduku
la Sr.Bernadeta mara baada ya masalio hayo kuhamishiwa katika kanisa hilo
Jumapili iliyopita
Makao makuu ya kanisa
katoliki Vatican yametoa ruhusa kwa
jimbo kuu katoliki la Songea kuanza mchakato wa utafiti kuhusu maisha,fadhila za uhodari,sifa ya
utakatifu na nguvu za kimaombezi za Sr. Bernadeta Mbawala ili aweze kutangazwa
kuwa mwenyeheri na hatimaye mtakatifu.
Sr. Bernadeta Mbawala
aliyezaliwa Oktoba 27,1911 katika kijiji cha Likuyufusi wilayani Songea
mkoani Ruvuma alifariki Novemba 29,1950
na kuzikwa katika makaburi ya Abasia ya
Peramiho ambapo mapema mwaka huu masalia yake yalifukuliwa kwa lengo la kuanza
mchakato wa kutangazwa mwenyeheri kisha mtakatifu.
albano.midelo@gmail.com,simu 0766463129

No comments:
Post a Comment